Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niungane na Wabunge wenzangu na Watanzania wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa majaliwa yake kwetu sote.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili; nimpongeze sana Mheshimiwa Rais. Zipo sababu za msingi za kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu ya mikopo hii ambayo juzi tumepata ya COVID-19 kwa sababu imegusa mpaka mwananchi yule wa chini na tumepata miundombinu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zile sababu zinapopingana na mikopo hii ni sababu za kiuelewa tu kwa sababu kila mtu hapa anadaiwa na kila Taifa linadaiwa. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais na aendelee kutafuta fedha zaidi ili kutatua matatizo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nikupongeze Profesa na timu yako, Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na Watendaji wote kwa jinsi ambavyo mnaihudumia Wizara hii na kwa jinsi ambavyo mnaitendea haki. Hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza pia Wizara kwa mapitio ya sera na mitaala kwa wakati wa sasa. Elimu yetu ya sasa ni lazima iendane kukidhi matakwa ya wakati wa sasa na wakati ujao. Sera iweze kufanya mapitio kwa wadau wote ili kupata mawazo mazuri na namna ambavyo itakidhi haja pengine kwa miaka 50 ama pengine hata 100 kwa huko tuendako.

Mheshimiwa Naibu Spika, huku kila mmoja ana mawazo. Mimi nizungumzie hili suala la fikra ya Serikali kutaka kuondoa kada ya Maafisa Elimu Kata. Nadhani suala hili tulitazame kwa upana kabla ya maamuzi. Tunaweza kuwa na maamuzi tukafikiri kwa muda wa haraka yanatija lakini athari ziko. Kata moja ina shule mia na kitu, Maafisa kwenye Wilaya tunao wawili. Hivi ni kwa kiasi gani tunaweza tukawapanga wale Maafisa wa Elimu wa Wilaya wakasaidia kusimamia shule zaidi ya 100 ama shule takribani 100 na wale walioko kwenye hizo shule wakaweza kutoa tija na kutimiza majukumu yao bila usimamizi wa ngazi yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni tuliondoa Kada ya TRC’s hivi Vituo vya Ualimu. Muda mfupi baadae tukarudisha, nadhani kila jambo tunapoangalia tufanye tathmini lakini pia ushauri wangu kwa Serikali na hata Wizara kwenye Sera inayokuja kama kada hizi zilikosa majukumu na kazi za kufanya, basi tutazame majukumu ya kimsingi ya usimamizi wa kada hii na iwe imewekwa kwenye mitaala na kwenye Sera ya Elimu ili na wao tuone product yao au uzalishaji wako na ustawi wa eneo hili, kwa sababu siyo rahisi Walimu wa shule zote nchini wakafanya kazi bila usimamizi ambao ni wa utashi na kitaaluma na ambao unapimwa katika muda fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia mfumo ambao unatumika ingawa Wizara hii ni mtambuka na Wizara ya TAMISEMI. Kwa mfano, Watendaji Walimu Wakuu, Waratibu Elimu hawa TRC’s na Maafisa Elimu wa Wilaya, wanafanya vibaya kwenye eneo moja anapewa uhamisho kwenda kwenye eneo jingine wakati bado tuna rasilimali ya watendaji wazuri sana. Jambo hili ambalo baadae mwisho wa siku tunakuja kukuta alipokuwa amebomoa anakwenda kubomoa sehemu nyingine na yule ambaye anafanya vizuri kwenye eneo moja anahamishwa kwenda eneo jingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, badala ya kuwa na mfumo wa maboresho tunakuwa na mfumo wenye mkanganyiko wa Watendaji ambao tunawahamisha bila sababu za msingi badala ya kuwaondoa. Nadhani ifike mahali hatuoni haya, utendaji na usimamizi wa mtu ulingane na tathmini inayofanyika na mafanikio yanayopatikana kwenye nafasi ambayo ameteuliwa na mamlaka fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nimekupa jana mchango mkubwa sana wa maandishi, kutokana na muda huu wa dakika tano ambao siyo rafiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme kwamba twendeni kwenye eneo hili la chakula cha mchana shuleni. Bila kuwepo kwa chakula cha mchana kwenye Shule za Msingi, kuzungumzia eneo la ufanisi wa taaluma ni kazi bure. Kama ni kwenye eneo la mtaala tazameni kama ni Sheria au Kanuni itakayowataka wazazi kuhakikisha chakula cha mchana shuleni kwa wanafunzi ni lazima. Isiwe tena ni hiyari kama ilivyo kwenye maeneo mengi nchini na shule moja ya jirani inafanya vizuri na shule nyingine haifanyi vizuri, lakini shule hizo ziko kwenye eneo moja na mazingira yanafanana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo jingine ni semina za Kamati. Kamati za Shule tunapoteua, tunawateua kwa tabia zao, mienendo yao katika jamii, lakini baada ya kuwachagua hatuna namna yoyote ya kuwafanyia semina na namna yoyote ya mafunzo ili wajue majukumu yao na jinsi ambavyo wataisaidia jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nadhani kama inawezekana eneo hili pia la semina kwa Kamati za Shule ni muhimu sana ili kuleta uwiano mzuri na daraja zuri kati ya jamii yenye shule na shule yenyewe ili kupata ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango mwingine Mheshimiwa Waziri amezungumza kwenye hotuba yake. Miundombinu aliyozungumza ya nyumba za Walimu, majengo mengine. Mwalimu anakosa nyumba kwenye shule aliyopelekwa anatoka kilomita 10 ama kilomita tano kutoka mahali yalipo majengo ya kupangisha. Gharama tu ya kwenda kwenye hiyo shule na kurudi kwa mfano anakuja asubuhi kama ni 5,000/= ya bodaboda, mchana 5,000/= kwa ajili ya chakula, kurudi tena shuleni 5,000/=, kurudi tena nyumbani 5,000/=. Mshahara wa Mwalimu huyu unaisha kwenye gharama tu za kuhudumia nafasi yake bila kupata chochote na bila kuwa na manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nataka kuishauri Serikali, niungane na wale wenzangu wote waliozungumza namna ya motisha kwa Walimu na namna ya ruzuku ya ufundishaji kwa Walimu. Kada hii ya Ualimu vijana wetu wanaenda tu kwa sababu ya kupata ajira lakini kwa jinsi mazingira yake yalivyo na kama kuna kada zingine tunavyotoa motisha pengine kwa kazi zingine wanazofanya pamoja na zile za ajira na utumishi, tuna haja kubwa ya kuitazama upya ili kundi hili nalo tulione kwa moyo mkubwa na jinsi ambavyo kazi yao ya utume imetufikisha hapa tulipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la upungufu wa Walimu wa Sayansi limekuwa na athari kubwa sana. Vijana walioko Sekondari na hata wa Shule za Msingi wanashindwa kupata taaluma ya sayansi kwa majaribio na sayansi kwa kina kwa sababu Walimu hawa hatuwezi kuwaajiri kwa jinsi tunavyoona. Serikali itazame ni kwa namna gani walau hata shule moja inakuwa na Mwalimu wa Sayansi au hata wawili kwa sababu unakuta wanafunzi ni wengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa jinsi ambavyo maeneo mengine yana Walimu wa Sanaa, tunakosa Walimu wa Sayansi muda mrefu. Katika migao ya Walimu wa Sayansi, tutazame eneo hili kwa sababu muda wa wanafunzi wetu shuleni huwa hausimami unakwenda na mwisho wa siku wanafanya mtihani na ndiyo maana tunakosa Walimu wengi wa Sayansi kwa jinsi ambavyo hali inakuwa ngumu sana ya kuwaajiri kwa wingi unaohitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani Serikali ifanye tathmini ione namna gani sasa tunapata walau hao Walimu, hata kama siyo kwa kiasi kikubwa tuweze kupata eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni jinsi ambavyo matatizo ama mashtaka ya Walimu yanachukua muda mrefu sana. Unakuta Mwalimu ana mashtaka…

NAIBU SPIKA: Ahsante. Kengele ya pili hiyo Mheshimiwa.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, basi mchango wangu uungane na mchango ule wa maandishi. Naunga mkono hoja. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa kuandika jana na leo andika tena ni vizuri.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.