Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii, lakini pia nichukue nafasi hii kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini kwa kunichagua kuwa Mbunge wa Jimbo lao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii pia, pamoja na Mpango huu tunaojadili wa Bajeti, nami nitoe mchango wangu kwa sehemu ambayo naiona katika Mpango huu. Kwanza napenda kuishauri Serikali katika ukusanyaji wa kodi. Ifike mahali sasa tukusanye kodi kwenye viwanda, tukusanye kodi kwenye makampuni makubwa, bandarini na tuwe na lengo kubwa la kukusanya kodi kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, hatua hii ya Mpango huu wa Bajeti wa mwaka huu unakabiliwa na changamoto kubwa huko mbele. Kwa hivyo, tusipokusanya kwa kiwango kikubwa mapato ya Serikali, Mpango huu unaweza kuwa mzuri sana kama ulivyowasilishwa kwetu sisi, lakini hatimaye usiwe na matumaini na mafanikio mbele ya safari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango huu ninaoutoa katika kukusanya mapato ulenge zaidi yale makundi makubwa ya walipakodi kuliko wale wananchi wa ngazi za chini na wafanyabiashara wa ngazi za chini. Ifike mahali sasa tujijengee dhana ya udhibiti wa mapato ya Serikali na jinsi ambavyo wananchi wana hamu kubwa ya kupata huduma bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kutokana na muda, ni eneo la elimu bure. Nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya Mheshimiwa Rais kwa kutoa elimu bure. Naomba nishauri mambo machache.
Katika eneo hili sasa Serikali ije na mpango wake wa kuajiri nafasi zile za wazi katika Serikali ikiwemo zile za wale vijana wanaofanya vibarua katika shule hizi za sekondari ili gharama ipungue kwa mwananchi, lakini pia namna ya kupunguza zile gharama zilizobaki. Hadi sasa bado kuna michango mikubwa katika eneo hili la elimu ya sekondari na elimu ya msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iweze kuona ni namna gani inajaza nafasi za wahudumu, wapishi, walinzi na pia nafasi za kupunguza gharama zile zinazotokana na mwananchi ili wanafunzi wengi wapate elimu hii na kwa nafasi yao wapate kunufaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo linalohitaji kuboreshwa zaidi. Katika mchango wangu naomba kuishauri Serikali.
Kwanza ichukue nafasi kubwa ya kuweza kuanzisha Vyuo vya VETA, lakini pia Vyuo vya Ufundi Stadi vilivyopo katika Wilaya na kwenye Majimbo yetu, vibadilishwe kuwa Vyuo vya VETA haraka ili vijana wetu wengi wapate hatua ya kuwa na nafasi ambayo vijana wanapata ujuzi na ufundi stadi na kuweza kuajiriwa na hatimaye kumudu changamoto zitakazotukabili katika uanzishaji wa viwanda.
Eneo la viwanda, naomba basi niishauri Serikali, eneo hili la viwanda, tuweze kufanya utafiti kama Serikali, tuone kiwanda gani katika kanda ipi, rasilimali gani inahitajika na ipo katika eneo hilo ili kupunguza gharama na viwanda hivyo viweze kuwa na tija na kwa hivyo tunapofanya hivyo tunapunguza gharama kubwa ya uendeshaji wa Serikali katika kuanzisha viwanda na kuleta tija zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, nitoe angalizo pia katika eneo hili, ni eneo ambalo linatupa kazi kubwa kwenye madeni ya Serikali. Jimboni
kwangu, nichuke nafsi hii kukuomba sana. Serikali ina madeni makubwa sana, isifumbie macho. Madeni ya maji, madeni ya maabara, madeni mengine mengi ya barabara, lakini wakati huu Mpango umewasilishwa kwetu ni mpango mzuri, tutashindwa kutekeleza kule mbele ya safari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali, wakati wa sasa hadi kufikia bajeti, ikusanye orodha kubwa na takwimu kubwa ya madeni ya Serikali ya miradi iliyoanzishwa. Kama Jimbo ninalotoka, madeni ni zaidi ya shilingi bilioni tatu kwa Mradi wa Maji wa Benki ya Dunia. Fedha zinazodaiwa na wakandarasi kwa ajili ya malipo yao, wale waliokamilisha kazi na wale ambao wamefikia hatua mbalimbali, ni zaidi ya shilingi milioni 700, lakini hata kama tumekuja na Mpango mzuri mbele ya safari tutakuja kuhitilafiana na hatutakuwa na tija katika hii mipango mizuri kama hatutaweza kuona ni kwa namna gani madeni ya maji, barabara, maabara zilizoanzishwa na wananchi kwa kiasi kikubwa sana na sasa hata umeme vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo ninalotoka mimi, umeme umekwenda kwa vijiji takriban tisa au kumi, huku Waziri anatupa matumaini makubwa sana. Naomba kama itawezekana maeneo haya ambayo tayari Serikali imekuwa na madeni makubwa, yawekwe kwenye Mpango huu wa sasa ili yaweze kutatuliwa na wananchi waweze kunufaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naona ni jambo jema kama tutakuwa tunakamilisha miradi na inatoa huduma. Miradi ya aina hii iko mingi, kwa mfano, tulikuwa na ahadi ya Mheshimiwa Rais katika barabara ya Magara inayounganisha Mji wa Mbulu na Mji wa Arusha na Mji wa Babati kwa maana ya Makao Makuu ya Mkoa, Babati na Makao Makuu ya Mkoa wa Arusha. Kilometa 13 za ahadi ya Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete imewekwa kilometa moja na nusu hadi leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Daraja la Magara katika barabara hiyo, ambayo imepoteza maisha ya Watanzania wa Wilaya ya Mbulu na Wilaya ya Babati Vijijini, haikuwekwa hadi leo, kutoka ahadi ya Mheshimiwa Jakaya Kikwete, ahadi ya Mheshimiwa Mkapa na leo ahadi ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli na ni kilometa hiyo yenye mazingira magumu na hatarishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapanga mipango, ikifahamu kwamba ahadi za Mheshimiwa Rais ni moja ya utatuzi wa kero za wananchi. Pale ambapo Rais anafanya ziara, anapokutana na changamoto ya kero zao anawaahidi. Kufanyike utaratibu wa kuratibu ahadi za Mheshimiwa Rais. Iwekwe kwenye Mipango ya Serikali, ili Serikali kila wakati na kila mwaka katika bajeti yake, iweze kutatua. Barabara hii ya Magara, ambayo ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi, nashangaa kama tena leo, tunatafuta fedha za usanifu kwa ajili ya Mlima Magara na Daraja la Magara, wakati Serikali imetumia pesa nyingi kufanya usanifu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii, ahadi nyingi za Rais ziwekwe katika bajeti hizi na Mlima Magara usipowekwa kwenye bajeti ya mwaka huu, natoa angalizo kwamba sitakuwa tayari kupitisha Mpango wa Bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii pia kuzungumzia eneo la kero ya akinamama, wauza matunda, mbogamboga, ndizi, waendesha bodaboda, kodi hizi ziondolewe, ni kero. Haya ni makundi madogo, hayana uwezo wowote na hali hii inawasababishia mazingira magumu ya kufanya kazi zao. Naomba nitoe mchango huu kwa kuishauri Serikali itazame kwa jicho la huruma makundi haya ambayo tayari ni makundi ya jamii. Yanafanya shughuli hizi, wana mapato madogo, hawa watazamwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitoe angalizo kwa jinsi tunavyopoteza muda wetu katika ukumbi huu. Mara nyingi tumekuwa wa kuzomeana, mara nyingi tumekuwa wa mipasho, mara nyingi kiti chako kimeshindwa kulinda kikao na kwa mara nyingi tunashindwa kupata nafasi ya kutoa michango yetu. Tunaminywa katika dakika hizi mnazotupa kwa sababu ya mipasho, mizozo na migongano ya kisiasa yasiyo na tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu, miaka mitano ni kama mshale wa saa na Rais alisema tupunguze mipasho, mizozo na vijembe. Sasa Bunge hili, takriban muda wote tuliotumia ndani ya ukumbi huu, tumetumia muda mwingi vibaya na kwa hivyo hasara hii ni kubwa kwa Bunge, ni kubwa kwa Serikali, tunagharamikiwa kwa kodi za Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uongozi wa Bunge, kutoka kwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti, watusimamie ipasavyo kwa kulingana na kanuni zetu humu ndani. Ili haki itendeke kwa kila mmoja wetu kukosolewa, kurekebishwa na kuadhibiwa ikibidi. Kwa sababu tusipofanya hivyo, tutafanya makosa makubwa na mbele ya safari tutaleta uvunjifu wa amani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo imefika mahali, unafika mlangoni unaambiwa uvue mkanda. Hii ilikuwa jeshini, ilikuwa magerezani, sio huku. Huku ni eneo la heshima, tunatakiwa tujiheshimu na wale wenzetu wanaotuhudumia watuheshimu na hata kiti chako kiti kwa jinsi ambavyo tunafanyiwa, sio vizuri na sio itifaki ya Bunge. Naomba nafasi hii itumike vizuri, tusikejeliane na yeyote yule ambaye hataki kuheshimu kwa kweli tunakoseana.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Issaay muda wako umekwisha.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nafasi hii ni ndogo sana na ni ya hasara kwetu sisi na tunaminywa. (Makofi)
MWENYEKITI: Muda wako umekwisha Mheshimwa Issaay.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)