Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami niungane na wenzangu kumpongeza sana Waziri wetu wa maji ndugu yetu Jumaa Aweso na Engineer Maryprisca Mahundi, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, viongozi wa mamlaka za maji, RUWASA na wale wa mabonde kusema ukweli hawa watu wanafanyakazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa jinsi inavyoiangalia kwa jicho la huruma hii Wizara yetu ya Maji. Lengo letu ni kuhakikisha kwamba vijiji wanapata maji kwa asilimia 85 na mijini asilimia 95. Mpaka sasa hivi vijijini tumeshafikisha asilimia 74.5 na mijini tumeshafikisha asilimia 86.5. Kwa hiyo naipongeza Serikali kwa jinsi inavyopeleka fedha za kutosha katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu ilikuwa imetenga Shilingi Bilioni 785.9, na hadi kufikia mwezi Machi tulishapeleka asilimia takriban 77, bado asilimia 23 tu. Kwa hiyo, najua Serikali ikimalizia hii asilimia 23 iliyobakia Wizara itaendelea kufanyakazi nzuri; na kutokana na upatikanaji huu wa fedha, Jumaa Aweso na wenzake wanafanyakazi nzuri wanang’ara vizuri kabisa. Wamejitahidi kuhakikisha kwamba ile kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mama ndoo kichwani wanaitekeleza kwa vitendo kwa sababu kuna fedha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukubaliane kwamba takriban kila Mbunge hapa ana mradi mmoja au miwili ya maji. Kwa hiyo nitashangaa tunapopitisha bajeti ya Wizara hii; mimi ninawaomba kwa sababu mimi ni Mbunge wa Kamati inayoisimamia hii Wizara tupitishe ili Jumaa na wenzake wakafanye kazi vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kusimamia Wizara hii tulitembelea miradi ya maji kukagua kama wanafanyakazi vizuri. Tukaenda katika mradi wa Kimbiji – Mpera huko Dar es Salaam tukatembelea mradi wa Mlandizi – Chalinze, tumeona maajabu, DAWASA wanafanyakazi nzuri; na tulipendekeza, Mameneja wengine waende kwenye maeneo hayo wakajifunze jinsi ya kufanyakazi kama yule wa DAWASA, nampongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kutembelea hii miradi lakini pia, katika hotuba ya Waziri ameonesha miradi ambayo imekamilika. Kwa mfano, kufikia mwezi wa Aprili miradi 303 ya vijijini ilikamilika, kuna miradi 127 iliyokuwa chechefu ameshakamilisha. Kuna miradi ya mijini 40 ambayo pia imeshakamilika. Yote hii ni kazi nzuri anayofanya Waziri pamoja na wenzake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka huu ameomba kupatiwa kiasi cha Shilingi Bilioni 657.9, na anategemea kukamilisha miradi na kutekeleza miradi mingi mipya ambayo kwa ujumla wake vijijini kuna miradi kama 1,029 yenye fedha nyingi ambazo ameonesha; mabwawa 15 na miradi ya mijini 175. Hii yote ni kazi nzuri ambayo Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi inataka ifanyike ili akina mama wasipate shida ya maji. Kwa hiyo, nirudie tena kuwaomba Waheshimiwa Wabunge tupitishe bajeti ili Jumaa aendelee akafanye kazi pamoja na wenzake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nirudi kwenye Jimbo langu la Moshi Vijijini kwa sababu kuna changamoto kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kata ambayo ninatoka ya Kibosho Kirima nikiri hapa kwamba Mbunge wenu huwa ninakwenda Jimboni kila nikitoka hapa, lakini mwaka mzima uliopita mwaka wote kwenye bomba langu pale nyumbani hakuna maji. Kwa hiyo najua una mipango mizuri naomba mtusaidie, ili mimi Mbunge wenu na wale wananchi wangu wapate maji ya kunywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Kibosho Kati ambaayo ina vijiji 14 kati ya Kibosho kati na Kibosho Okaoni watu wameongezeka sana na mradi wa zamani hautoshelezi mahitaji ya watu pale. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri uangalie hizi Kata mbili vijiji 14 ni watu wengi, ili tuboreshe ile miundombinu wapate maji ya kunywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Kibosho Magharibi hapa kuna vijiji nane ambavyo havijapata maji. Kata hii kwa sasa hivi ilikuwa inapata maji kutoka eneo la Mheshimiwa Saashisha. Tunaiomba Wizara kwa jicho la huruma tutafute chanzo kwenye DC yetu, ili tuwaletee hawa watu maji ya kunywa nao wanufaike kama watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Mabogini kuna vijiji ambavyo tangu tupate uhuru vilikuwa havina hata maji ya mfereji kwa mfano, kule Umasaini. Niliuliza swali la nyongeza hapa bado narudia kukuomba Mheshimiwa Waziri kule Umasaini kule Remiti tuhakikishe tumepeleka maji ili wale wafugaji na wananchi wengine wapate maji ya kunywa.

Katika Kata ya Old Moshi Mashariki nakushukuru sana umenipa Shilingi milioni 400, Engineer Kija Limbe anajitahidi, lakini ninaomba, ikiwa ni pamoja na pale Kata ya Mbokomu, manunuzi myaboreshe ili hawa watu wapate maji ya kunywa na tuendelee kuisifia Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi. Katika Kata ya Kimochi pia nashukuru tulipata Shilingi 500,000,000 kazi imeshaanza naomba tuchakarike ili hii miradi ionekane na watu wanufaike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Uru Kusini katika ripoti ya CAG alisema kwamba yale maji ni machafu na hayafai kwa matumizi ya binadamu. Mheshimiwa Waziri watu wameshaogopa kwa sababu CAG ameshaandika kwamba yale maji yana matatizo. Naomba mje muangalie ili tuangalie tutakavyowasaidia hawa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaushauri kidogo; mambo ni mengi nitapeleka kwa maandishi. Kwa kuwa changamoto kubwa kule Kilimanjaro imekuwa ni upatikanaji wa vifaa ninashauri muwe na mkakati wa kuhakikisha kwamba, procurement inafanyika mapema miradi inasainiwa mapema ile ambayo haihitaji Force Account. Kwa hiyo, manunuzi yafanyike ili hao Mameneja wetu wa RUWASA na yule Mkurugenzi wa MUWASA apate vifaa kwa wakati kwa sababu shida kubwa tumeona ni kwenye ununuzi wa vifaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)