Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri Mheshimiwa Nape Moses Nnauye kwa uwasilishaji mzuri. Michezo na sanaa ni ajira kubwa sana duniani. Wizara ije na mipango thabiti ya kukuza michezo hususan mpira wa miguu kwa timu za wanaume na wanawake ili kuwapa vijana wetu fursa kubwa ya kupata ajira.
Suala la rushwa katika maamuzi ya mpira wa miguu ni janga la Taifa, aibu hii lazima ikomeshwe na Wizara husika. Kushinda mchezo na kushindwa katika mchezo ni haki ya timu zinazocheza. Mwamuzi anapofanya maamuzi kwa upendeleo anawanyima haki waliostahili ushindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu TFF itumie ushahidi wa video za michezo inayolalamikiwa kwa kutumia wachunguzi wenye kutenda haki ambao hawafungamani na upande wowote, ikithibitika kwamba kweli mwamuzi amependelea basi adhabu iwe moja tu, kumuondoa mwamuzi huyo asichezeshe mchezo wowote wa mpira wa mguu kwa miaka mitano. Pasiwepo na nafasi ya kuomba msamaha, rushwa ni adui wa haki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Morogoro Kusini kuna mwamko wa hali ya juu kwenye michezo na sanaa. Jimbo limeanzisha ligi ya jimbo ya mpira wa miguu. Timu kumi na saba za kata zitashindana. Mbunge ndiye amegharamia vifaa vya awali vya mipira, jezi na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ligi hiyo ni kwa wavulana mpira wa miguu na wasichana upande wa netball. Lakini pia kuna timu mbili za timu ya mpira wa miguu (soka) kwa wanawake. Naomba Waziri mwenye dhamana ya michezo nchini akubali kuwa mgeni rasmi wakati wa fainali za mechi hizi za ligi ya jimbo la Morogoro Kusini kwa tarehe tutakayokupatia hapo baadaye. Lakini pia tunaomba Wizara ichangie kata hizi kumi na saba zinazoingia kwenye ligi vifaa vya michezo kususan mipira ya kutosha, jezi na viatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la timu zetu za mpira wa miguu kutofanya vizuri chanzo chake ni uongozi. Viongozi wengi wa michezo wamejawa na ubinafsi, wasio na weledi na wanaotengeneza makundi ndani ya timu yao badala ya kujenga umoja kwenye timu.
Ushauri wangu Wizara iwaangalie viongozi wa timu zetu na kuwataka waongoze timu kwa misingi ya katiba na sheria, kanuni na kujenga umoja kwenye timu wanazoziongoza badala ya kubagua wanaowaongoza. TFF lazima ijiangalie yenyewe kiuongozi ili itende haki kwa timu zote bila ya kubagua. Naunga mkono hoja.