Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kauli mbiu yake ya kumtua mama ndoo. Wote tunatambua imeitikiwa sana na inafanya vizuri. Lengo la mama lilikuwa ni kuhakikisha kwamba kila mama anayetafuta maji ayapate ndani ya mita 200 na ndio maana umeona wabunge wengi hapa wanasimama kupongeza. Kwa hiyo tunamshukuru sana Mheshimiwa wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pili nimpongeze Mheshimiwa Waziri Aweso pamoja na timu yake yote bila kumsahau Mheshimiwa Engineer Naibu Waziri pamoja na timu yote kama ambavyo wanafanya kazi. Kimsingi wameonyesha nia thabiti ya kupata majibu ya changamoto ya uhaba na upungufu wa maji safi na salama; kama sehemu yao ya kazi ninawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri. Kuna wakati kule Mtwara uwa hakukaliki kabisa na sauti zilipaswa kwa kiasi kikubwa. Mheshimiwa Katani jana alisema, Mheshimiwa Waziri alikuja na alijionea hali halisi mimi hapa ndani kila ninaposimama ninakuwa nikiuliza maswali ya maji ya kuokota; na nilitamani sana Mheshimiwa Wiziri ama waziri mdogo Naibu Waziri wangekuja kujionea hayo maji ya kuokota.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wenzangu, kwa sisi wananchi wa Mkoa wa Mtwara bado changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuambie leo, kuna kipindi wakati wa kiangazi sisi wananchi wa Mtwara tunakosa maji hata ya kupikia chakula; na hiyo ilishuhudiwa na viongozi wetu wa Chama cha Mapinduzi Kitaifa, Mheshimiwa Naibu Katibu Mkuu, wali ulipikwa kwa maji ya tikiti sijui kama ninaeleweka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunavyozungumzia suala la upungufu ama uhaba ama hii changamoto ya maji safi na salama nadhani kwa Mkoa wa Mtwara ndio inaongoza, namba moja. Hata takwimu za upatikanaji wa maji, zile ambazo zimekuwa zikiandaliwa na wataalam kwenye mkutano wa RCC zilikataliwa, na hapo ilikuwa inaonyesha ni asilimia 61. Lakini kiuhalisia, kule vijijini maji hakuna kabisa ndiyo maana tunapopata mvua zinaponyesha yale maji yanayotiririka juu kabisa tunayakusanya tukichota kwenye ndoo tunayaweka ili lile tope likae chini halafu ndipo tunakunywa hayo maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba, kwenye hilo eneo tu, hivi Serikali ilishawahi kufanya coordination kati ya Wizara ya Maji na Wizara ya Afya ikajua kwamba ikitatua hii changamoto ya maji kwa kiasi kikubwa tutapunguza gharama za matibabu kule kwenye Wizara ya Afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara wamesema; mimi sisemi kwamba Serikali haijafanya kazi, imefanya, na Mheshimiwa Waziri alikuja na tumeona alikwamua miradi chechefu lakini pia yapo maeneo pia kwama vimeshimbwa lakini bado changamoto yetu ni kubwa sana hali ya upatikanaji wa huduma za maji vijijini tunavijiji 800 kati ya hivyo vijiji 800 vijiji visivyo na maji ni 324 unaweza ukajionea hali ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suluhisho la kwetu sisi ni maeneo mawili tu kwanza ni chanzo cha Mto Ruvuma ambapo kwenye kitabu cha waziri inasema hiyo ndio maeneo ya miradi ya kimkakati lakini pili ni chanzo chetu cha Makonde ambayo inajazwa kwa chanzo cha Mahuta Mkunya pamoja na Mitema.

Mheshimiwa Mqwenyekiti, sasa, ukienda kwenye chanzo cha Mitema reserve yake kwa mwaka ni mita za ujazo milioni 65 lakini kwa mahitaji ya watu wa Newala Tandahimba na Nanyamba kwa siku ni mita za ujazo elfu 27; ukifanya kwa mwaka ni mita za ujazo milioni 9.9. Ukienda Mtwara peke yake mahitaji ni mita za ujazo 21, na ukifanya kwa mwaka ni milioni 7.7. Total ya mahitaji yetu sisi kwa Nanyamba Mtwara Newala na Tandahimba ni mita za ujazo elfu 17 wakati chanzo cha Mitema uwezo wake kwa mwaka ni mita za ujazo milioni 65; maana yake ni kwamba inatumika kwa asilimia 27 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri watu huku wamepongeza, na wewe umekuwa ukisema ndio mheo wa mgonjwa ndio utaweza kutoa dawa. Nikuombe sana kaka yangu Aweso, hiki chanzo cha Mitema kitumike chote kiweze kutatua tatizo la maji kwenye hizi wilaya nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mradi hapa tumeona imeandikwa Makonde, lakini Mheshimiwa Waziri hatujui, hivyo scope ya mradi huu wa Makonde ni ipi? inaanzia wapi? Mawanda yake yanaanzia wapi na yanaishia wapi? Fedha zake pia hazionekani, ndiyo tunasubiri fedha za ndani, ni Shilingi ngapi, zitafanya nini, zitawanufaisha wananchi wangapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini, mimi bado naona kama hali ni tete na haitabiliki. Ukienda kwenye Mradi wa Kuboresha Miji 28 imetajwa pale Makonde. Sasa mimi nikawa najiuliza, hivyo beneficially wa Makonde ni akina nani? Haitaji kwenye kitabu. Je ni Newala, Tandahimba, Nanyamba, Mtwara? Sasa hapo ndipo ambapo panaleta kizungumkuti. Ni vema Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie, nani maana Makonde ni chanzo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti ninaomba sana; pamoja na hilo ukarabati wa mabomba ya Mtwara ukafanyiwe kazi kwa sababu yale mabomba bado yana miaka 40 na pengine tutakapokuja mwakani na sisi hatutasema kwa sauti hizi kwa sababu tutakuwa tumenufaika…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Agnes kwa mchango wako.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)