Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maji. Nitaanza kwanza kwa kuugusa Mkoa wa Songwe kwa sababu Mkoa wa Songwe tuna changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji safi na salama. Mkoa wetu una kata zaidi ya 90 lakini hakuna kata yenye uhakika wa kupata maji safi na salama. Changamoto hii imepelekea baadhi ya maeneo kujikuta wana-share maji pamoja na mifugo; hasa ukienda katika Wilaya za Ileje, Momba na maeneo mengine changamoto kubwa ya maji wananchi wamejikuta wana-share maji pamoja na mifugo jambo ambalo ni hatari sana kwa afya za wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nitazungumzia sana changamoto kubwa pia iliyopo katika Jimbo la Tunduma iliyo ya muda mrefu. Changamoto ya maji imekuwa ni kubwa sana ndani ya Jimbo la Tunduma na changamoto hii imepelekea wananchi watumie muda mwingi sana kwenda kuyatafuta maji, badala ya kufanya masuala mengine yanayohusiana na maendeleo ya Taifa letu. Lakini pia ndani ya mji wa Tunduma kuna mradi mkubwa wa maji ambao ulikuwa umeshafanyiwa upembuzi yakinifu tangu mwaka 2013 na Kampuni ya Networkers ya Marekani.

Mheshimiwa Spika, upembuzi huu ulifanyika kutoka Mto Songwe Ileje na kuja kuyaleta maji katika Jimbo la Tunduma, jambo ambalo mpaka leo halijatekelezeka na bado wananchi wa Tunduma wana kilio kikubwa cha changamoto ya maji.

Mheshimiwa Spika, nitaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anakuja hapo atuambie ni lini mradi huu utaanza kutekelezeka ili wananchi wa Mji wa Tunduma waepukane na changamoto ambayo wamekuwa wakiipata kwa muda mrefu zaidi?

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna mradi mwingine wa maji kutoka katika Wilaya ya Mbozi. Mradi huu unatoka katika Kijiji cha Ukwile na ulikuwa ukiwahudumia wananchi wa Kata ya Mpemba na Kata ya Katete. Mradi huu kutokana na ubovu na uchakavu wa ile miundombinu, kwasababu miundombinu iliyopo kwenye ule mradi ni ya mwaka 1971, hivyo miundombinu hiyo imechakaa sana, na kupelekea wananchi kushindwa kupata maji. Lakini nitaomba pia Waziri atakapokuwa anakuja atuambie ni lini watafanya mabadiliko wa ile miundombinu ili wananchi wa Kata ya Mpemba na wananchi wa Kata ya Katete waweze kuwa na uhakika wa kupata maji safi na salama kutoka katika mto Ukwile. hii inaweza ikatusaidia sana kutokana na changamoto kubwa ambayo inawakuta wananchi wa mji wa Tunduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Lakini changamoto nyingine kubwa ni kwa wananchi kusomewa bills zisizo sahihi. Hiki ni kilio cha maeneo mengi sana ndani ya Mji wa Tunduma na ndani ya Mkoa wa Songwe kwa ujumla. Changamoto hii imekuwa ikiwakabili wananchi wanapewa bills kubwa ambazo ni tofauti na uhalisia wa maji ambayo wanakuwa wameyatumia kwa wakati huo; jambo ambalo limekuwa likiwaumiza sana wananchi wetu,

Mheshimiwa Spika, ningeomba kuishauri Wizara. Wana sababu ya kuhakikisha kila mwananchi wanae mhudumia kwenye suala zima la maji wafunge mita ili waweze kupata uhalisia wa gharama ambazo wanakuwa wanawatoza wananchi wetu. Kwasababu hatimaye wananchi wetu wamebaki wakiumia, wanatoa kodi kubwa tofauti kabisa na ule uhalisia wa matumizi yao yam aji. Tunaomba hili lizingatiwe kwasababu linawaumiza sana wananchi wetu (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala zima la upotevu wa maji. Katika ripoti ya CAG ya Machi, 2022 inaonesha kabisa kwamba kuna tatizo kubwa ambalo linaikabili Wizara la upotevu wa maji; changamoto ambayo imesababisha Wizara kupata hasara kubwa. Ukisoma katika ripoti ya CAG inaonesha kwamba kwa mwaka 2020/2021 upotevu wa maji uliigharimu mamlaka kiasi cha Shilingi bilioni 175. Hii ni gharama kubwa sana ambayo pengine ingeweza kutusaidi hata kuendeleza miradi katika maeneo mengine ambako haiwezekani kabisa, kumekwama kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini leo hii nazungumzia mradi wa kutoka Ileje kwenda Tunduma pengine kusingekuwa na hizi changamoto fedha hizi zingeweza kutusaidia hata sisi wananchi wa mji wa Tunduma kuweza kutatua changamoto ya maji. Kwasababu ukirudi kule Tunduma huu mradi ninaouzungumzia unagharimu kiasi cha Shilingi bilioni tatu tu. Sasa kama tunaweza kupoteza fedha Shilingi bilioni 175 Shilingi bilioni tatu inawezaje kutushinda. Hili tunaomba Wizara pia ilizingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini changamoto kubwa ninayoiona, Wizara ina sababu ya kuongeza watumishi katika eneo la maji ili waweze kufanya ufuatiliaji kwenye maeneo ambayo wanawahudumia wateja. Kwasababu sababu wanazozitoa hapa zilizosababisha kupata hasara hii kubwa ni kama vile wateja kujiunganishia maji kinyume na utaratibu. Jambo hilo limepelekea Wizara kupata hasara kubwa sana. Jambo la pili ambalo wanalisema ni kuvuja kwa mabomba.

Mheshimiwa Spika, sasa, Wizara ikipata watumishi wengi katika maeneo ambayo wanawahudumia wateja hizi changamoto zinaweza kupungua na hatimaye hatuwezi kuwa na idadi kubwa ya upotevu wa maji kiasi ambacho tunapata hasara kubwa. Tuombe hili lizingatiwe. Wizara ione umuhimu wa kuongeza watumishi katika sekta ya maji ili waweze kufanya ziara na kutembelea yale maeneo ambayo wanatoa huduma kwa wateja…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)