Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

NAIBU WAZIRI MADINI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kutumia dakika zangu tano kuchangia kwa kifupi kuhusu hoja yetu ambayo imepokelewa na kujadiliwa na Bunge lako Tukufu.

Mhehimiwa Spika, kabla sijasema mambo mawili, matatu kwa hizi dakika tano, niruhusu kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kunipa nafasi hii ya kuwa Naibu Waziri wa Madini. Leo ni mara yangu ya kwanza kusimama kuchangia kwenye hoja ya bajeti yetu kwa mwaka huu 2022/ 2023 na nikiwa chini ya Waziri wangu mahiri Dkt. Biteko, niseme tu kwamba kazi tuliyopewa na Mama Samia tunaisimamia usiku na mchana kwa uadilifu mkubwa na kwa umahiri mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru pia wewe Mheshimiwa Spika pamoja na Naibu wako kwa ushirikiano mnaotupa na niwapongeze kwa sababu na ninyi mmeingia kwenye nafasi hizi hivi karibuni, lakini mnavyotuongoza tutafika salama. Mungu azidi kuwaongoza katika kutuendesha katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo yaliyosemwa katika mjadala wa bajeti yetu ni mambo ya msingi ambayo kwanza Kamati yetu ya Nishati na Madini imeyafunika kwa asilimia kubwa kupitia kwenye taarifa yake na nipende tu kusema kwamba haya yote yaliyosemwa na Kamati na sisi tumekuwa na desturi ya kusikiliza ushauri wao na kufanyia kazi kila aina ya ushauri na mwongozo wanaotupatia kwa kuchambua kila hoja na kuifanyia kazi. Haya yote tumeyapokea na kwa kumsaidia waziri tunakwenda kuyafanyia kazi na baadhi ya mambo yameshaanza kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa maoni ya Waheshimiwa Wabunge katika maeneo mbalimbali ya ushauri waliotupa pia tumeyapokea na kuna eneo moja mahsusi ambalo nilipenda kuligusia zaidi nimwachie Waziri wangu atahitimisha yale mengine, ni eneo la wachimbaji wadogo. Ni kweli wachimbaji wadogo ndiyo kundi kubwa ambalo likiwezeshwa watakwenda kuinyanyua sekta ya madini ili iweze kuleta tija zaidi ya hapa tulipokwishafikia.

Mheshimiwa Spika, katika kutambua hilo sisi tumechukua juhudi za ziada kama Wizara na tutaendelea kuzifanyia kazi ya kuhakikisha kwamba tunaziwezesha hizi taasisi zetu zilizo chini ya Wizara hasa GST na STAMICO kwa kuwapa vifaa na kuendelea kuwaongezea rasilimaliwatu ili wafanye utafiti wa kina katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu yanapopatikana madini. Katika kufanya hivyo wataweza kubainisha maeneo mahususi yanayofaa kupewa wachimbaji wadogo, kwa sababu moja ya malalamiko ambayo yanajitokeza hapa ni kwamba mitaji inapotea wanawekeza katika maeneo ambayo ni ya kubahatisha.

Mheshimiwa Spika, sisi katika kutambua hilo STAMICO sasa hivi wao wameagiza mitambo mipya ambayo inakwenda kusaidia kwa bei punguzo, kuwasaidia wachimbaji wadogo kubaini madini yanayopatikana katika maeneo ambao wanapendelea kuchimba kwa aina ya madini ili waweze pia kupata dhamana katika mabenki yetu ambapo tumeshapata benki zaidi ya nne ambazo zimekubali kutoa mikopo ama ya fedha ama ya vifaa kwa wachimbaji wadogo; mabenki hayo ni NBC, KBC na CRDB. Hawa wote wameshasaini maridhiano na Wizara kupitia taasisi ya STAMICO kwamba wako tayari kutoa mikopo. Wachimbaji wadogo wanapoungana na kuunda vikundi vya uchimbaji wao wako tayari wakizingatia vigezo vya kuhakikishiwa na kudhaminiwa na Wizara kwamba wanayo maeneo yenye mashapu ya dhahabu au maeneo yenye madini ya vito, wapo tayari kuwakopesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baadhi ya wachangiaji wanasema kwamba masharti ni magumu. Masharti siyo magumu ni suala tu la kufuata utaratibu, ni suala la tukufuata vigezo vya kawaida kabisa ambayo wakivifuata kimoja baada ya kingine na sisi tukiwa tumewapa taarifa za viashiria vya uwepo wa madini katika eneo husika watakwenda kupata hiyo mikopo.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu naona muda ni mfupi sana nimalizie pia kwa hili suala Local Content na CSR.

Miongozo ya Wizara imewekwa bayana inadhihirisha kabisa kila mwekezaji anatakiwa aje na mpango wake wa CSR aje na mpango wake wa Local Content kwamba katika aina ya uchimbaji wanaofanya vifaa gani vinapatikana nchini na ataweka katika orodha ya database ambayo inaandaliwa na Wizara ataweka yaani ata- float yale mahitaji yote ambayo yeye anahitaji katika uchimbaji wake na watu wa ndani ndiyo wanaopewa kipaumbele na wale wengine yale yasiyopatikana nchini ndiyo yanayokwenda kuagizwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, CSR ni mwongozo ambao namshukuru Mheshimiwa Salome amelitolea ufafanuzi mzuri, ndivyo ilivyo, ni wao wenyewe ndiyo wanapambana kule katika halmashauri zao kwa sababu hawazingatii…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa mchango wako.

NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)