Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na mimi katika hotuba hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza Serikali hasa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa yale ambayo amekuwa akiyatenda na haya ambayo yameelezwa katika bajeti ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhahiri kama ambavyo mara nyingi nimekuwa nikizungumza humu ndani. Mwaka 2025 Chama changu cha Mapinduzi hakitakuwa na kazi ya kumrejesha Mheshimiwa Dkt. Samia madarakani Wabunge wote wa Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa ambayo inaendelea kufanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba nichangie katika masuala yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, katika sekta ya Miundombinu, napongeza kwa jitihada ambazo zinaendelea kufanyika. Ningeomba sasa Ofisi ya Waziri Mkuu katika bajeti yake hii ione umuhimu wa kuleta mabadiliko ya Sheria ya Manunuzi ili kuruhusu Sekta ya Miundombinu iwe kama Sekta nyingine za kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sifurahishwi sana kuona mpaka leo bado tunajenga barabara mfano za Mwendokasi kupitia fedha ambazo zinatafutwa na Rais Samia na Serikali yetu. Kama tumetoa fursa kwa wafanyabiashara wakaweza kuja kujenga viwanda, tukawapa vivutio mbalimbali vya kodi, wakajenga viwanda wakazalisha ndani ya Tanzania, watanzania wakaajiriwa, Serikali ikapata kodi, kwa nini tunashindwa kutoa fursa kama hizo kwa wawekezaji wakajenga miundombinu hasa ile ya mwendokasi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu barabara ya mwendokasi inapojengwa sio watanzania wote na magari yao wanaruhusiwa kutumia ni magari maalumu. Kwa hiyo, ni magari maalumu ambayo yanapita na kufanya biashara katika barabara hiyo. Sasa kwa nini Serikali isitangaze kwa wenye fedha duniani wakaja wakajenga barabara za mwendokasi ili fedha ambazo zingekwenda kujenga barabara zikatumika kwa shughuli nyingine kama vile kuhudumia hospitali zetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo jambo sio geni na huko duniani lipo. Serikali yetu ilitupa nafasi sisi tulikwenda kujifunza nje. Huko duniani ziko bandari zimejengwa na watu kwa asilimia 100 na Serikali inakusanya kodi tu. Sasa kwa nini katika sekta ya miundombinu tusiende huko katika kuleta vivutio kama tulivyoleta vivutio katika sekta ya viwanda? Ningetamani kuona katika suala la bandari ya Bagamoyo linakwisha na kuanza kujengwa kupitia wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli inawezekana tumekosea sasa je, tumekosea ndio tuache ibaki hivyo hivyo? Tuache tusiwe na bandari kubwa Zaidi? Makosa yaondoshwe Sheria iletwe katika Bunge hili tuone namna inavyoweza kubadilishwa basi Bandari ya Bagamoyo na Bandari nyingine ziweze kujengwa kupitia sekta binafsi kwa maslahi ya taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba sasa pia nizungumzie suala katika Manispaa hasa zile asilimia 10 zinazohusu vijana wenzangu akina Mama pamoja na Watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwanza nikupe taarifa nina miaka 32 hivi karibuni nitatimiza miaka 33, kwa hiyo bado ni kijana na nina maslahi makubwa sana na vijana katika Taifa hili pamoja na Wananchi wangu wa jimbo la Mtoni. Fedha zile ambazo zinakopeshwa asilimia 10 mara nyingi ukopeshwaji wake hauleti matokeo mazuri. Nafasi hii niitumie kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuelekeza fedha hizi zianze kutolewa kupitia Mfumo wa Kibenki. Hata hivyo, Mheshimiwa Rais amesema suala hilo litafanyika katika bajeti ya Serikali ijayo bajeti ya mwaka 2024/2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, fedha hizi katika bajeti hii ambayo tunaendelea nayo zimetengwa kuendelea kusimamiwa na Halmashauri. Nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu kama Msimamizi Mkuu wa Serikali basi fedha hizi katika mwaka 2023/2024 zisije zikatumika kama kiinua mgongo kwa wale watu ambao wamekuwa wakigawana na vikundi vyao kwa sababu wanajua baada ya hapo zitaanza kutumika kupitia Benki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya mwaka 2020/2021 ilionesha kwamba takribani Shilingi bilioni 47 katika halmashauri 155 katika hizi fedha za asilimia 10 zimeshindwa kukusanywa kurejeshwa. Maana yake nini? Bilioni 47 zingekusanywa wangekopeshwa vijana kila mmoja mwenye uwezo wa kufanya Biashara Milioni 100 maana yake tungetengeneza Mamilionea 470 wakasimamiwa na halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri zote zina maafisa biashara. Laiti Maafisa biashara wangeweza kusimamia kuwasaidia wafanyabiashara sio tu kuwakimbiza pale wanapokuwa hawajakata leseni labda tungekuwa na wafanyabiashara wakubwa wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa fedha hizi katika bajeti hii ya mwaka 2023/2024 kwa sababu ndio itakuwa ya mwisho kusimamiwa moja kwa moja na halmashauri kufuatia maelekezo ya Mheshimiwa Rais, basi Ofisi ya Waziri Mkuu ikazisimamie lasivyo nitakapokuja hesabu ya Maguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka huu 2023/2024 ambao tunapitisha bajeti yake itakuja na matatizo yale yale. Ningetamani kuona Ofisi ya Waziri Mkuu inakwenda kuzisimamia ili nione Mamilionea vijana kutokana na fedha ambazo zinatengwa na halmashauri yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa suala la vyama vya siasa. Nitumie nafasi hii kuomba bajeti ya Waziri Mkuu wale ambao wanasimamia masuala ya vyama vya siasa watenge muda zaidi kuvipa Elimu na kuvikumbusha vyama vya siasa umuhimu wa Demokrasia. Mheshimiwa Rais ametuonyesha njia umuhimu wa ustahimilivu, umuhimu wa kusikiliza sasa na wao wawe wastahimilivu na wawe wenye kusikiliza. Hata hivyo, hivi vyombo ambavyo vinasimamia vyama vya siasa vitimize wajibu huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda tukumbushane humu ndani, mwaka 2015 watanzania waliamua Kumchagua Dkt. John Pombe Magufuli na Rais Samia ambaye yuko sasa madarakani kama Makamu wake wa Rais. Watanzania hao hao waliamua kuchagua Wabunge wengi wa upinzani pia na waliamua kuchagua Wabunge wengi zaidi wa CCM lakini mwaka 2020 Watanzania waliamua Kuchagua Wabunge wa CCM wengi zaidi kwa sababu ya yale yaliyotendwa na Serikali iliyokuwa madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa vyama vya siasa kama ambavyo vilifurahia na hasa vya upinzani vilivyopata Wabunge wengi mwaka 2015 vijifunze kustahimili Watanzania wakiendelea kuiamini CCM.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyotangulia kusema awali, kwa mwendo wa Rais Samia hakuna pahala katika Taifa hili ambapo hajaweka mkono. Dhahili, Wabunge wa Chama cha Mapinduzi mwaka 2025 watatawala katika viti vyote vya Bunge hili kwa sababu watanzania watawaamini.

Mheshimiwa Naibu Spika, wale wenye kusimamia vyama vya siasa wakae watukumbushe viongozi wa Chama Tawala na vyama vingine kwamba kushindwa katika uchaguzi Mkuu ni matokeo na baada ya kushindwa wasije wakatumia nafasi hiyo kuwafitinisha watanzania maana baada ya uchaguzi watahitajika kuendelea kulijenga taifa lao. Hata hivyo, wakati wa kuwakumbusha pia wawasomee basi katiba ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 5 ili mioyo yao iwe na amani pale mambo yoyote yatakapotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo nakushukuru sana naunga mkono hoja hii. (Makofi)