Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, kwa sababu maandiko yanasema yapaswa kushukuru kwa kila jambo.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu. Kwa namna ya kipekee nimshukuru sana Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuniamini kuwa kwenye dhamana ya Wizara hii ya Maji kuwapatia wananchi maji, kwa imani yangu ukiwapatia wananchi maji basi unapata baraka. Na nipo tayari kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge kuendelea kupata baraka hizi za kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee nikushukuru wewe binafsi kwa mijadala tangu mwanzo mwisho mmeusimamia mpaka leo tunafika katika suala zima la kuhitimisha; nimshukuru pia Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wote wa Bunge kwa namna walivyozisimamia shughuli zao katika Bunge mpaka leo hii tunakwenda katika hitimisho.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nimshukuru sana Mwenyekiti wetu wa Kamati, Makamu pamoja na Wajumbe wote wa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli Wizara yetu ya maji yawezekana kipindi hicho nyuma sikuwahi kuwa Mbunge lakini kuona Wizara inapongezwa, sijawahi kuona. Wizara ya Maji ilikuwa ni Wizara ya lawama, lakini leo hii Waheshimiwa Wabunge mnatupongeza; mmetutia moyo sana. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naninachotaka kukisema tu mbele ya Waheshimiwa Wabunge ni kwamba kama ni betri basi iko fully charged. Sisi viongozi wa Wizara ya Maji; mimi pamoja na Naibu wangu, Maryprisca Mahundi; Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Engineer Anthony Sanga; Naibu Katibu Mkuu, Nadhifa Kemikimba, na watumishi wote kwa maana ya wataalam wa Wizara ya Maji, tutafia kwenye matenki katika kukahikikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru kwa dhati kabisa Mwenyekiti pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, kwa maoni na ushauri waliolenga kubadili mitazamo na fikra na kuboresha namna tutakavyofanya kazi Sekta ya Maji.

Mheshimiwa Spika, maeneo yaliyotolewa ushauri ni pamoja na upatikanaji wa fedha, uvunaji wa maji ya mvua, upatikanaji wa misamaha ya kodi, ujenzi wa miundombinu ya majitaka, matumizi ya maji kutoka katika vyanzo toshelevu kwa maana ya ziwa na mito, umuhimu wa matumizi ya dira za maji za malipo kabla ya matumizi, masuala ya takwimu pamoja na maji kwa ajili ya wananchi na mifugo yao katika maeneo yanayopitiwa na mabomba makuu. Nataka niseme tu yote tumeyachukua na tutayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa Wabunge zaidi ya 65, wamechangia kwa kuongea na kwa maandishi. Kwa dhati kabisa nitumie fursa hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao ambayo kwa kiasi kikubwa inalenga kuongeza tija katika utekelezaji wa majukumu yetu ndani ya Wizara ya Maji na taasisi zake na sekta kwa ujumla. Itoshe tu kusema Waheshimiwa Wabunge kwa kuwa wachangiaji ni wengi sana nitaomba nijibu hoja kwa ujumla wake. Lakini kwa kweli nawashukuru sana na Mwenyezi Mungu awabariki sana Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza kwa ujumla, michango ilivyotolewa na Waheshimiwa Wabunge ni mingi na yote inalenga kuleta tija kwenye sekta yetu ya maji. Hata hivyo, michango kadhaa imerudiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi na mingine imechangiwa kwa hisia kali. Kwa kuwa muda uliopo hautoshi kujibu hoja zote, moja baada ya nyingine, naomba nitumie fursa hii kujibu hoja chache kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hoja moja wapo ambayo imezungumza ni juu ya upotevu wa maji; ni aibu na hatuwezi kukubali kuona Serikali inawekeza fedha nyingi wananchi wapate huduma ya maji halafu zije taarifa kwamba kumekuwa na upotevu mkubwa sana wa maji.

Mheshimiwa Spika, na mimi kama Waziri wa Maji nilishawahi kufanya ziara katika baadhi ya mamlaka zetu za maji. Niliwahi kupata taarifa kwamba hapa kuna upotevu wa maji wa asilimia 40, nilihoji kama kuna upotevu wa maji wa asilimai 40 kwa akili yangu tu ya kawaida kwamba ninategemea kuona mabwawa ya Samaki mtaani.

Mheshimiwa Spika, kwa akili yangu ya kawaida nilitegemea nione chemichemi za mito. Asilimia 40 ya upotevu wa maji si jambo dogo Waheshimiwa Wabunge. Kwa bahati nikamwambia hebu nipitishe baadhi ya mitaa sasa nione maji yanayopotea; tumepita baadhi ya mitaa sikuona hiyo asilimia 40 ya maji inayopotea.

Mheshimiwa Spika, ukweli wa dhati kabisa ni kwamba maji tunayosema yanapotea asilimia kubwa au kwa kiwango kikubwa yanaibiwa. Baadhi ya viwanda wanaweza wakajiunganishia kinyemela pasipo kulipa halafu mamlaka ya maji inadai kwamba au inatoa taarifa kwamba maji yale yamepotea, lakini yule ni mteja ambaye ametumia maji lakini hahesabiki katika taarifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hayo ni maelekezo ambayo tumetoa kwa baadhi ya mamlaka zetu za maji kuwajua wateja wao wakubwa na wadogo katika kuhakikisha wanadhibiti ili maji na malipo yaweze kupatikana na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Na vipo baadhi ya viwanda tulishawahi kukamata na tumeweza kuchukua hatua, lakini Waheshimiwa Wabunge hili jambo lazima tukubali kushirikiana. Serikali inawekeza fedha nyingi kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa namna nyingine sisi kama Wizara tumejipanga kutoa fedha na kukarabati maeneo ambayo yamekuwa na miundo mbinu chakavu ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, mathalani, eneo la Mtwara pale mjini. Mahitaji ya Mji wa Mtwara ni lita milioni 15, uzalishaji wa vyanzo vyetu ni lita milioni 13, lakini changamoto ya pale Mtwara ni miundombinu chakavu tangu ukoloni. Kupitia bajeti hii tunatoa fedha kwa eneo la Mtwara kuhakikisha wanakwenda kutengeneza miundombinu ile na wananchi waendelee kupata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kikubwa ni kwamba hili tumeliona na tutahakikisha kwamba kila mtumiaji anakua na dira bora ili kudhibiti upotevu huu wa maji na tuweze kuuweka katika asilimia ambayo inakubalika, asilimia 20. Sasa hivi kinchi tupo asilimia 36, lakini maelekezo ya Wizara ambayo tumewapa mamlaka zetu, na ndiyo kipimo, katika kuhakikisha kwamba lazima wasimame hapa na kwa kushirikiana na EWURA tunaendelea kudhibiti mamlaka zetu kuhakikisha kwamba tunakuwa katika hiki kiwango cha asilimia 20.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili lililozungumzwa ni tatizo la bei za maji mijini na vijijini; ni haki ya mwananchi kupatiwa huduma ya maji lakini mwananchi naye asisahau ana wajibu wa kulipia bili za maji. Ili gari liende lazima liwe na mafuta.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mwananchi kupatiwa huduma hii ya maji lazima atambue maji kutoka mtoni hayana miguu useme yatafika nyumbani lazima tuweke pampu na umeme ili kuhakikisha kwamba maji yale yanafika. Kwa maana hiyo, pale kutakuwa na gharama zinazohitajika.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na wajibu wa mwananchi kulipia bili za maji, sisi kama Wizara ya Maji tunasema bili hizo zisiwe bambikizi. Haiwezekani mwananchi ametumia maji ya 15,000 unamwambia alipe 120,000; haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja, tumetoa maelekezo kwa wasomaji mita wetu kwamba lazima wawe waamini na waadilifu juu ya usomaji. Lakini tumekwenda mbali sisi kama Wizara ya Maji kwa maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge, sisi lazima tutumie teknolojia ya sasa kuhakikisha tunafanya mageuzi katika Wizara yetu ya maji.

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha Unified Billing System. Kabla mteja hajasomewa mita zake au hajachajiwa bili anayotakiwa kulipa, anapokea message kwamba bwana fulani umetumia maji unit 30 unadaiwa kiasi fulani, thibitisha, anathibitisha mwisho wa siku tunaweza kum-charge bili ili aweze kulipa.

Mheshimiwa Spika, lazima tukubali kwamba sisi Wizara ya Maji si kisiwa, lazima tukubali kubadilika. Na kizuri huigwa. Tunaona wenzetu wa TANESCO wana mita za LUKU. Ni muda muafaka, na tumeshatoa maelekezo kwa Wizara. Na nimshukuru sana Katibu Mkuu wetu wa Wizara ya Maji, kaka yangu, Engineer Anthony Sanga, mimi nasema anatosha mpaka chenji inabaki, tumpigie makofi mengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi wadau mbalimbali wameshakuja, tunajifunza hizi mita kabla hatujaenda kumfungia mwananchi, zile changamoto ambazo tunaziona basi tuweze kuzitatua. Lakini eneo ambalo tunaweza kuondokana na changamoto ya bili za maji lazima tukubali mwarobaini wake ni prepaid meter, lazima twende katika katika uelekezo huo.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo naomba tusaidiane katika hili ili kuhakikisha kwamba tunafanya mageuzi katika Wizara yetu ya Maji.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo kama Waziri wa Maji nimejifunza, inakuwaje mwananchi Jijini Dar es Salaam unit ya maji analipa 1,600, lakini ukienda kijijini mwananchi anatumia maji ndoo ananunua kwa shilingi 50. Unaposema unit moja maana yake nini; unit moja maana yake ni lita 1,000. Lita 1,000 maana yake nini; lita 1,000 maana yake ndoo za lita 20, ziwe 50.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa mwananchi wa kijijini akinunua ndoo shilingi 50 maana yake ndoo 50 analipa shilingi 2,500 ilihali pale DAWASA Dar es Salaam mwananchi ananunua unit moja kwa shilingi 1,600 tena anapata nyumbani; hilo haliwezekani. Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, ametupa maelekezo Wizara ya Maji; wananchi watumie maji kwa bei rahisi na nafuu na wanufaike na matunda ya Serikali yao ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi Wizara ya Maji kupitia RUWASA tumetoa maelekezo mahususi kupitia bei zote za maji vijijini. Baada ya Bunge hili tutatoa bei elekezi kwa vijijini ili kuhakikisha wananufaika kwa kazi kubwa na maoni mazuri yanayotolewa na Waheshimiwa Wabunge wao hapa katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndugu zangu, nataka nizungumze jambo moja; lazima tukubali Rais wetu tangu ameingia ni mwaka mmoja tu. Hatuwezi kusema kwamba tumemaliza matatizo ya maji kabisa. Lakini tunachotaka kusema ni kwamba jitihada za muda mfupi ambazo amezifanya Rais wetu Mama Samia Suluhu si za kubeza hata kidogo, anatakiwa kuungwa mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi katika Wizara yetu ya Maji, haijawahi kutokea bajeti kutekelezwa kwa asilimia hata 80, leo tunaitekeleza bajeti asilimia 95; haijawahi kutokea. Yapo maandiko ya dini yanasema Waama “Bi-Neemat Rabbika Fahadithi”, zielezeeni neema za Mwenyezi Mungu kwa kushukuru; tumshukuru sana Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, actions speak louder than words, matendo yanaongea kuliko maneno. Leo tunaona Mheshimiwa Rais kwa mwaka mmoja kwa namna ya fedha hizo zilizotoka, achana na hilo tu la fedha, yeye kama Mama maelekezo ambayo ametupa sisi Wizara ya Maji, mimi ndio Waziri pekee ambaye niliwahi kusimamishwa katika Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, nakumbuka alisema Waziri wa Maji uko wapi nikasimama. Akasema yeye ni Mama na anatambua asilimia kubwa ya wanaoteseka ni akina mama Vijijini. Akina mama wanatembea umbali mrefu kwa kukosa maji kwa maana ya kutafuta maji, wengine wamepoteza ndoa zao. Hataki kusikia, hataki kuona akina mama wakiteseka juu ya tatizo la maji.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, nataka niwaambie baada ya maneno yale mimi sikuwahi kulala, lakini nilikaa na nikajitafakari na Waheshimiwa viongozi wenzangu kwa maana watendaji wote.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge, hakuna sikio lolote duniani lisilosikia vinywa vingi vikisema pamoja; tumewasikia.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Maji ilikuwa na changamoto nyingi sana lakini mpaka hapa tulipofika, tulipotoka ni mbali. Moja ya changamoto kubwa sana ambazo zilikuwa zinaiathiri Wizara yetu ya Maji ni miradi iliyojengwa chini ya kiwango ya vijiji 10. Ni miradi ambayo imejengwa matenki lakini haitoi maji.

Mheshimiwa Spika, kazi ya kwanza ambayo tumejipa – na tuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kuona haja ya kuanzishwa Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA), hayo ni maoni yenu Waheshimiwa Wabunge. RUWASA ina miaka miwili hadi mitatu sasa tunakwenda, kama ndama, amezaliwa na kwenda. Ameikuta miradi 177. Kwa muda huu mfupi nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge miradi 127 tumekwishaikwamua katika kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa tunaona nuru na mwendo wa Wizara yetu ya Maji, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha; Mheshimiwa Rais anatu- support. Tumezungumza hapa, Wizara ya Maji, kwa maana kama nchi, hatuna uhaba ama umasikini wa vyanzo vya maji, tuna maji juu ya ardhi zaidi ya mita za ujazo bilioni 105, maji chini ya ardhi ni mita za ujazo bilioni 21 kwa maana ya total ya bilioni 126; hatuna sababu ya kulalamika juu ya matatizo ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya changamoto zilizokuwa zinatuathiri sisi Wizara ya Maji ni vitendea kazi. Leo kwa Mheshimiwa Kuchauka, pale miaka yote watu wamefanya tafiti pamoja na tunatambua rasilimali za maji tulizokuwa nazo, ni mita za ujazo bilioni 21 lakini hatupati maji na tulishaaminishwa kwamba hapa maji hakuna. Lakini nashukuru sana wataalam wetu kwa mind set ambazo tunazigeuza, leo wamekwenda Liwale tumepata maji ya kutosha, na Mheshimiwa Mbunge ni shahidi, tunakwenda kupeleka fedha sasa kutatua tatizo la maji Liwale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nini maana yake; wakati mwingine tunashindwa kujua maji chini ya ardhi yapo au hayapo kwa sababu ya ukosefu wa vifaa vya kisasa. Uking’ang’ania vifaa vilivyopitwa na wakati utakuwa umepitwa na wakati. Samia Suluhu Hassan ndio suluhu ya matatizo ya maji hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ametupatia fedha, tunakwenda kununua mitambo 25 kwa ajili ya kuchimba visima. Na kila mkoa utakuwa na mtambo wake wa kuchimba; haijawahi kutokea, tumpigie makofi mengi sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, achana tu na mitambo, anatambua kwamba siyo maeneo yote ukichimba unaweza ukapata maji; siyo maeneo yote. Yapo maeneo ambayo tukichimba tunapoteza fedha za Serikali. Ametupatia fedha kwenda kununua seti tano kwa ajili ya kuchimba mabwawa, siyo tu kwa wananchi kupata maji, bali hadi mifugo yao nayo iweze kupata maji. Haya ni mageuzi makubwa sana kwa Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mitambo kwa ajili ya utafiti, zaidi ya minne, fedha ameshatupa. Ndani ya mwezi huu wa Sita tutapokea vifaa vile katika kuhakikisha watu wanakwenda kupata huduma ya majisafi na salama.

Mheshimiwa Spika, na ninataka niwaambie wakandarasi na wahandisi wetu wa maji – nilishazungumza kwenye bajeti – sisi viongozi wa Wizara ya Maji tutacheka kwa kuona maji bombani, lakini kwa mhandisi ama mkandarasi ambaye atatuchelewesha juu ya upatikanaji wa maji, ukicheka na nyani utavuna mabua, sisi hatupo tayari kucheka na mtu yeyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la miji 28. Tulikuwa na viporo ama miradi ambayo ilikuwepo tu kwenye makaratasi Waheshimiwa Wabunge. Suala la miji 28 lilikuwa likizungumzwa tu, halitekelezeki. Samia Suluhu Hassan ndiyo amekuja kuwa-unlock mradi huu wananchi wapate huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, amefanya mazungumzo na Viongozi Wakuu wa India, amemuita Balozi Ofisini kwake. Leo nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge, tumalize Bunge, Mheshimiwa Rais tumemuomba ashuhudie utiaji saini wa miradi hii kwenda kutekelezeka.

Mheshimiwa Spika, na narudia hapa; tusidanganyane, tunakwenda kutekeleza Mradi wa Maji HTM kwa maana Handeni, Korogwe, Muheza, Pangani; tunakwenda Kilwa Masoko, Nanyumbu, Ifakara, Chunya, Rujewa, Waking’ombe, Makambako, Njombe, Kiomboi, Singida, Manyoni, Chemba, Chamwino, Mugumu, Kasulu, Mpanda, Sikonge, Urambo, Kaliua, Kayanga, Geita, Chato, Mafinga, Makonde, Rorya, Tarime na Songea. Hizi ni jitihada kubwa zinazofanywa na Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, jana kaka yangu, Mheshimiwa Katani – hapa naona ameondoka – nataka nimueleze yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara ya Maji maelekezo ambayo Mheshimiwa Rais ametupa hajatueleza kwamba sehemu fulani peleka maji, sehemu nyingine usipeleke. Ametupa maelekezo kuhakikisha asilimia 85 ya upatikanaji wa maji vijijini na asilimia 95 ya upatikanaji wa maji mjini.

Mheshimiwa Spika, tumetenga kiasi cha shilingi bilioni 29 kwenda kutekeleza miradi ya maji 44 katika Mkoa wa Mtwara. Lakini katika Jimbo la Mheshimiwa Katani tunakwenda kutekeleza mradi ambao unajumuisha zaidi ya vijiji 15 ambao unaoitwa Mradi wa Nanyuwila – Maundo. Mradi ambao utakwenda kutatua matatizo ya maji kwa Vijiji 15 vya Nakayaka, Mnyawa, Mchichira, Mkwajuni, Shangani, Pachani, Mnarani, Namahonga, Maundo, Chiumo, Chang’ombe, Kunanundu, Lukokoda, Ghanajuu na Ghanachini; hizi ni jitahada za Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuna Mradi ambao tunauita wa Mkwiti ambao unakwenda kutatua shida ya maji katika vijiji 17, Kijiji kimoja sasa hivi cha Mangombya kimeshaanza kupata huduma ya maji. Mkandarasi yuko site anaendelea na ujenzi wa matenki matano ili kuhakikisha wananchi hawa wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumesikia maombi ya Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Mtwara juu ya ujenzi wa Mradi wa Makonde. Mimi binafsi Mheshimiwa Rais alinituma kwenda zangu Newala nimekwenda kujionea hali ya mradi ule.

Mheshimiwa Spika, mradi ule ni chakavu, mradi ule tangu Baba wa Taifa, mradi una umri mkuwa kuliko mimi Waziri wa Maji na hamna namna nyingine zaidi ya kujenga mradi mpya. Nataka nimpe taarifa baba yangu, Mheshimiwa Mkuchika, na Mheshimiwa Katani, waandae futi. Mheshimiwa Rais ametupa maelekezo na tumekwishapata mkandarasi, kilichobaki tunakwenda kusaini mradi wa zaidi ya bilioni moja kuhakikisha Wanamakonde, Tandahimba pamoja na Nanyamba wanakwenda kupata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ipo miji tunasema kwamba imeachwa. Lakini pia moja ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezijenga ni kuhakikisha kwamba Serikali inatumia rasilimali toshelevu kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwishaanza; ukienda Lindi pale Mjini tuna mradi wa bilioni 33 umekwishakamilika. Mradi ule wa bilioni 33 tumetoa bilioni tatu kwa ajili ya kupeleka maji Mitwero. Sasa hivi tumetoa bilioni 12 kwa ajili ya kupeleka maji Mchinga kwa mama yetu, Mheshimiwa Salma Kikwete. Hizo ni jitahada kubwa sana za Serikali.

Mheshimiwa Spika, leo hii ukaenda zako Musoma kwa dada yangu, Mheshimiwa Esther Matiko, Mkoa wa Mara, tuna mradi wa zaidi ya bilioni pale, tumeshaukamilisha. Lakini tumekuja na Mheshimiwa Rais katika Mradi wa Mugango – Kiabakari – Butiama, zaidi ya bilioni 70. Tumekwishautekeleza. Sasa hivi tumeshaukamilisha mradi pale Bunda Mjini zaidi ya bilioni 10; hivi Mheshimiwa Rais awape nini au awape donda mfukuze nzi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kikubwa sisi tunachotaka ni kumuunga mkono Rais wetu. Tumeona ameyatoa maji Ziwa Victoria tumeyaleta Tabora, tumeyapeleka Igunga, tumeyapeleka Nzega, zaidi ya bilioni 600, na vijiji 100 vinapata huduma ya maji safi na salama. Mradi ule sasa unakwenda Kaliua, unakwenda Sikonge hadi Urambo kwa Mheshimiwa Mama Sitta, katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, ukienda Arusha tuna mradi wa zaidi ya bilioni 520 hii; hii yote ni katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, ukienda zako pale Sumbawanga Mjini tuna mradi wa zaidi ya bilioni 35; hizi ni jitihada kubwa. Kwa hiyo kikubwa Waheshimiwa Wabunge tunakubaliana kwamba rasilimali toshelevu kwa maana ya maziwa na mito tuliyokuwa nayo, ikitumika itakwenda kutatua matatizo ya maji. Na mimi Waziri wa Maji naamini hilo kupitia Kamati yangu.

Mheshimiwa Spika, leo tunakwenda kutatua mradi mkubwa wa maji pale Mbeya kwa kutumia Mto Kiwira kwa maelekezo tu. Sisi Waheshimiwa Wabunge maelezo na maoni mliyotupa tumeyapata tutayafanyia kazi katika kuhakikisha watanzania wanapata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho; Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan lazima tumuunge mkono. Kama nilivyotangulia kusema awali, kuna mambo ambayo ni magumu kufanyika lakini Rais wetu ana uthubutu. Tumeona Dar es Salaam namna tulivyopitia kwenye changamoto ya crisis ya Mto Ruvu kukauka, leo tunakwenda kujenga Bwawa la Kidunda. Huu ni uthubutu wa hali kubwa sana, na tumpigie makofi sana Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Lakini tunaona eneo hili la Jiji la Dodoma tangu Serikali ihamie hapa kumekuwa na uhitaji mkubwa sana wa maji. Kwa muda mfupi Mheshimiwa Rais ameingia, kutokana na mahusiano yake mazuri, tumepata fedha kupitia African Development Bank, zaidi ya USD milioni 125 kwa ajili ya kwenda kuanza kujenga Bwawa lile la Farkwa; hizi ni jitihada kubwa sana. Bunge limeshauri kwa muda mrefu lakini utekelezaji wake ulikuwa wa kusuasua, leo tunakwenda kulitekeleza hili jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumza haya, ahsante sana na Waheshimiwa Wabunge Mwenyezi Mungu Awabariki sana. Naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naafiki.