Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Nianze kama alivyozungumza ndugu yangu Mheshimiwa Saashisha, leo sitaki kabisa kumpongeza Mheshimiwa Waziri. Nitampongeza baada ya matokeo ya kile atakachokileta baadaye, baada ya michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge na namna atakavyokuja kuleta maboresho wakati wa kuweka mipango hii sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia ukisoma Mpango wa Miaka Kumi wa Serikali ambao tunakwenda kwenye viwanda na sera ambayo tunayo ya elimu ya leo hatuendi kutoa majibu ya kile tunachokwenda kukifanya kwenye Mpango huu wa Uchumi wa Viwanda. Hii iko wazi ukienda leo Shule ya Ufundi Mtwara ambapo tunatarajia tungepata mafundi hao watakaokwenda kufanya kazi viwandani kutoka kwenye mashule yetu, shule zetu za ufundi zinaendelea kufa. Mtwara Tech ukienda pale wamebadilisha badilisha mambo, kwa hiyo shule zetu za ufundi zinakwenda kufa, wakati tunakwenda kwenye uchumi huu wa viwanda maana yake ni lazima tuwe polytechnic schools.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ushauri wangu kwa Serikali, wenzetu Kenya wamefanya; ukienda Kenyatta University leo hata mitaala wamejaribu kubadilisha. Kozi zile nyingi ambazo zilikuwa za utawala ambazo sisi leo ndiyo tunazo; Vyuo vyetu vya kati vingi vinafundisha kozi za utawala badala ya kozi za ufundi. Maana yake yake ni nini? Ndiyo yale matokeo ambayo leo ukienda kwenye kuajiri utakuta bahasha 150,000 watu wanatafuta ajira kwa sababu tulishindwa kutengeneza mifumo ya shule za ufundi ambazo Watanzania wengi wangekwenda kufanya kazi kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye hili nimwombe sana Mheshimiwa Waziri. Leo vyuo vyetu vikuu; vipo vyuo vikuu na vyuo vya kati wanaendelea kutengeneza mitaala na kutengeneza kozi ambazo hata ukienda kwenye Ajira Portal hukutani na hicho kitu. Nenda Mipango pale kuna kozi unakutana na Bachelor Degree ya Development Finance and Economics; ukienda kwenye Ajira Portal, hicho kitu hukikuti kabisa na mzazi wa Tandahimba ameshampeleka mtoto chuoni, ame-grauduate pale, ana degree yake lakini kwenye Ajira Portal ya Serikali huioni hiyo kozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nenda Mwalimu Nyerere utakutana na wanafunzi wa namna hiyo chungumzima. Nenda TRA huko utakutana na makozi hayo wametoa ajira lakini wametengeneza kozi ambazo ukienda kwenye Ajira Portal hazitambuliki kabisa. Maana yake nini? Tunaendelea kutengeneza mitaala ambayo haiendi kumsaidia Mtanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri atakuja kulisaidia Taifa hili kama watakaa chini sasa, tukatoka kwenye mitaala ya kikoloni ambayo ndiyo tunaitumia; maana ndiyo ukweli wa wazi huo. Tunaendelea kutumia mitaala ya kikoloni, mwanafunzi unampa masomo 11, anapokwenda form five, six anakwenda kuchagua masomo matatu, lakini ulimpa mzigo wa masomo 11 au 12. Cheti cha form four mtu ana division one ukiangalia imejichanganya changanya hivi, wala hujui kwamba mtoto huyu uwezo wake halisi ni upi? Maana mwingine ana ‘A’ zote saba; kwa hiyo, unaamua wewe tu kwamba huyu mtoto sasa nimpeleke HGK lakini kumbe uwezo wake labda ni PCB.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa umefika wakati tuone siyo tu kuanzia darasa la saba watakapokaa kuandaa mitaala vizuri ikiwezekana tuwe na foundation hii ya darasa la kwanza na la pili, lakini kuanzia la tatu mtoto tayari aingie kwenye combination kama mtoto atakayesoma sayansi akasome sayansi; kama ni mtoto anakwenda kusoma arts akasome arts, kuanzia darasa la tatu watakuja kulisaidia Taifa. Tutoke kwenye kutoa hizi kozi nyingi ambazo ni za utawala wakati ni kozi ambazo zinakosa fursa za soko la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukija kwenye sera ya elimu, niseme hatuna sera ya kudumu ya elimu. Ukiangalia sera ya 2006 tulikuwa na sera ya exclusive education. Kabla hatujaitekeleza 2012 tukaja na jambo lingine elimu ya msingi iishie darasa la sita na lugha ya kufundishia iwe Kiswahili; toka 2012 ilishapitishwa huko. Leo tunarudi nyuma tunakaa hapa tunamwambia Waziri akae kutafakari sera sahihi ambayo tutakwenda nayo. Maana yake ni kwamba bado tunaendeshwa na sera za kikoloni ambazo kama tutaendelea na sera hizi za kikoloni, mitaala hii ya kikoloni maana yake Taifa hili tutaendelea kutumikishwa na wenzetu waliopo nje. Kwa sababu watakachokitaka wao ndicho tutakachokifanya. Sasa Profesa aende akatafsiri, elimu yake ije isaidie Watanzania na Taifa hili kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu Walimu wana kazi ngumu sana. Januari Walimu walishajiandaa tayari na scheme of work zao. Baadaye ukaja waraka ikaja kitu kinaitwa Kalenda ya Elimu; Walimu wakatakiwa wakae tena chini kuandaa scheme of work. Haijakaa vizuri kalenda, likaja jambo la sensa, Walimu wakakaa tena kutengeneza scheme of work nyingine, yaani ndani ya mwaka huu mmoja, Walimu wametengeneza scheme of work zaidi ya tatu. Hivi tunavyozungumza, Walimu wanafundisha kwa uzoefu tu siyo kufuata scheme of work; kwa sababu wanazo nne ambazo hawakuwahi kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye jambo hili Walimu hawa ambao tunawapa kazi kila dakika wanakaa kuandaa scheme of work inabadilika, wanakaa tena inabadilika, wawape mahitaji yao ya msingi kwama ilivyo askari. Askari tarehe 15 wanawapa allowance na walimu nao waanze kupata allowance kwa sababu kazi wanayoifanya ni kubwa kwenye Taifa hili. Hakuna watu wanaofanya kazi kubwa kama Walimu na wenyewe waingizwe kwenye allowance kama wanavyofanya majeshi kwa sababu wanabadilikabadilika, kila wanavyosema wanabadilika na walimu wanabadilika hivyo hivyo.

Kwa hiyo, niombe sana sana ikifika tarehe 15 Walimu nao wale allowance zao vizuri, lakini wapandishiwe mishahara yao, posho zao na kama kuna wanaowadai wawalipe Walimu hawa ili walete tija kwenye Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, wenzangu wamezungumza sana juu ya Baraza la Ushauri; hiki chombo Mheshimiwa Waziri akifanyie kazi kwa haraka sana. Atakuwa na chombo cha wataalam ambacho kitamshauri mambo ya msingi yanayohusu elimu ya Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa hili na kitamsaidia sana kupeleka elimu yetu mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)