Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti hii muhimu ya Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika maendeleo endelevu ya dunia na sisi kama nchi ambayo tunapaswa kuyatekeleza, lengo Namba Nne tunapaswa kuzingatia ubora wa kiwango cha elimu tunayoitoa kwa wanafunzi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri kwamba katika maendeleo ya nchi yoyote ile ubora wa kiwango cha elimu unamchango mkubwa katika maendeleo ya nchi husika. Ili Walimu wetu waweze kutoa kiwango bora cha elimu ni lazima wao wenyewe wawe bora zaidi kwa kuwa na ujuzi stahiki vilevile sisi kama Serikali tuweze kuwaendeleza Walimu hawa mara kwa mara ili waendane na mabadiliko mbalimbali ya kidunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Bajeti ya Elimu kama Wizara, Wizara hii ni nyeti sana lakini mara zote tumekuwa tukitoa Bajeti ambayo ni ndogo ya Wizara hii ili kuendeleza elimu yetu. Hata ukilinganisha katika nchi za Afrika Mashariki, Tanzania bado tuko chini kwenye bajeti tunayoitoa katika Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwango kile kidogo cha bajeti tunayotenga bado hatukipeleki kwenye eneo husika ili kuweza kuboresha kiwango cha ubora wa elimu tunayoitoa. Naishauri Serikali kwenye bajeti zijazo tuweze kutenga kiasi kikubwa cha bajeti kwa ajili ya kuboresha kiwango cha elimu tunayoitoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika vitu ambavyo vinaboresha moja kwa moja elimu yetu ni lazima tuwape mafunzo mara kwa mara Walimu wetu ili waweze kuendana na matakwa ya kidunia vilevile ni lazima tuwe na nyenzo za kutosha ikiwemo vitabu ili tuweze basi kutoa elimu hii yenye viwango.

Naishauri Serikali kwenye bajeti zijazo iangalie na ihakikishe pia inatenga bajeti ya kutosha kwenye miundombinu laini ili basi tuweze kuendana na matakwa haya ya kidunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie pia kwenye ufanisi wa Vyuo vyetu vya Kati ikiwemo VETA. Kama Kamati ilivyoshauri, imeshauri vizuri sana kwamba ujenzi wa Vyuo hivi vya Kati uendane sambamba na kuajiri Walimu wa Vyuo hivi. Natolea mfano tu pale Wilayani Ngorongoro - Samunge kuna Chuo cha VETA, chuo kizuri sana, kina majengo mazuri, chuo kina mandhari nzuri lakini kina uhaba mkubwa wa Walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chuo hiki kina uwezo wa kutoa wahitimu zaidi ya 500 kwa wakati mmoja ambapo pia kwenye hili, chuo hiki kingeweza kuhudumia hata Wilaya tatu ikiwemo Ngorongoro, Karatu na Monduli kwa wakati mmoja. Tungeweza kukitumia chuo hiki vizuri tungeweza kutatua tatizo kubwa la ajira kwa wanafunzi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo hiki ukiangalia kwa sasa kina Walimu Watano tu, idadi ya Walimu inayohitajika ni ziadi ya Walimu 30 mpaka 40. Naomba Wizara hii iweze kuzingatia maoni haya ya Kamati ili basi Vyuo vyetu hivi vya VETA viweze kuleta tija kwa wahitimu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la mikopo ya NMB ambayo Mheshimiwa Waziri ameeleza jana kwa kifupi sana kwa wahitimu wetu.

Kwanza kabisa naomba niwapongeze Benki ya NMB kwa kuona umuhimu wa kuwekeza katika elimu yetu. Japo kuwa Waziri jana alieleza kwa kifupi sana lakini jambo hili ni jema na linaonesha kabisa dhahiri kwamba litaenda kutatua tatizo la mikopo kwa wahitimu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama wawakilishi wa wananchi tunahitaji kulijua hili jambo. Hili ni jambo jema na zuri kwenye sekta hii ya elimu, kulijua vizuri na kupata ufahamu mpana ili basi tuweze kwenda kuwaambia wananchi wetu ambao tunawawakilisha fursa hizi watazipataje, ikiwemo tuweze kujua vigezo na terms mbalimbali ili wanafunzi wetu waweze ku-access mikopo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa ninaouwakilisha, Mkoa wa Arusha wanahitaji kufahamu watapataje mikopo hii ambayo inatolewa kwa riba nafuu na Benki yetu ya NMB. Naishauri Wizara pamoja na Benki hii ya NMB kwa pamoja waweze kuendesha semina kwa Wabunge kama wawakilishi wa wananchi ili tuweze kujua vizuri wananchi wetu watapataje fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)