Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri Mheshimiwa Juma Aweso na Naibu wake Engineer Maryprisca Mahundi pamoja na wataalamu wa Wizara ya Maji kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, Waziri na timu yake wamekuwa mfano wa kuigwa kwenye kutatua changamoto za maji na kuwatua akinamama ndoo kichwani, kwani maji ni haki ya msingi kwa binadamu wote. Kwa ujumla, inatia faraja kuona upatikanaji wa maji vijijini unaongezeka, kama alivyoonesha kwa kina katika hotuba yake ya bajeti ya mwaka huu wa 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, katika jimbo langu la Moshi Vijijini kuna changamoto ya upatikanaji wa maji ya bomba katika maeneo yafuatayo; Kata ya Kibosho Kirima yenye vijiji vya Kirima Juu, Kirima Kati na Boro ina wakazi 10709 na kaya 2,332. Kata hii inahudumiwa na RUWASA. Miradi ya Maji ya Boro na Kirima ina changamoto kubwa ya upungufu wa maji kwenye mifumo. Upungufu huu umeleta usumbufu mkubwa sana kwa wananchi na taasisi zikiwemo Chuo Kikuu cha Kilutheri cha Masoka, shule za sekondari zenye mabweni (Kirima na Masoka), shule za msingi na taasisi za dini zilizopo kwenye kata.

Mheshimiwa Spika, kwenye taasisi hasa zile zenye mabweni, wanafunzi wameishia kutumia maji yasiyo salama kutoka miferejini na mtoni na kusababisha magonjwa mbalimbali ya tumbo na ngozi. Tunaishukuru Serikali kwa kutenga fedha za kuboresha mradi huu.

Mheshimiwa Spika, maeneo ya kata za Kibosho Kati na Okaoni zenye jumla ya vijiji 14 zinahudumiwa na Mradi wa Maji Otaruni ambao ulijengwa miaka ya 1980. Eneo hili linahudumiwa na RUWASA. Kwa sasa watu wameongezeka sana na mifumo ya usambazaji maji imechakaa. Kwa hiyo, kuna uhitaji wa kuupanua na kuukarabati. Tunaishukuru Serikali kwa kutenga shilingi 200,000 katika mwaka huu wa fedha unaoishia ili kufanya ukarabati. Tunaomba Serikali iangalie miundombinu ya eneo hili kwa jicho la pekee na kuongeza bajeti ili mradi huu ukamilike.

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto ya upatikanaji maji ya uhakika katika baadhi ya vijiji kumi vya kata ya Kibosho Magharibi. Vijiji hivyo ni Manushi Sinde, Manushi Ndoo, Mkomongo, Kifuni, Umbwe Onana, Umbwe Sinde, Manushi Sinde, Manushi Mashariki, Manushi Kati na Umbwe Kati. Kata hii ina wakazi 20,291 na baadhi ya maeneo haya yanaunganishwa na chanzo cha maji toka Jimbo la Hai, kwenye mradi wa Makeresho - Lyamungo - Umbwe na inahudumiwa na RUWASA.

Mheshimiwa Spika, maji ya mradi huu huelekezwa zaidi kwenye Jimbo la Hai. Ili kutatua kero hii, kuna umuhimu wa Wizara kutenga fedha za kusaidia kununua mambomba na kuunganisha wananchi wa maeneo haya na chanzo kingine cha maji kilicho karibu katika eneo la Moshi DC na kuachana na kile cha Jimbo la Hai.

Mheshimiwa Spika, katika kata ya Mabogini kuna mradi unaoitwa mradi wa vijiji vitano; vijiji hivyo ni Muungano, Chekereni, Maendeleo, Mtakuja na Mserekia. Mradi huu umeanza na umekwishaombewa fedha na MUWSA na unangoja utekelezaji na kukamilisha.

Mheshimiwa Spika, kero nyingine kubwa iko katika kijiji cha Mabogini. Tunaomba miradi hii ipewe kipaumbele, kwani wakazi wa Kata ya Mabogini ni wengi (28,992) na kuna changamoto kubwa ya maji ya kunywa. Hili ni eneo la kimkakati ambalo wahamiaji wengi toka mlimani wameanzisha makazi huko na hawana vyanzo mbadala vya maji. Tunashukuru kwa kupatiwa shilingi milioni 500 ili kutekeleza mradi huu.

Mheshimiwa Spika, tunaiomba Serikali itutengee pesa za kutosha ili maji yafike mpaka Remiti Umasaini kwani maeneo haya yana uhaba mkubwa wa maji. Tunashukuru kwa kupatiwa shilingi milioni 500 ili kutekeleza mradi huu. Tunashukuru kwa kupatiwa shilingi milioni 500 ili kutekeleza mradi huu. Tunaiomba Serikali itutengee pesa za kutosha ili maji yafike mpaka Remiti Umasaini kwani maeneo haya yana uhaba mkubwa wa maji.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Old Moshi Mashariki, MUWSA ilikabidhiwa mradi wa maji ya kunywa wa Old Moshi Mashariki unaohudumia vijiji vinne vya Kikarara, Tsuduni, Mahoma na Kidia takribani miaka miwili iliyopita. Eneo hili lina wakazi wapatao 9,528. Tunaishukuru Serikali kwani wameanza kuweka mabomba ambayo hayajasambaa kata nzima. Tunaiomba Wizara iwawezeshe MUWSA wakamilishe huu mradi.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Uru Shimbwe yenye vijiji vya Shimbwe Juu na Shimbwe Chini, wananchi wana changamoto kubwa ya maji na wamejiongeza na kuanza kujenga miundombinu katika vyanzo vyao vya maji vilivyoko mlimani kwa kutumia nguvu za wananchi. Kuna Mradi wa Maji Kimangara (kilometa nne) na mradi wa maji Mofuni (kilometa nne).

Mheshimiwa Spika, baada ya ujenzi, wana Shimbwe wanakabiliwa na changamoto ya mabomba ya kusafirisha maji kwenye kila mradi kwenda vijiji husika.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kimochi ina zaidi ya wakazi 13,000. Kata hii ina vijiji vya Mowo, Sango, Shia, Miami, Lyakombila na Kisaseni. Eneo lote linahudumiwa na MUWSA. Tunaishukuru Serikali kwa jitihada za awali kuwafikishia wakazi wa eneo hili maji. Ila bado kuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji maji katika maeneo mengi hasa Kijiji cha Sango. Tunaiomba Serikali itutengee pesa za kutosha ili maji yafike maeneo yote ya kata hii vikiwepo vijiji vya maeneo ya tambarare.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Uru Kusini yenye vijiji saba (Okaseni, Kimanganuni, Rua, Kariwa, Longuo A, Kitandu na Shinga) ina takribani wakazi 22,904 na ina miradi mitatu ya Mang’ana, Kisimeni na Mbora. Changamoto ya miradi hii ni maji kidogo katika mifumo ambayo hayatoshelezi na mara kwa mara huwa ni machafu sana. Hata ripoti ya Mkaguzi Mkuu yam waka huu imeeleza kwamba maji hayo hayafai kwa matumizi ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Arusha Chini katika vijiji vya Mikocheni yenye wakazi 4,378 na Chemchem yenye wakazi 2,140 kuna uhaba wa maji. Sasa hivi ni watu wa Kirua Kahe wanatoa huduma ya maji ya kuuza katika maeneo haya. Maji huuzwa kwa bei ya juu na si salama kwa matumizi ya binadamu. Kata hii inahudumiwa na RUWASA.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa kujenga mradi wa Ochai Ngoma katika Kata ya Uru Mashariki unaohudumia vijiji vinne kati ya saba, tenki lililopo ni dogo na halitoshelezi. Kuna umuhimu wa kujenga tenki kubwa la kuhifadhi maji ili lihudumie vijiji vyote saba (Materuni, Mruia, Mwasi Kaskazini, Kishumundu, Mwasi Kusini, Mnini na Kyaseni) yenye wakazi 14,78. Kata hii inahudumiwa na MUWSA.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Uru Kaskazini, MUWSA haijatekeleza ahadi ya kuunganisha vijiji vya Msuni (wakazi 2,272) na Njari (wakazi 3,327). Chanzo cha maji haya kiko Uru Kaskazini na maji haya yamepita maeneo ya Uru Kaskazini na kwenda Kata ya Uru Kusini na Kata ya Pasua ya Jimbo la Moshi Mjini.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Old Moshi Magharibi kuna mradi wa maji wa Tela Mande ambao umekamilika. Mradi huu una maji mengi sana na ya ziada ambayo kwa sasa yanahudumia wananchi wa ukanda wa milimani. Vijiji na vitongoji vya kata hii vilivyopo ukanda wa tambarare kama kile cha Mandaka Mnono havina maji ya bomba.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuelezea changamoto zilizopo hapo juu, naishauri Wizara ya Maji itekeleze yafuatayo; kwanza naishauri Serikali itenge fedha za kutosha ili watafute na kujenga vyanzo vipya vya maji na kuyapeleka kwenye miundombinu ya miradi ya maji ya Boro na Kirima Kata ya Kibosho Kirima ili kutatua changamoto ya uhaba wa maji.

Mheshimiwa Spika, pili naishauri Serikali itenge fedha za kutosha kukarabati, kupanua na kujenga upya mradi uliopo katika Kata za Kibosho Kati na Okaoni kwa kutumia vyanzo vilivyojengewa tokea miaka ya 1980.

Mheshimiwa Spika, tatu naishauri Serikali kupitia Wizara ya Maji itenge rasilimali pesa ya kutosha ili kujenga miundombinu mipya kwa ajili wa wananchi wa Kata ya Kibosho Magharibi yenye vijiji 14 kwani maji kutoka mradi wa Lyamungo - Umbwe kutoka Jimbo la Hai hayafiki kwa uhakika katika Jimbo la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Spika, nne, naishauri Serikali ipeleke fedha za kutosha kukamilisha mradi ulioanza na kuhakikisha maji yanafika Umasaini, eneo lenye uhaba mkubwa wa maji.

Mheshimiwa Spika, tano naishauri Serikali itenge rasilimali fedha ya kutosha kukamilisha mradi wa maji uliopo Kata ya Old Moshi Mashariki.

Mheshimiwa Spika, sita naishauri Serikali kupitia Wizara ya Maji isaidie juhudi zilizoanzishwa na wananchi wa Kata ya Uru Shimbwe kwa kuwanunulia mabomba ya kusafirisha maji na kuyafikisha kweye vijiji vya Uru Shimbwe Juu na Chini.

Mheshimiwa Spika, saba naishauri Serikali kupitia Wizara ya Maji iwekeze vya kutosha na kuhakikisha wakazi wa Kata ya Kimochi wanapata maji ya kutosha kuanzia ukanda wa juu na tambarare.

Nane, naishauri Serikali kupitia Wizara ya Maji iwekeze na kutatua kero ya maji kidogo kwenye mifumo ya miradi na ile ya maji machafu iliyolalamikiwa katika kata ya uru kusini, kwani mkaguzi mkuu ameeleza hayafai kwa matumizi ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, tisa ninaishauri Serikali iangalie kwa jicho la pili na kuwapatia maji wananchi wa vijiji vya Mikocheni na Chemchem vilivyoko Kata ya Arusha Chini.

Mheshimiwa Spika, pia kumi ninaishauri Serikali ije na mkakati wa kujenga tenki kubwa la kuhifadhi maji na litumike kuhudumia Kata saba za Uru Mashariki.

Kumi na moja, nanaishauri Serikali iwaunganishe kwenye mfumo wa maji wananchi wa vijiji vya Msuni na Njari vilivyopo Kata ya Uru Kaskazini kwani vyanzo vya mradi huu viko kwenye kata yao. Kwa kufanya hivyo, wananchi watakuwa walinzi bora wa miundominu na vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, mwisho ninaishauri Serikali ipeleke maji ya mradi wa Tela Mande uliopo Old Moshi Magharibi katika maeneo ya tambarare huko Mandaka Mnono na vitongoji vyake.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.