Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nachukua fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika hotuba ya bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ya mwaka 2016/2017 kwa kauli na maandishi. Namshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya KUdumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Mheshimiwa Peter Serukamba, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Vijijini, kwa maoni na ushauri wa Kamati yake katika hotuba ya bajeti ya Wizara yangu ya mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, namshukuru sana rafiki yangu, Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Joseph Mbilinyi (Sugu), kwa mchango wake katika hotuba yangu. Mheshimiwa Mbilinyi ni mdau mkubwa na muhimu katika tasnia ya sanaa ya muziki, hivyo kuimarika kwa tasnia hii kunamgusa moja kwa moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba michango yote ya Waheshimiwa Wabunge inalenga kuimarisha na kuendeleza sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo ili iweze kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya Taifa letu, kuzalisha ajira hususani kwa vijana, vilevile kuendeleza utamaduni, mila na desturi za Mtanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba yangu imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa Wabunge 41 ambapo waliochangia kwa maandishi ni Waheshimiwa Wabunge 22 na kwa kauli ni Waheshimiwa Wabunge 19. Majibu na ufafanuzi nitakaoutoa umezingatia hoja zilizotolewa na Kamati ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, hotuba ya Kambi ya Upinzani Bungeni na hoja za Waheshimiwa Wabunge zilizotolewa kwa kauli na maandishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hoja ya mwisho, mwisho. Kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanasema, Mheshimiwa Nape ni katika wanasiasa wachache vijana wanaochukiwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli mafisadi wananichukia sana, ni kweli wasiopenda ukweli wananichukia sana, lakini wapo Watanzania wengi wakiongozwa na wananchi wangu wa Jimbo la Mtama, wananipenda sana na wananiamini kwa msimamo wangu wa kuwa mkweli hata pale ambapo ukweli unauma. Kwa hiyo, katika majibu nitakayoyatoa hapa, yako majibu mengine yanauma kwa baadhi ya watu lakini nitaomba tuvumiliane. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, imekuwepo hoja hapa ya kuhoji wadau wa Wizara hii wamekujaje Dodoma? Nataka nichukue nafasi hii kuwashukuru sana kwa dhati wadau waliokuja kutuunga mkono kwenye hotuba hii kwa sababu wadau hawa wamejitolea kwa pesa zao mfukoni, kwa uzalendo wao na mapenzi yao kwetu, wakajitolea kuja Dodoma. Hakuna senti tano ya Wizara iliyotumika kuwaleta Dodoma. Nawashukuru sana wadau wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichofanya ni jambo rahisi sana. Hawa wadau wako Dodoma, akina Mzee King Kiki wako Dodoma, tukawaomba kwa uzalendo huo huo wapate muda wa saa chache kuja kutoa burudani hapa Bungeni. Hakuna dhambi ya wao kufanya hivyo. Wamejitolea wenyewe, badala ya kuwasema, badala ya kuwakashifu, badala ya kuwasemea maneno mabaya ya kuwavunja moyo nilidhani tuwapongeze kwa uzalendo wao na moyo wao. Kwa hiyo, Mzee King Kiki na wenzako nawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuwatangazia Waheshimiwa Wabunge kwamba baada ya kumaliza kazi hii nzuri twendeni pale tukacheze muziki vizuri, tufurahi pamoja. Hili haliwezi kuwa rushwa, hii ni Wizara ya Sanaa; Wizara ya Burudani. Baada ya kazi tunaburudika. Kazi na dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye jambo la pili ambalo nalo limezungumzwa sana. Nadhani ni vizuri nikazungumza mambo machache. Tumelizungumza kwa muda mrefu ndani ya Bunge letu, nalo ni suala la uhuru wa vyombo vya habari na hasa hili suala la Bunge live. Nadhani nigusie kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, uamuzi wa kuanzisha studio ya Bunge siyo uamuzi wa Mheshimiwa Nape kama Waziri, siyo uamuzi wa Serikali, ni uamuzi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Serikali haina mkono wake. Wanaonyoosha mikono, vidole na kusema Serikali, Serikali, nataka nirudie, huu ni uamuzi wa Bunge, ulipitishwa Bungeni hapa, ukatengewa pesa wakati Serikali ya Awamu ya Tano na Mheshimiwa Nape akiwemo, tulikuwa bado hatujawa wala Wabunge hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, leo kunyoosha kidole kwa Serikali kwa uamuzi uliopitishwa na Bunge hili, siyo sawasawa hata kidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, mara kadhaa nimekuwa nikisimama hapa Bungeni kulifafanua jambo hili, siyo kwa sababu jambo hili ni la Serikali, lakini kwa sababu Wizara yangu ndiyo yenye dhamana ya kusimamia Sera ya Habari; kwa hiyo, inapofikia mahali mambo yanapotoshwa kwa makusudi tunadhani tuna umuhimu wa kusimama na kufafanua. Leo nitazungumza ambayo sijawahi kuyazungumza, niyatolee ufafanuzi kwa uchache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, kuna watu wanasema uamuzi huu umevunja Katiba na kwa kweli maana yake umevunja sheria. Wizara hii inasimamia Sheria na Kanuni za Utangazaji hapa nchini na nitawasomeeni. Kanuni ya Utangazaji Namba 13(1) nitainukuu kama inavyosema na inasema hivi, ni ya kiingereza: “A licensee shall be free to cover Parliamentary sessions subject to laid down Parliamentary rules, regulations, procedures and on Parliamentary broadcasting.” Hii ndiyo Kanuni ya Utangazaji ambayo Wizara yangu inaisimamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tafsiri rahisi inasema; “Chombo cha utangazaji kitatangaza matangazo ya Bunge kwa kuzingatia taratibu, sheria na kanuni zitakazowekwa na Bunge.” Siyo la Serikali; na Bunge lenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama kuna lolote linafanyika, halijapangwa na Serikali, Kanuni inalitaka Bunge ndiyo lipange namna gani vikao vyake vitarushwa na vyombo vya habari. Hii Serikali kuingizwa kwenye hili tunatoka wapi? Mimi nadhani tukae upya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, kama wasimamizi wa Sera ya Habari, tuliposikia kelele zinakuwa nyingi, mimi kama Waziri nilikwenda Mwanza kuhudhuria shughuli ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani. Nikiwa Mwanza nikasema hadharani, wanahabari ziko kelele juu ya jambo hili, sisi kama Serikali wasimamizi tuko tayari kusimama katikati ya Bunge na wadau tuzungumze upungufu wowote uliopo kwenye huu mfumo wa utangazaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyoongea, wako wadau zaidi ya ishirini na kitu wakiongozwa na Jukwaa la Wahariri, wako hapa Dodoma leo siku ya tano, wanazungushwa kwenye studio ya Bunge, wanaongea na uongozi wa Bunge na mimi niliwashauri; ongeeni na uongozi wa Bunge, piteni kwenye studio ya Bunge, zungumzeni na wadau, wekeni mezani upungufu mnaouona halafu sisi Serikali tutakaa katikati yenu na Bunge tuzungumze upungufu uliopo. Hiyo ndiyo kazi yangu, huo ndiyo wajibu wangu na huo nautimiza na ndiyo maana wadau wako hapa. Juzi nilikutana nao, tumekaa nao mpaka saa 9.00 usiku, leo watu wananinyooshea vidole, Nape, Nape, Nape, Nape! Eeh!
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI SANAA NA MICHEZO: No, no, no! Lazima tuambiane ukweli, maana hili jambo mnalipigia kelele sana. Ni vizuri tukaambiana ukweli. Mliamua wenyewe, mmepitisha wenyewe, mmetenga pesa wenyewe; kama yako matatizo, kaeni chini yatatueni. Kanuni inataka Bunge hili ndilo lipange namna ya kurusha hiyo studio yenu. Studio hiyo siyo mali ya Serikali, studio hiyo ni mali ya Bunge. Tafadhali twendeni taratibu. (Makofi)
La nne, naona yako mengi katika hili, lakini labda la nne nizungumze. Ni vizuri, maana wakati mwingine tunabebeshana mizigo isiyokuwa na sababu. Kuna maneno yanazungumzwa na shemeji yangu na bahati nzuri wako shemeji zangu wengi Wakurya huku; shemeji yangu Mheshimiwa Mwita alisema kwamba unajua hili Bunge lenyewe linaonyeshwa mpaka saa 9.00 usiku. Mimi nawashauri Waheshimiwa Wabunge, studio ziko hapa nyuma; chukueni muda mchache nendeni mkatembelee pale, muwaulize namna gani studio inafanya kazi? Wanaoonyesha mpaka usiku, wameamua wenyewe; kituo kimeamua na hao ni TBC wameamua waonyeshe kila kitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini viko vituo ambavyo vinaonyesha mwisho saa 3.00 na saa 3.00 ndiyo mwisho wa studio hii kurusha matangazo yake. Sasa kwa sababu ume-concentrate na kituo kimoja kinaitwa TBC ambacho pia bahati mbaya baadhi ya Waheshimiwa Wabunge humu humu huwa wanasema TBC bwana, Mbunge mmoja alikuwa anasema wala sikumbuki mara ya mwisho nimeiona lini, lakini akisimama hapa, kwa nini umeifungia?
Sasa namwambia wewe hukumbuki mara ya mwisho umeiona lini, lakini unapigia kelele kwa nini imefungiwa! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema pateni muda, nendeni pale mkaangalie inavyofanya kazi. Inarusha matangazo yake studio hii mwisho saa tatu. Ina delay ya saa moja. Dada yangu Mheshimiwa Minja, hii ni practice ya Mabunge ya Commonwealth.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda Mabunge ya Commonwealth, na mimi mifano ninayo ya kutosha. Sitaki kuwa msemaji wa studio hiyo, lakini nadhani ni vizuri Waheshimiwa Wabunge, studio si ziko hapa, nendeni mkaangalie. Dunia ya leo iko mikononi, just google Commonwealth practice ikoje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye uhuru wa vyombo vya habari, la pili kutoka mwisho, kuna hoja imezungumzwa na rafiki yangu Mheshimiwa Sugu, kama vile hii nchi inaongoza kwa kuvunja haki za vyombo vya habari na kukandamiza uhuru wa vyombo vya habari. This is not right! Hebu tufike mahali tuwe fair, kama kuna mahali pa ku-improve semeni, ongezeni hapa na hapa, badala ya ku- condemn kama vile hakuna kinachofanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Sugu anatoa taarifa hapa, akieleza kwamba sisi tumekubuhu kwa kuvunja haki za uhuru wa vyombo vya habari, waandishi wa habari, Shirika la Waandishi wa Habari wasiokuwa na Mipaka, wametoa ripoti yao mwezi wa nne wanasema hivi, wamefanya utafiti kwa nchi 180, katika nchi 180 duniani, Tanzania ni nchi ya 71 duniani; tumewazidi wakubwa wengi sana. Kwa Afrika, Tanzania ni nchi ya 11, lakini Afrika Mashariki Tanzania ni ya kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti imetolewa juzi mwezi wa nne na ni ripoti imefanywa na Shirika la Waandishi wa Habari Wasiokuwa na Mipaka na vyombo vya habari vya Tanzania vimenukuu ripoti hii. Nilipokwenda kwenye Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani, wenyewe waandishi wa habari walikuwa wakizungumza ripoti hii. Utafiti umefanyika, ripoti imetolewa na huo ndiyo ukweli. Kwa hiyo, tunapoangalia upande mmoja, twendeni na upande wa pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni upande wa habari. Kuna hoja hapa zinatolewa, kwamba sisi tumeleta hotuba hapa Bungeni ambayo haijali kabisa waandishi wa habari, maslahi yao, haki zao na kila kitu, tumepuuza. Dada yangu Mheshimiwa Minja, mimi ni mwandishi wa habari. Degree yangu ya kwanza ni ya uandishi wa habari na nimeisotea miaka mitatu, sikupewa, nimesoma! Kwa hiyo, tasnia ya habari iko ndani ya damu yangu, sijakurupuka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii kwenye hotuba tumesema, katika mipango, mpango wa kwanza tutakaofanya mwaka wa fedha 2016/2017 ni kuboresha mazingira ya tasnia ya habari kwa kukamilisha mchakato wa utungaji wa Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari. Ndani ya muswada ule, haki zote zinazozungumzwa tumeziweka mle.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muswada ule uliletwa, ukapigiwa kelele, ukatolewa, tumerekebisha, tunatengeneza mchakato, ukikamilika tumeahidi mwaka huu wa fedha wa 2016/2017 tutauleta Bungeni. Wenye uchungu mzuri tupitisheni huo Muswada. Ukipita, una majibu ya changamoto nyingi sana ikiwemo nani mwandishi wa habari. Maana yake leo kila mmoja anasema ni mwandishi wa habari, mpaka makanjanja wanasema ni waandishi wa habari. Matokeo yake tasnia inafika mahali inakosa heshima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweke heshima lazima tutafsiri nani mwandishi wa habariwa kweli. Mmezungumza kuhusu habari ya elimu; dunia ya leo huwezi ukapuuza elimu. Mbona madaktari wameweka viwango? Mbona wanasheria wameweka viwango? Kwa nini leo waandishi wa habari tusiweke viwango?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kazi zetu ziwe na weledi, ni lazima tuweke viwango vya elimu ili tufike mahali tulipane vizuri. Kwa hiyo, Muswada ule ukija uta-take care haya yote yaliyozungumzwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndiyo nilikuwa juu kidogo, sasa twende taratibu, kuna hoja ya maudhui, kuna hoja ya haki, mkwe wangu ananiambia ninywe maji.
Tutulie kidogo eeh! Nakushukuru Mheshimiwa Sugu. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya kujali muziki wa ndani, upande wa sanaa. Tunayo sheria inayosimamiwa na TCRA, inazungumzia habari ya asilimia 60 ya maudhui ya ndani (local content). Bahati mbaya kanuni hii imejumlisha maudhui yote yakiwemo habari, vipindi, muziki na vitu vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utekelezaji wake umekuwa na matatizo. Matatizo yake nini? Uzalishaji wa vipindi vya ndani, vile vya kawaida ambavyo siyo vya muziki una gharama kubwa. Practice inaonyesha hili jambo limekuwa gumu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunapitia upya kanuni hizo na mwenye dhamana hiyo ni mimi. Tunapitia kanuni hizo na moja ya jambo tulilolipendekeza kwenye kanuni ni kutenganisha maudhui ya vipindi vingine na maudhui ya muziki ambapo uzalishaji wake haufanywi na kituo cha utangazaji. Ukishafanya hivyo, hata ukiwawekea asilimia 80 hawana ujanja wa kukwepa kwa sababu cost of production siyo yao ni ya mzalishaji wa ile kazi ya sanaa. Kazi hiyo inaendelea, tunakamilisha na kwa kuwa iko mikononi mwangu, tutamalizana nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie wasanii wa nchi hii, haki zenu ziko salama mikononi hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko tatizo limezungumzwa pia la kulinda haki zao. Bahati mbaya tunayo sheria ambayo kwa kweli imeweka adhabu ndogo sana, kwa hiyo, ukimkamata mtu ameivunja, ana uwezo wa kulipa na akaendelea na usaliti wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili tutalileta, tutabadilisha, tuwe na sheria ambayo ukimkamata mtu anaiba kazi ya msanii, adhabu yake iwe kubwa kiasi kwamba kila mmoja a-feel kwamba ni adhabu kubwa na hivyo akwepe kwenda kufanya kosa hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ushiriki wa wasanii, namshukuru sana Mheshimiwa January amelizungumzia.
Niende kwenye michezo, muda wangu unakimbia sana. La kwanza, Kamati ya Kudumu ya Bunge wameeleza masikitiko yao juu ya makusanyo kidogo kwenye sekta ya michezo, na sisi tunakiri kwamba kwa kweli makusanyo yako chini sana. Moja ya tatizo kubwa ilikuwa ni mifumo ya ukusanyaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuliarifu Bunge lako kwamba sasa Wizara imekamilisha utaratibu wa uwekaji wa mfumo kwenye uwanja wetu wa Taifa wa kulipa kielektroniki tiketi za kuingilia kwenye uwanja ule. Jambo hili likifanyika, litaongeza sana mapato na hivyo tutaondokana na hili tatizo la mapato kidogo kwenye sekta ya michezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tunapitia upya Sheria ya Baraza la Michezo lakini pia tunapitia upya Sera ya Michezo katika nchi yetu. Wako watu wamezungumza maoni yao juu ya hili, Waheshimiwa Wabunge, nataka niwahakikishieni, mwaka huu wa fedha tutakamilisha hili. Kwenye Sheria ya Baraza la Michezo, moja ya jambo ambalo tutalizingatia ni kuhakikisha tunaangalia kwenye sheria na sera vyanzo vingine ambavyo vitaisaidia Baraza hili kupata pesa za kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie kwa haraka haraka, suala la mshahara wa kocha. Ni kweli Serikali ya Awamu ya Nne ilikuwa ikilipa mshahara wa kocha wa mpira wa miguu. Hili nililitangaza hadharani kwamba uamuzi wa Serikali ya Awamu ya Tano ni kutolipa mshahara huo, kwa nini? Kwa sababu michezo iko mingi katika nchi yetu na sisi hatukuona busara ya kumlipa Kocha mmoja na ukaacha michezo mingine.
Kwa hiyo, uamuzi huu ulishapita, ni kazi ya vyama vya michezo, Serikali tutawawezesha kuwatengenezea mazingira mazuri vyama vya michezo vipate uwezo wa kulipa makocha wake badala ya Serikali kubagua na kulipa makocha wachache na michezo mingine ikaachwa nje ya wigo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ilikuwepo hoja hapa ya unaoitwa mgogoro kati ya TFF na TRA hasa lile sakata la kufungiana akaunti. Hili nalo tulilieleza lakini labda nilieleze tena.
Mheshimiwa Mwenyekiit, ni kweli kwamba kimsingi ukisikiliza kesi hii, tatizo siyo la TFF, tatizo ni la Serikali. Kwa nini? Mshahara huu ulikuwa unalipwa na Hazina, bahati mbaya wote wawili (Hazina na TFF) walitegeana kwamba ile kodi inayotokana na mshahara inalipwa na mwenzake. TRA mteja wao wanaomjua ni TFF ndiyo maana wanakwenda kumkamata TFF na kukamata mali zake. Hivyo hivyo kwenye mechi ile ya Brazil na Taifa Stars, Ndugu yangu Mheshimiwa Nkamia amelieleza vizuri kwamba kwa kweli TFF hawakushiriki, lakini kwa kuwa mteja wa TRA ni TFF, TRA wanambana TFF. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliambie Bunge lako, tumekaa pamoja Serikali, TFF na TRA tukakubaliana kimsingi anayetakiwa kuilipa kodi hii ailipe na ndiyo maana hali imetulia. Na sisi kama Serikali tutajitahidi kufuatilia na kusukuma jambo hili liishe. Bahati mbaya limekuwa ni jambo ambalo limekuwa linaisha, linarudi, linaisha na kurudi. Safari hii tunaamini tutalisimamia na kuhakikisha kwamba jambo hili linakwisha.
Mheshimia Mwenyekiti, nadhani kwenye michezo, pia niwapongeze watani zangu Yanga, Mheshimiwa Zitto alisema timu yako imeshinda; mimi ni Waziri wa Michezo. Nilivaa jezi ya Yanga kuwatia moyo na Simba mkifanya vizuri nitakuja kuvaa jezi yenu msipate shida, mimi Taifa Stars. Ila nawatakia kila la kheri Yanga kwenye mchezo wao na kuhakikisha kwa kweli tunawaombea wafanye vizuri. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia hoja hii, naomba mashabiki wa timu zetu hasa Simba na Yanga, inapotokea timu moja inakwenda kucheza mchezo wa Kimataifa, kwa kweli ni nchi yetu inacheza na Taifa hilo lingine. Tutangulize uzalendo mbele. Tumeona timu hizi wakati mwingine zikizomeana, lakini aibu siyo ya timu, ni aibu nchi. Ushauri wetu kama Wizara, tunaomba inapofikia mechi za Kimataifa, basi tupunguze kidogo ushabiki, tuweke uzalendo wa nchi yetu na nadhani litakuwa ni jambo zuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kidogo juu ya Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC). Kuna hoja hapa kubwa, nadhani ni vizuri nikaigusa, hoja ya mkataba kati ya Startimes na TBC kupitia Star Media. Wengi waliochangia wanasema jambo hili halina tija, lakini siyo kweli kwamba hakuna tija kabisa. Ngoja niziseme baadhi ya faida zilizopatikana kwenye mkataba huu na kabla ya kuzisema, niseme kwamba tulipopata Bodi mpya ya TBC moja ya kazi tuliyowapa kama Wizara ni kuupitia upya mkataba huu na kuangalia maeneo ambayo yanalalamikiwa kwamba ni maeneo yanye matatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri nataka niliarifu Bunge lako, maeneo hayo yamepitiwa na Bodi imefanya kazi nzuri, taarifa yao wameikabidhi kwangu, na sisi kama Wizara tunaifanyia kazi kuona upungufu wowote ambao umebainisha tukae mezani tuone namna ya kushughulika nayo. Pamoja na upungufu mkataba huu umeiwezesha Tanzania imekuwa mojawapo ya nchi za kwanza Afrika ikiwemo Rwanda na Visiwa vya Shelisheli kuhama kutoka mfumo wa utangazaji wa analojia kwenda dijitali mwaka 2012, ni kupitia huu mkataba nchi yetu imepata sifa na heshima ya kuwa nchi ya kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ya pili, mwaka 2015 Startimes walishinda tuzo ya Kimataifa ya World Quality Commitment ijulikanayo kama Golden Quality Award ambayo ni heshima kwa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ya tatu, mwaka 2016 Startimes imeshinda tena tuzo ya European Society Quality Research, ambayo watakabidhiwa Juni mwaka huu wa 2016, jijini Brussels, Ubelgiji. Tunadhani hii bado ni faida kwetu. Startimes imeajiri zaidi ya Watanzania 400 katika nafasi mbalimbali. Startimes imesajili wateja takribani milioni 1.2 lakini Startimes walikarabati jengo la ghorofa tano ambapo kwa sasa wanailipa TBC pango lake, kwa sababu kuna watu wanasema kama vile TBC hawapati chochote kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo waliyojenga vituo vya kurushia matangazo wamekodi kutoka TBC kwa sababu wao hawakuwa na maeneo, maeneo mengi waliyojenga ni maeneo ya TBC, kwa hiyo, wanailipa TBC na ziko faida nyingine nyingi, lakini nataka nikiri kwamba yako maeneo yanayolalamikiwa, nasi kama Serikali tuliagiza Bodi, Bodi imepitia mkataba na kwa kweli wameleta ripoti nzuri na tunaifanyia kazi na baada ya muda tutachukua hatua za kuboresha baadhi ya maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya mwisho pengine kwa sababu muda umeisha, kuna hoja nzuri ilitolewa na Kambi ya Upinzani, hoja ya kuangalia namna ambavyo tutahifadhi historia yetu. Niseme, kwa awamu sasa tumekuwa na mradi wa kuweka kumbukumbu ya ukombozi Kusini mwa Bara la Afrika na Tanzania imepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa mradi huo. Katika bajeti tunaomba mpitishe hapa, kuna pesa tumeomba kwa ajili ya kuweka kwenye mradi huo. Mradi huu ni mkubwa, unahusisha nchi za Kusini mwa Bara la Afrika na kwa sababu Tanzania ilishiriki katika harakati za ukombozi wa hizo nchi, tukapewa heshima hiyo, tunasaidiwa na wenzetu wale lakini pia kuna mashirika ya Kimataifa ambayo nayo yanaingiza mkono wake kusaidia kuhakikisha mradi huu unatekelezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia mradi huu tumeanza mazungumzo ya kuona namna ambavyo tutaufanya huu mradi pia u- trickle-down kwenye nchi yetu ili tuwe na uwekaji mzuri wa kumbukumbu na hasa kumbukumbu za ukombozi na nyingine ambazo zitalisaidia Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie, kwa kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, niwahakikishie hoja zenu ambazo sikuzigusa zitaletwa kwenu kwa maandishi na kila Mbunge atazipata. Tutazifanyia kazi na ninaamini mtapitisha bajeti yangu. Safari ijayo tukija, tutaripoti namna tulivyofanya vizuri. Kwa vyovyote vile, safari ni hatua, turuhusuni tupige hatua katika safari hii njema tunayoianza na ninaamini mtaturuhusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa muda wako, ahsanteni sana, naomba kutoa hoja.