Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kidogo kwenye hoja hii ambayo ipo mezani; na nijielekeze moja kwa katika pongezi. Nipende kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Jumaa Aweso na Naibu wake pamoja na watendaji wote pale Wizarani, nikianza na Katibu Mkuu, Wakurugenzi lakini pia Mtendaji Mkuu wa RUWASA, Injinia Clement kwa kweli wameonesha wanatekeleza shughuli zao vizuri sana na wanastahili pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukijaribu kuangalia taarifa ya utekelezaji kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, hali ya upatikanaji wa maji lengo mpaka 2025 kwa upande wa vijini ni asilimia 85 lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza Wizara imeshafanikiwa kwa kiwango cha Asilimia 74.5 upatikanaji wa maji safi na salama vijijini; lakini pia asilimia 86.5 kwa upatikanaji wa maji salama mijini. Haya ni mafanikio makubwa sana, tunaendelea kuwapongeza Waziri na timu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafanikio katika utekelezaji wa miradi mpaka tunavyozungumza sasa hivi kwa mwaka wa fedha tunaoumalizia, Wizara imekwishatekeleza miradi kwa kiwango cha percent 95. Hayo ni mafanikio makubwa sana, na tunaipongeza wizara kwa kazi nzuri hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisoma Pugu miaka ya nyuma hiyo, wakati nasoma pale A level tatizo la maji lilikuwa nightmare. Lakini mwezi Machi nilikwenda kule nikiwa kwenye ziara ya Kamati yetu nikakuta Wizara imetekeleza mradi, pale Kisarawe kuna tanki la lita milioni 10 na kuelekea upande wa Pugu kuna tanki la lita milioni mbili maana yake ni kwamba lile tatizo la maji Pugu limemalizika. Nilifurahi mno, nilibubujika furaha; nichukue nafasi hii kwa kweli kipekee kabisa kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na watumishi wote wizarani kwa kazi nzuri ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mafanikio ya wizara hayakuishia Pugu hata kule jimboni kwangu mambo ni mazuri. Kuna mradi ambao unaendelea sasa hivi katika Kata ya Keri na kwa Lusambu mradi wa maji Kijiji cha Patandi wenye thamani ya shilingi bilioni 2.7, Mkandarasi yupo kazini. Tunashukuru sana na tunapongeza Serikali kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, kuna mradi wa milioni 379 Kijiji cha Nshupu wa uboreshaji, kazi inaendelea tunaishukuru sana Serikali na kumpongeza Waziri. Pia kuna Mradi wa Kijiji cha Nkure milioni 502 wa fedha za UVIKO utekelezaji unaendelea, tunaishukuru na kuipongeza Serikali. Aidha, wakati Waziri walivyokuja kwenye ziara jimboni kwangu kukabidhi Kituo cha Utafiti wa Kuondoa Madini ya Fluoride kwenye Maji ambapo ilikuwa kinakabidhiwa Chuo cha Maji, Mheshimiwa Waziri ali-initiate mradi wa kuboresha upatikanaji wa maji Kijiji cha Kiwawa na Ngongongare na akatoa Shilingi milioni 100 kama fedha za awali. Mradi ule ni Shilingi bilioni, 1.6. Kazi inaendelea na RUWASA na AUSA wanashughulikia hiyo kazi. Tunashukuru na kuipongeza Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa Imbasen, Kikatiti na Maji ya chai wa gharama ya Shilingi bilioni nne. Nasikia sasa hivi utekelezaji bado upo kwenye stage ya manunuzi. Tunashindwa kuelewa ni kwanini huo mradi umechelewa sana kwa sababu ulikuwa unapaswa uanze wakati mmoja na mradi wa Patandi. Niweke angalizo kwamba inaelekea RUWASA wanakumbatia sana sana taratibu za manunuzi, hawajaweza kuzi-delegate chini kwa Mamlaka za Mkoa na Wilaya. Ni vizuri wakafanya delegation ili hizi kazi zikafanyika haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mafanikio ya wizara si bure, ni reflection ya kazi nzuri ambayo inafanywa na Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. Nichukue nafasi hii kipekee kabisa na kwa dhati ya moyo wangu kumpongeza kwa kazi nzuri ambayo anaifanya, anatubeba Watanzania kama watoto wake. Hata ukiangalia anavyohangaika; juzi tulizindua Filamu ya Royal Tour ambayo kimsingi imekuja kuitangaza nchi yetu hasa kwenye utalii. Yote kwa ajili ya kuhakikisha kwamba watanzania tunatoka hapa tulipo tunakuza utalii kwa maendeleo ya nchi hii. Lakini pia mwaka jana alituletea fedha za maendeleo nje ya bajeti ambapo hivi fedha milioni 502 ambazo na sisi tumepata Kijiji cha Nkure zilielekezwa kutoka kwenye lile fungu Shilingi trilioni 1.3.; tunamshukuru na tunampongeza tunamuombea maisha marefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mengi ya kuzungumza lakini nasiki kengele imeshalia, basi nichukue nafasi hii kukushukuru sana naunga mkono hoja, ahsante sana.