Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nimshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ameendelea kutujaalia uzima na kutuwezesha kuifanya kazi hii ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na mimi kwa kuungana na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Timu yenu yote mnafanyakazi nzuri sana na kazi yenu inatubariki sana; tunawapongeza tunawatia moyo muendelee na kazi hiyo. Mheshimiwa Waziri kwenye Wizara yako siyo ninyi tu Wizarani hata ukienda kwenye taasisi zenu sisi wa vijijini tunabarikiwa na kazi nzuri sana inayofanywa na wenzetu wa RUWASA. Mkurugenzi Mkuu anajitahidi anafanyakazi vizuri. Kule Tanga sisi Injinia wetu wa Mkoa anafanyakazi nzuri na kipekee sana Meneja wetu wa RUWASA wa wilaya na timu yake nzima. Kwenye kazi huweza kuwa kuna changamaoto lakini kijana yule anajitahidi anafanyakazi nzuri muendelee kumtia moyo sisi tunamtegemea na anaifanyakazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kumpongeza Waziri na timu yake, napenda nitumie nafasi hii katika kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Wizara ya Maji, kumpongeza sana sasa sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa mambo makubwa mawili; jambo la kwanza kwa kujiongeza na kutafuta fedha nje ya utaratibu wetu; fedha kwa ajili ya UVIKO, zimetusaidia sana kwenye upande pia wa sekta ya maji. Jambo la pili, kipekee ninampongeza sana Mheshimiwa Rais na Serikali yake; kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwenye ule ukurasa wa 10 mpaka Mwezi Aprili, wizara imepokea fedha kwa asilimia 95 ya matarajio tuliyoyaweka kwenye bajeti. Tunavyosema mama anaupiga mwingi wako watu wengine wanakuwa na mashaka mashaka na wengine wanakuwa na maswali. Kunawezi kuwa na changamoto za ndani, za kitaifa lakini haiondoi ukweli kwamba mama anaupiga mwingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwenye hili nitafanya tu rejea ya maeneo machache. Tumepokea fedha kwa asilimia 95 mpaka Mwezi Aprili, 2022. Nimekwenda kutafuta hotuba za bajeti za Wizara ya Maji, nikachukua na maandiko mengine, mwaka 2017/2018 mpaka mwezi Machi, 2018 fedha za maendeleo zilitoka kwa asilimia 12.3, matumizi ya kawaida ilitoka asilimia 73. Mwaka 2018/2019 mpaka mwezi Machi, 2019 fedha za matumizi ya kawaida zilikuwa asilimia 68, fedha za maendeleo zilitoka kwa asilimia 51; nimekwenda Mwaka 2019/2020 matumizi ya kawaida tulipewa kwa asilimia 70 mpaka mwezi Machi, matumizi ya maendeleo kwa asilimia 74. Lakini mwaka uliopita 2021 Mpaka mwezi Aprili, 2020 zilizotoka kwenye bajeti zilitoka kwa asilimia 72 kwa matumizi ya kawaida na asilimia 53.4 kwa matumizi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumza kwenye bajeti hii Wizara imepokea fedha kwa asilimia 95. Huu ndio ushahidi kwamba mama anaupiga mwingi sana. Kizuri zaidi sio tu kwenye kutoa fedha; sisi wote ni mashahidi, fedha zinatolewa kazi inafanyika na kazi inaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikichukua mfano wa Jimbo la Korogwe Vijijini tuna miradi zaidi ya mitano ambayo imekamilika; na miradi sita ambayo ipo kwenye hatua mbalimbali inaendelea sasa hivi na miradi minne tunatarajia kusaini mikataba wiki inayokuja na nina miradi mitano iko kwenye hatua mbalimbali za manunuzi hakika mama anaupiga mwingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo kwa kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Rais lakini na Serikali yake, na kwa hiyo kwa pongezi hizi mimi sina mambo mengi; nina maombi tu machache nikukumbushe wewe na wenzako wa Wizarani ili kazi iweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi ule wa maji wa Vuga – Mlembule pale Mombo ni wa muda mrefu umeshatoa fedha. Kuna uzito kidogo kwa upande wa ule mradi wa kule Lushoto, ambako ndiko kwenye chanzo cha maji. Tusaidie kuongeza nguvu mradi huo ukamilike tuwape huduma ya maji watu wa Mombo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la pili, nimeona kwenye ukurasa wa 56, umesema vizuri sana kuhusu Mradi wa Maji wa Miji 28, na umesema tayari kila kitu kimekamilika tunasubiri kusaini utekelezaji wa miradi hii ukaanze. Naendelea kukumbusha Wizara yako, katika ile miradi ya miji 28 ambayo inaanza sasa kwa fedha kutoka India; kuna miji ya Muheza kwa akina Hamis, Handeni na Korogwe Mjini chanzo chao maji kiko pale Jimbo la Korogwe Vijijini Kata ya Mswaha. Ninakuomba sana kama tulivyokuwa tumeomba tangu mwanzoni tutakwenda kwenye utekelezaji, vile vijiji vilivyojirani na kile chanzo msikisahau vijiji vya hii Kata ya Mswaha viweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni mradi wa maji wa Mwanga – Same – Korogwe. Umeusema vizuri sana kwenye ukurasa wa 55 wa hotuba yako, na umeeleza changamoto ulizokutana nazo na hatua tulizochukua. Mimi nikuombe, baada ya kupitisha bajeti hapa hebu kaongeze nguvu jambo hili likamilike ili mradi huu ukamilike watu waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maombi hayo matatu ombi la nne, tulizungumza na Mheshimiwa Waziri kuhusu Bwawa la Mayuyu, na ulikuwa umeniahidi kwamba kesho ungekwenda kufanya ziara, na watu wa Korogwe wanakusubiri. Ninakuomba sana tuliangalie tuwajali wale watu bwawa lile ni bwawa muhimu ndilo wanalolitegemea kwa ajili ya kupata huduma za maji na huduma nyingine kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Mkoa wa Tanga ni miongoni mwa mikoa nane ambayo haimo kwenye ule mradi wenu wa EP4R; na huko nyuma tumekuwa tukihudumiwa sana kwenye miradi yetu midogo midogo iliyo mingi kupitia mradi wa PbR. Tunajua program ya PbR ndiyo inakwenda mwishoni PbR5 ndiyo ya mwisho mradi una-Phase Out. Tunawaomba sana Wizarani mtusaidie kupata mradi mwingine wa aina hii au mtuunganishe na wenzetu wale wengine ambao wako kwenye EP4R na sisi tuweze kupata huduma za miradi hii midogo midogo ili wananchi wetu waweze kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, Mheshimiwa Waziri unatambua changamoto niliyonayo kwenye Kata za Mkomazi, Mkalamo, Magambo Kwalukonge na Mpale. Kata hizi zinachangamoto kubwa ya vyanzo vya maji. Tumeamua na ninyi Wizarani mliamua kutusaidia mradi mkubwa kutoka kwenye maji ya Mto Ruvu. Mkatuahidi kututafutia mshauri kwaajili ya kuja kufanya kazi ya usanifu na upembuzi yakinifu. Tunaomba mchakato huu uharakishwe kidogo, tumeusubiri kwa muda mrefu ili mambo yaende vizuri ili tumalize maeneo haya machache, tuunganishe na yale maeneo mengine makubwa ambayo watu wa Korogwe wanapatia huduma ya maji ili mambo yao yaweze kwenda kuwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninakushukuru sana kunipa nafasi. Ninaunga mkono hoja ninawatakia kila la kheri katika kutekeleza bajeti mtakayopitisha. Ahsante sana. (Makofi)