Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na ninaomba nimuunge mkono kabisa Mheshimiwa Kigua kwa hoja yake. Hoja yake iko wazi na ni halisi na Watanzania karibu wote wanaguswa na madhara ya upandaji wa bei za mafuta, na jambo la dharura huwa linatatuliwa kwa njia ya dharura. Kwa hiyo, nataka nikubaliane sana na wote wanaozungumza kutatua jambo hili kwa njia ya dharura huku tukiendelea na mipango ya muda wa kati na muda mrefu. Kwa sasa shida ipo na wananchi wanaumia sasa hivi tunavyozungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan halali kwa sababu ya jambo hili; Mheshimiwa Makamu wa Rais, Dkt. Philip Isdor Mpango halali; Mheshimiwa Waziri Mkuu halali; na Waheshimiwa Mawaziri na viongozi hatulali kwa sababu jambo hili naamini limetugusa sote na ndiyo maana hata Wabunge hamlali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunapokuwa na jambo kama hili, la kwanza ni maelewano kati yetu viongozi, jambo ambalo tayari nayaona mafanikio makubwa kwamba Bunge sasa na Serikali tunashikamana pamoja kujadili positively namna ya kutatua tatizo. Huu ni ushindi wa kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana jana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais, ameitisha kikao cha Mawaziri wachache, inawezekana tulikuwa wachache, lakini tulijadili jambo hili kwa uzito mkubwa mno na ndiyo maana Mheshimiwa Waziri akija atazungumza; na hata ile taarifa iliyotokana na kikao kile imezungumza baadhi ya namna ambavyo Serikali itachukua mawazo ya Wabunge katika kutatua tatizo hili.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakiniā€¦

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, hapa unachangia kama Mbunge. Kwa hiyo, Mbunge anatoa taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Neema Mgaya.

T A A R I F A

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kumpa taarifa mzungumzaji aliyetoka kuchangia hivi punde; kutokana na unyeti wa suala hili na michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge walioomba suala hili litatuliwe kwa uharaka kutokana na unyeti wa jambo hili, haoni kwamba kuna umuhimu sasa Bunge liahirishwe ili Serikali ipate muda wa kuchakata jambo hili vizuri na ikiwezekana kesho asubuhi mrudi na majibu ambayo yatakwenda kuwapa unafuu wananchi wetu? (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Neema hiyo haiwezi kuwa taarifa ya Waziri, kwa sababu yeye hana uwezo wa kuahirisha Bunge. Pia wakiulizwa; nilimwona Mbunge mwingine naye kauliza maswali kama Serikali imjibu. Hapa Serikali inachangia, mwenye hoja ni Mbunge. Mheshimiwa Omari Kigua ndio mwenye hoja, ndiyo maana atahitimisha yeye. Kwa hiyo, hawa hawawezi kuulizwa maswali ya kujibu na hata Mheshimiwa January Makamba atakaposimama anachangia, siyo anajibu hoja za Wabunge. Msianze kusema haikujibiwa hoja yangu, hapana. Mwenye hoja yuko kule na ni Mbunge.

Mheshimiwa Simbachawene, malizia mchango wako.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwamba Serikali tunaliangalia hili jambo na tunahitaji kwa kweli kutafakari kwa uangalifu mkubwa kwa sababu mnafahamu nyie wote Waheshimiwa Wabunge na tumeshiriki kutunga hapa sheria za fedha mbalimbali. Kuna maeneo ambayo huwezi kugusa kwa sababu ni statutory; yapo kwa mujibu wa sheria na yanatupatia mapato.

Mheshimiwa Spika, leo hii katika maamuzi ya jambo hili tukienda kwa fujo fujo, tukienda bila kutafakari, tujue kwamba tunaenda kuathiri miradi ya maji, tunaenda kuathiri miradi ya barabara, tunaenda kuathiri miradi ya ujenzi wa reli na tunaenda kuathiri miradi mingi ya TARURA. Kwa hiyo, tuwe makini. Haya yote ndiyo yanayotugusa na ni kipimo kwetu sisi Wabunge juu ya kuwaletea maendeleo wananchi wetu na tumeahidi na yapo kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, lazima tuwe makini.

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na mawazo yanayotolewa kwamba tuangalie masuala ya tozo na nini, lakini tumejaribu kuangalia hata hayo ni sehemu kidogo sana, kwa hiyo, inaweza isilete hata huo unafuu. Umakini mkubwa upo, lakini nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla, lazima tukipewa nafasi kama Serikali, muda siyo mrefu tunaweza tukaja na majibu kwa sababu Rais hawezi kushindwa kutupatia majibu Watanzania kwa sababu yeye ni Rais, ana uhalali wa kuamua chochote, hawezi akashindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali haiwezi ikashindwa kupata majibu. Kwa msaada huu wa mawazo ya Wabunge, haiwezekani tukashindwa kupata majibu. Mimi naamini tutapata majibu na tutajitahidi kabisa kupunguza kwa namna yoyote ile. Kupata majibu ni kupunguza bei. Ni kupunguza bei, hakuna njia nyingine, ni kupunguza bei. Tunapunguzaje? Tutafanyaje? Njia zote zitatumika kuhakikisha kwamba, tunapunguza. Kama ni ku-subsidize, kama ni kufuta kodi au vyovyote vile, tutafanya, maana sisi ndio tunaotunga sheria na tuko hapa wote na Rais yupo, analiona hili tatizo. Waziri Mkuu yupo, Makamu wa Rais yupo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naamini tutatoka salama, Waheshimiwa Wabunge watuamini Serikali. Nami nataka niwahakikishie kwamba, tukipewa muda siyo mrefu tunaweza tukaja na majibu.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Simbachawene kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Bilakwate.

T A A R I F A

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nataka kumpa taarifa mchangiaji anayeendelea na mchango wake: Pamoja na Serikali kuchukua hatua za dharura kupunguza bei ya mafuta, lazima Serikali iangalie huko vijijini ambako ndiko kuna wananchi ambao wanapata shida. Bidhaa zinapanda, lakini sehemu nyingine zinapanda siyo kwa sababu ya kupanda kwa mafuta.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu haiwezekani kitu kilichokuwa kinauzwa shilingi 2,000/= leo hii kimepanda zaidi ya asilimia 200. Kwa hiyo, pamoja na hatua mnazochukua kama Serikali, lazima mwangalie bidhaa huko chini ambazo zimepandishwa zinaendana na uhalisia?

Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Haya, ahsante sana. Mheshimiwa George Simbachawene.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa ya Mheshimiwa Bilakwate kwamba gharama nyingi za maisha zinapanda kwa sababu leo hii tunavyozungumza kutokana na maendeleo ya nchi hii ambapo hakuna kitongoji hakina chombo cha moto; hakuna kijiji hakina vyombo vya moto; kila mahali kuna vyombo vya moto; na kwa hiyo, usafiri ni karibu kila mahali. Ukitaka kutoa mazao shambani kwenda sokoni utapakia kwenye pikipiki, utapakia mgonjwa kwenye chombo cha moto. Kwa hiyo, kila kitu kitaguswa tu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni kweli tunafahamu kama Serikali na kwamba ni lazima tujitahidi kutumia njia yoyote kuhakikisha kwamba bei ya mafuta inapungua kama jambo la dharura.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda niunge mkono hoja ya Mheshimiwa Kigua na kwamba Serikali tunachohitaji kwa kweli ni muda wa kutafakari, tukikurupuka hapa tutaharibu na mambo mengine ambayo kwa kweli yapo na tulishayapanga sote kwa kushirikiana, na mengine ni mambo yaliyopitishwa na Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)