Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye Bajeti ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anachapa kazi katika kuiendeleza nchi yetu ikiwemo katika Sekta hii ya Maji. lakini pili nawapongeza pia Mheshimiwa Waziri rafiki yangu Mheshimiwa Aweso pamoja na dada yangu Maryprisca kwa kazi kubwa wanayoifanya katika Wizara hii na kuhakikisha kwamba wanaisimamia vizuri miradi ambayo inatekelezwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi binafsi katika Jimbo langu nimenufaika sana. Tangu nimeingia madarakani miezi 18 iliyopita tayari miradi zaidi ya 11 imekuwa ikitekelezwa yenye thamani ya jumla ya Shilingi Bilioni 2.18. Kwa hiyo naipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya ndani ya jimbo langu na nchi nzima kwa ujumla. Kwa mfano kuna vijiji vya njia nne tayari kuna mradi umeshakamilika pale. Somanga kuna mradi umekamilika, Mtumbei Mpopera kuna mradi umekamilika, Kipatimu kuna mradi unaendelea kutekelezwa. Vilevile kuna ukarabati wa visima vifupi unaendelea kufanyika katika vijiji mbalimbali. Kipindimbi kuna mradi wenye thamani ya Shilingi Milioni 497 wa UVIKO-19. Lakini pia kuna Vijiji vya Malendego, Chumo, Chapita, Kinjumbi kuna miradi inaendelea kutekelezwa iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna uchimbaji wa visima unaendelea kufanyika katika Vijiji vya Mitole, Zinga Kibaoni Namayuni pamoja na Kisima Mkika. Pia nina furaha kubwa kusikia katika mpango wa bajeti wa mwaka ujao katika Kitongoji cha Nasaya, Kijiji cha Mtekimwaga pamoja na Kijiji cha Miteja, Kitongoji cha Masaninga Serikali imepanga kuchimba visima virefu ili kuweza kuwahudumia wananchi waweze kupata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na ufanisi huu uliopatikana bado kuna baadhi ya maeneo takribani vijiji visivyopungua 15 vina changamoto kubwa sana ya maji. Wamekuwa wakitumia majitope wakati wa masika, wakati wa kiangazi wanapata tabu sana kusafiri mbali kutumia visima vya asili kupata maji; navyo ni Vijiji vya Nandete, Nandembo, Namatewa, Ngarambi kwa Kinjeketile Ngwale huko, Nambondo, Bugo, Kinywanyu, Namakoro, Ngorongoro, Lyombanga, Somanga Simu, Handa, Mtende pamoja na Mwegei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ulizungumza hapa, kuna kauli zilitolewa na baadhi ya Wabunge jana na leo zinagongana kidogo. Lakini mimi niseme katika baadhi ya maeneo yetu ni kweli kuna hali fulani yakutoeleweka. Kwa sababu mgao wa fedha katika baadhi ya Majimbo au Wilaya umekuwa ni mdogo sana. Kwa mfano, tarehe 14 mwezi Machi mwaka 2022 mimi pamoja na Kamati yetu ya PAC tulitembelea katika mradi mmoja wa maji kule Manyara katika Kijiji cha Hydom kuna mradi pale wa bilioni 12 umewekezwa lakini unahudumia kata tatu tu.

Mheshimiwa Spika, lakini katika jimbo langu miradi yote iliyowekezwa pamoja na UVIKO-19 ina gharimu shilingi bilioni 2.18 tu, haifiki hata robo ya mradi mmoja tu ule ambao umewekezwa kule Manyara. Kwa hiyo kwa kweli jambo hili ni lazima Wizara ilifanyie kazi ili kuhakikisha hii keki inayopatikana iweze kugawanywa vizuri.

Mheshimiwa Spika, nimesema hapa kuna vijiji 15 bado vina shida ya maji. Kwa hiyo tukiigawa vizuri ile keki ni wazi kabisa kwamba mambo yatakwenda vizuri. Na mimi katika kuzingatia hilo ningependa kusema kwamba nimefuatilia kuhusu utekelezaji wa maji kutoka Mto Rufiji kwa karibu sana kupitia DAWASA na RUWASA Wilaya ya Kilwa. Kule DAWASA tayari wameshapata designer wa mradi wa maji kutoka Mto Rufiji. Tayari walitanga zabuni wameshapata, na tayari wako katika hatua mbalimbali za kuelekea kutekeleza ule mradi ambapo wataweka chujio pale katika Kijiji cha Mloka kule Rufiji.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa upande wa Kilwa wao walikuwa nyuma kidogo tarehe 19 mwezi huu wanatarajia kufungua zabuni ya kumpata designer, yule Mhandisi mshauri kwa ajili ya ku-design mradi wa maji kutoka Mto Rufiji.

Kwa hiyo ombi langu na ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba hii miradi miwili iunganishwe. Inawezekana kwenye ku-design mradi ikawa wametofautina, lakini kwenye utekelezaji wa mradi ningeomba basi iuanganishwe ili apatikane mkandarasi mmoja ambaye atajenga huu mradi wa maji kutokea kule Mloka Rufiji, bomba basi kama litapita Ikwiriri au litakwenda kule Kibiti, likifika pale linagawanyika lile lingine linakwenda Kusini kuanzia wilaya ya Mheshimiwa Mchengerwa pale Rufiji inaendelea mpaka wilaya yangu linakwenda mpaka kwa mama Kikwete kule Mchinga Liwale, Nachingwea, Newala na maeneo mengine yote ya kusini. Lakini pia na hawa wa Kaskazini kwa maana ya Mkoa wa Pwani, Bungu Mkuranga mpaka Dar es salaam nao waweze kupata maji mengi yanayotokana na maji ya Mto Rufiji.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna hii miradi ambayo inatekelezwa na Mfuko wa Maji, imekuwa na tatizo sana kwenye ulipaji. Pale mimi ninao ule mradi wa Kinjumbi pale ambao una gharimu shilingi milioni 326 za Serikali Mkandarasi hivi sasa ana miezi miwili ali-rise claim lakini mpaka leo haulipwi. Sababu ukifuatilia unaambiwa shida ni kwamba mlolongo mrefu kwenye hii miradi ambayo inatekelezwa na mfuko wa maji.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali ijaribu kuona namna ya kupunguza mlolongo ili tusije tukaangukia kwenye changamoto ya kulipa riba ikaigharimu zaidi Serikali.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nasema nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuzungumza jioni ya leo. Naunga mkono hoja kwa asilimia 100.