Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuniwezesha kusimama na kuzungumza mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuchukuwa nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa ushindi wa kishindo alioupata katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015. Vilevile namshukuru kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na imani yake kwangu, naahidi kutekeleza majukumu yangu kwa weledi na juhudi kubwa ili kumsaidia Mheshimiwa Waziri katika kutekeleza majukumu aliyopewa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nampongeza Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kuchaguliwa tena kuiongoza Zanzibar katika kipindi kingine cha miaka mitano. Natumia fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Makamu wa Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kuteuliwa na Rais kuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vilevile nawapongeza Mawaziri wote walioteuliwa kuongoza Wizara mbalimbali katika Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa napenda kumpongeza Spika, Mheshimiwa Job Ndugai; Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson Mwansasu, wewe mwenyewe pamoja na Wenyeviti wote kwa kuchaguliwa kuliongoza Bunge la Kumi na Moja la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumshukuru sana Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, kwa kunielekeza na kuniongoza katika kufanya maamuzi sahihi yanayohusu utekelezaji wa shughuli zinazohusu sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee kabisa, nawashukuru wanawake wa UWT Mkoa wa Mtwara kwa kunichagua kwa kipindi cha tatu kuwa Mbunge wao kupitia tiketi ya Viti Maalum. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sitakuwa nimetenda haki pasipo kuishukuru familia yangu, hasa mume wangu mpenzi, Bwana Laurent Werema Paul na watoto wangu kwa ushirikiano wao mkubwa wanaonipa na kunitia moyo katika kutekeleza majukumu yangu ya kazi za kila siku za Wizara ninazozifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, timu ya Yanga katika historia ya nchi yetu imeweka rekodi kwa mara nyingine baada ya rekodi ya mwisho iliyowekwa na timu ya Simba mwaka 2003. Napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza sana timu ya Yanga kwa kuwa Bingwa wa Soka Tanzania Bara, lakini pili kushiriki Kombe la Washindi Bara la Afrika; na ni matarajio yetu kwamba wataingia hatua ya makundi baada ya mechi yao na timu ya Angola na hasa kutokana na ushindi walioupata katika mechi ya kwanza katika Uwanja wa Taifa Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja ya Wizara yetu na baada ya kusema hayo, naomba sasa kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya kwanza ambayo inahusu kutokuwepo viwanja vya michezo katika ngazi za Mkoa, Halmashauri na shule. Hoja hii imetoka kwa Waheshimiwa wafuatao; Mheshimiwa Kasuku Bilago, Mheshimiwa Lucy Owenya, Mheshimiwa Stanslaus na Waheshimiwa Wabunge wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kila Halmashauri, nadhani tunatambua kabisa kwamba kuna Kamati za Mipango Miji na vilevile kuna Baraza la Madiwani na Wabunge sisi ni miongoni mwa Baraza la Madiwani. Sasa Wizara tunasisitiza kabisa kwamba Halmashauri kupitia Baraza la Madiwani na Kamati ya Mipango Miji watenge maeneo katika kila shule. Watakapokuwa wanatenga maeneo ya shule tunawaomba Halmashauri wakumbuke kuacha maeneo ya kutosha kwa ajili ya viwanja vya michezo ili hata watakapokuwa wakiongeza majengo, lazima yabaki maeneo kwa ajili ya michezo. Vilevile katika ramani za makazi, tunaomba Halmashauri wahakikishe kwamba wanaacha viwanja vya michezo katika makazi ili wananchi waweze kufanya mazoezi na kucheza michezo mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaomba Waheshimiwa Wabunge wasimamie zoezi hili na wahakikishe kwamba wanafanya ukaguzi katika maeneo ambayo yametengwa ili kuona kama viwanja vya michezo vipo. Kuhusu ubora, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) litakuwa likikagua ili kuangalia ubora wa viwanja hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya pili ambayo inahusiana na kutokuwepo watumishi wa sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo katika baadhi ya Halmashauri. Waliochangia wameonyesha kwamba pia hata zile Halmashauri ambazo zina watumishi hawa, bado kuna matatizo kwamba wanakosa vitendea kazi. Sasa sisi kama Wizara tumeshaongea na Wizara ya TAMISEMI ili ianzishwe Idara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika kila Halmashauri. Hii tunaamini kabisa itasaidia Idara hii kuwa na fungu lao la bajeti ili waweze kuwa wanapata vitendea kazi na kuwawezesha kufanya shughuli zao kwa ufanisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo kubwa ni kuendeleza sekta hizi za habari, utamaduni na michezo kuanzia ngazi za chini na tunataka Wizara iwafikie wananchi vijijini kupitia Idara hii. Lengo lingine ni kwamba tunataka Wizara iwe na mfumo mzuri wa upatikanaji wa taarifa kupitia Idara hii ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ili tuweze kupanga vizuri shughuli za maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingine ya tatu ambayo imetolewa na Mheshimiwa Martha Mlata na Wabunge wengine, ni kutaka wasanii wapatiwe ardhi lakini vilevile kuwepo kituo kwa ajili ya sanaa za aina mbalimbali. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba Wizara tumeshaongea na Wizara ya Ardhi kwa ajili ya suala hili na upatikanaji wa ardhi utakuwepo kwa sababu Wizara ya Ardhi imeshaanza kulishughulikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Kituo cha Sanaa na Utamaduni, Wizara tayari tumeshapata eneo la ekari 25 katika eneo la Kiromo, kule Bagamoyo na taratibu za ujenzi zitafuata, lakini vilevile kwa wale watu binafsi ambao wanapenda kuingia, sekta binafsi ambazo zitapenda kuingia ubia ili kuweza kuharakisha ujenzi tunawakaribisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya nne ambayo imegusiwa pia na wachangiaji wengi, ni kutokuwepo usikivu wa redio ya TBC katika baadhi ya Wilaya za nchi yetu.
Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba Wizara tayari imeshatenga fedha za maendeleo katika bajeti ya mwaka huu 2016/2017 kwa ajili ya Mkoa wa Kigoma ambayo itaongeza usikivu katika Wilaya za Kasulu na Kakonko, Mkoa wa Mara Wilaya ya Tarime, usikivu katika Mkoa wa Ruvuma Wilaya ya Nyasa, Mkoa wa Tanga Wilaya ya Mkinga, Mkoa wa Arusha Wilaya za Longido na Ngorongoro, Mkoa wa Kilimanajro Wilaya ya Rombo na Mkoa wa kipindi hiki cha mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wakubali kupitisha bajeti yetu ili tuweze kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.