Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nami nianze kwa kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Kigua na nijielekeze moja kwa moja katika kuipongeza Serikali kwa hatua ambazo imeanza kuzichukua.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu amewaita watu, amewaita Viongozi wahusika na ametoa maelekezo ya Serikali, nami nishauri kwenye jambo hili la msingi ambalo linaathiri maisha ya watu kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, unapozungumzia suala la kupanda kwa bei za mafuta katika Jimbo la Sumve ni tofauti sana na unapozungumzia jambo hili na Dar es Salaam. Watu wa vijijini unaposema Mwanza mafuta yanauzwa diesel kwa Shilingi 3,300 Sumve ujue yanauzwa kwa shilingi 5,000. Kwa sababu watu wetu hawana vituo vya mafuta wanakwenda kununua kwenye vituo vya mafuta ndiyo wanakwenda kuuziwa huko vijijini, usafiri wetu mkubwa ni bodaboda, kwa hiyo, suala la mafuta sisi pia watu wa vijijini limetuathiri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana mchango wangu mimi wa moja kwa moja ninaiomba Serikali, katika hatua ambazo imeanza kuzichukua jambo la kuondoa tozo za Serikali kwenye mafuta ni jambo ambalo haliwezi kuepukwa. Umefika wakati ni lazima sasa tuacha kugeuza mafuta kuwa sehemu pekee ya kutafuta fedha. Ni lazima tufikirie njia nyingine kwa huu muda hali ya wananchi huko vijijini ni na mijini ni mbaya kwa sababu mafuta yapo juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo hapa nataka pia tuliangalia wakati Serikali inajadili na inafuatilia najua ina vyombo na ina taratibu zake, suala hili la mafuta mimi limenishtua kidogo, kuna bei ya diesel imeizidi bei ya petrol, lakini namna ilivyoizidi kwa Tanzania bei ya petrol nilikuwa naangalia kwa Dar es Salaam ni karibu Shilingi 110 tofauti ya bei diesel na petrol, lakini ukiangalia kwenye soko la dunia tofauti si kubwa kiasi hicho.

Mheshimiwa Spika, mimi ninaona bado kuna shida kwenye namna ya manunuzi ya hii bidhaa ya mafuta. Hili jambo linatakiwa liangaliwe kwa jicho la tatu, inawezekana tunazungumza bei kupanda lakini pia kukawa kunakuwepo bei kupandishwa. Inaweza ikapanda lakini ikapandishwa visivyo kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia Serikali iangalie na kwa kuanzia vigezo vya namna ambavyo hizi taratibu za manunuzi za kupata wazabuni wa kutuletea mafuta zinafanyika. Kwa sababu pia kuna sehemu zinalalamikiwa na humu tulishawahi kushauriwa na baadhi ya Wabunge kufikiria njia mbadala kuhusu namna ya kununua mafuta, tusilazimishe kiwepo chombo kimoja tu cha kununua mafuta. Haya ndiyo madhara na inafika wakati namna ya ku-control inakuwa vigumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo, nashauri kwamba namna ya mafuta haya tunayoyatumia, tunayoyalalamikia kupanda bei, upo umuhimu wa Serikali mbali na kujadili namna ya kupunguza tozo, iangalie namna ya kuona kama kulikuwa kuna utaratibu unaofaa uliotumika kwenye namna ya kupata watu wa kutuletea haya mafuta kwa sababu ya hizo bei ambazo zinamkanganyiko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu...

SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)