Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi ya kuchangia. Kwa kweli leo kama kanuni zingekuwa zinaruhusu ningekuomba tungeimba nyimbo moja ya msemaji mkubwa sana wa timu kubwa nchini; kwamba hawaamini macho yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka mingi watu wengi walikuwa wanafikiri utekelezwaji wa Bajeti ya Serikali hasa kwenye hii Wizara ya Maji ulikuwa ni mdogo sana. Lakini kwa namna ya pekee kupitia hotuba ya Waziri mwenye dhamana ametuthibitishia Watanzania, kwamba Mama, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka huu ametoa asilimia 95 mpaka sasa ya bajeti ambayo iliombwa na Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa namna ya pekee kwa niaba ya Watanzania na hususani wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini nampongeza sana Mheshimiwa Rais na Serikali yake kwa kuwekeza nguvu kwenye miradi hii ya maji ambayo ni changamoto kubwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili nipongeze watendaji wa ngazi za chini. Pale Mkoa wa Pwani na Wilaya ya Kibaha tunao akina mama wawili Engineer Beatrice na Engineer Debora kwakweli ni akina mama wa mfano kwasababu wanashughulika sana na matatizo ya maji kwenye maeneo mbalimbali vijijini. Niwapongeze sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi kwenye hotuba ya Waziri ukurasa wa 14 ameonesha miradi inayotekelezwa kwa ajili ya utunzaji wa vyanzo vya maji. Nimeamua nianzie hapa nami kumuonesha sehemu ya chanzo cha maji ambacho kinaharibika kwa kiwango kikubwa lakini hakijatengenezewa mradi wa kuweza kudhibiti uharibu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunakumbuka jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani unapata maji ya kunywa na matumizi mengine kutoka kwenye chanzo cha Mto Ruvu. Chanzo hiki cha Mto Ruvu kinaathirika na mambo mbalimbali ikiwemo kule juu ambapo kunakwenda kuchimbwa bwawa kubwa kwaajili ya kuhifadhi. Lakini pale jimboni Kibaha Vijijini kwenye eneo la Kitomondo Mto Ruvu umehama, umeondoka kwenye njia yake ya asili unakwenda kwenye maeneo mengine unapeleka maji kwenye mabwawa ambayo si chanzo cha mabomba yanayopelekea Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri Wizara na hasa watendaji walio karibu na chanzo hicho wangekwenda pale Kitomondo wakaone, wakazibe ule mto uliohama ambao umepoteza muelekeo wake. Badala ya kuelekea kwenye vyanzo mashine ya maji pale Ruvu chini na Ruvu juu umechepuka umeenda sehemu nyingine. Kwa hiyo maji mengi sana yanapotea yanaingiwa kwenye Bwawa linaitwa Bwawa la Mongomole, yanasababisha yasipite kwenye chanzo cha Mtambo wa maji hivyo kupelekea kwenye mitambo ile kuwa na maji machache na yanayopelekea Dar es Salaam kukosa maji kwa kipindi kikubwa. Kwa hiyo ningewashauri sana Serikali wangekwenda pale wakaone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hapa ingekuwa busara sana nikaomba, kaka yangu wa Kibiti alimuomba Waziri ikiwezekana Naibu Waziri aende kule Kibiti. Na mimi nitumie nafasi hiihii kabla hujafika Kibiti ungeruhusiwa usimame pale Kibaha twende ukaone ile hali ya Kitomondo halafu uweze kuitolea maelekezo ya kuokoa maji kwenda Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini baada ya maneno haya, lakini vilevile kwenye Hotuba ya Bajeti Mheshimiwa Waziri amezungumza suala la Mradi wa Maji ya kutoka Mlandizi kwenda Chalinze mpaka kule Mboga. Mradi huu umekamilika na ni mzuri niwapongeze sana Serikali, lakini tarehe 22 mwezi wa tatu tulipokuwa tunafanya uzinduzi wa Mradi huu pale Chalinze na Mheshimiwa Rais, Rais alitoa tamko la kuongeza fedha la takriban milioni 500 kwa ajili ya kuongeza vitolea maji kwenye maeneo kadhaa.

Nikuombe Mheshimiwa Waziri, Mradi ule hauelekei tu upande huo, Mradi ule pia unahudumia kipande cha kutoka Kata ya Gwata na Maghimbi ambavyo vipo ndani ya Jimbo la Wilaya ya Kibaha Vijijini. Lakini upande ule wa Jimbo la Kibaha Vijijini upatikanaji wa maji ni wa shida sana, kwa sababu inaonekana wale watumishi hawafungui pale kwenye maunganisho yanayopeleka maji kule. Kwa hiyo Chalinze maji yanatoka lakini Gwata maji hayapatikani, Magindu maji hayapatikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kitendo hiki kunapelekea wananchi wa Kata hizo wawe na maswali ya sintofahamu. Na wanatafakari maswali ambayo kwa kweli mimi kama Mbunge siwezi kuyauliza na kuyazungumza hapa. Sasa, niwaombe watumishi waweze kuzingatia utoaji wa maji kwenye mradi ule kwa maeneo yote ambayo bomba hilo limepita kwa sababu linahitaji kuwahudumia watanzania wote kwa usawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kwenye maeneo hayo ambayo ninasema kutokana na zile fedha ambazo Mheshimiwa Rais amezitamka siku ile ya tarehe 22 ni vyema tukafikiria kupeleka maji kutoka kwenye bomba kubwa kutoka pale linapotoka Gumba kwenda Ndwati, Kigoda na Ngware, ambako hawana kabisa maji na bomba limepita karibu na wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo upo Mji wa Mlandizi, Mji wa Mlandizi ndiko kwenye mtambo mkubwa sana wa maji unaozalishwa kupeleka Dar es Salaam. Wabunge wote wanaozungumza wa Mkoa wa Dar es Salaam wanazungumzia mtambo ambao uko pale Mlandizi. Cha kusikitisha ni kwamba Mlandizi palepale vipo vitongoji ambavyo havina maji, wanatumia maji ya kisima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimuombe Mheshimiwa Waziri, pamoja na kwamba tunafahamu kwamba mtambo ule ni kwa watu wote, lakini ni vizuri basi watu wa Vitongoji vya Msongora, Kidai, Kisadi, Madimla, Mwanabwito, Kikongo, Mkino na Lupunga wangeweza kupatiwa maji kwa sababu mtambo uko karibu na wao na bomba kubwa haliko mbali kutoka kwenye maeneo ambao wao wapo. Lakini cha kusikitisha maeneo hayo niliyoyataja wanatumia maji ya kisima, jambo ambalo kwa kweli siyo zuri. Tunatakiwa tuwapatie maji safi na salama na ufumbuzi wake ni kuwaunganisha kwenye bomba la maji ambalo linatoka pale katika Mradi wa DAWASA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na haya nimalizie kwa kuishukuru Serikali. Nimeona kwenye Kitabu cha Bajeti na kwenye Hotuba ya Waziri, katika miradi mipya inayokwenda kutekelezwa kuna Miradi ya Kwala, Kimara Misale, Ruvu station na Mradi wa Vinyenze, Uyombo na Masaki. Kwa kweli niishukuru Serikali kwa kupanga miradi hii ambayo itatekelezwa kwenye Jimbo letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nilikuwa nataka nitoe angalizo kidogo kwenye eneo lile la Kwala. Kwala ni eneo kubwa la kimkakati na sote tunafahamu kwamba eneo lile tumeliandaa kwa ajili uwekezaji wa viwanda na bahati nzuri wameshapatikana wawekezaji wa kuweza kujenga viwanda kwenye eneo lile. Huu Mradi kwa kadri ambavyo uliandaliwa, kwa sababu unasimamiwa na RUWASA, na mimi ninaufahamu Mradi huu kwa jinsi ulivyodizainiwa ulikuwa unaishia pale kwenye eneo la katikati katika maeneo ya Kwala. Lile eneo la viwanda haukuwa na mpango wa kupelekwa maji kwa sababu kulikuwa ni eneo kubwa la wazi.

Sasa kwa sababu tumeshapata wawekezaji na tayari wana nguvu ya kutaka kwenda kuwekeza pale; ningewashauri na ningeomba sana Serikali tufanye utaratibu wa kuutanua huu Mradi Kwala ufike kule kwenye maeneo ya Kwala ili wakati wanaana ujenzi watu hawa wasiwe wanapata tabu ya tatizo la maji. Waweze kuhakikisha kwamba ujenzi unaendelea na maendeleo ya hilo eneo uwe unatekelezwa kwa kadri ambavyo mradi umekusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kuna Mradi wa Mpiji ambapo amesema ulikuwa umekamilika kwa utekelezaji. Mheshimiwa Waziri naomba nikujulishe kwamba mradi huu kweli umekamilika lakini kuna changamoto kubwa ya upatikanaji wa majie. Hii ni kwa sababu chanzo ambacho wanakitumia katika huu mradi nikuunganisha kwenye bomba kubwa la DAWASA ambalo linaunganishiwa pale Tumbi. Lakini kutokana na mazingira yaliyopo na bomba lilounganishiwa Tumbi kuwa dogo maeneo haya Mpiji pamoja na Boko Mnemela hayapati maji kabisa. Hayapati maji kwa sababu inaonekana sehemu ambayo wameunganisha haina nguvu ya kutosha kupeleka maji kwenye maeneo haya. Nikuombe Mheshimiwa Waziri utoe maelekezo yako kwa watendaji wa DAWASA ikiwezekana walibadilishe lile bomba dogo ambalo wanasema linaanzia pale kwenye kile chanzo ili waweke bomba linalofanana na kupeleka maji kwenye maeneo hayo ili tuweze kuondoa adha hiyo ya watanzania kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya naunga mkono hoja, ahsante sana.(Makofi)