Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa wasilisho lake japo lina upungufu, lakini ndiyo mwanzo wa Serikali yetu ya Awamu ya Tano. Tuko hapa kwa ajili ya kuyaboresha ili angalau bajeti itakayokuja mwaka unaofuata waweze kuyarekebisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na suala zima la TBC. Kama alivyomaliza kuzungumza mzungumzaji aliyemaliza, mawasiliano ya TBC hasa kwa mikoa ya pembezoni bado hayapatikani na hususan katika Wilaya ya Lushoto ambayo ina population ya watu takribani 500,000 wanapata redio zinazotoka Kenya, hasa Mombasa na Nairobi. Sasa ipo hatari kwamba wananchi hawa watakuwa hawapati huduma za habari la Taifa lao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Nape pamoja na Mkurugenzi wa TBC Dkt. Ayoub Rioba, najua yuko hapa, kule Lushoto hatupati matangazo ya TBC. Mwandishi wa habari, ndugu yangu Suleiman Mkufya, tulikuwa naye kwenye kampeni, kila mahali alipokuwa anakatiza ndiyo swali alilokuwa anaulizwa kwamba mbona TBC Lushoto haipatikani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nizungumzie la soka. Nitatofautiana na wachangiaji waliotangulia kwa maana ya kuipa uhai timu ya Taifa. Naamini katika hii miaka ya karibuni hata tufanye vipi, hakuna miujiza ya kuweza kwenda kwenye mashindano makubwa kwa kupitia crash program. Bila uwekezaji wa maana kufanyika katika soka, soka haina njia ya mkato.
Nawapongeza sana wenzetu wa Alliance Academy wale wa Mwanza, vile ndiyo vitalu ambavyo vinaweza vikatufanya siku za usoni tuweze kuheshimika katika medani za soka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna Chuo cha Michezo cha Malya. Chuo hiki kilikuwa kinatoa elimu za michezo lakini kinatoa ngazi ya preliminary. Tunaomba Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi, waanze kuongeza, angalau kitoe mpaka ngazi ya diploma pamoja na ngazi ya Shahada. Tutakapokuwa na walimu wa michezo wa kutosha na tukawatawanya kwenye shule, ndiyo hawa baadaye wanaweza wakaleta tija kwenye ulimwengu wa michezo katika Tanzania yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi kama tunataka mafanikio ya njia ya mkato, basi tutayapata kupitia timu ya wanawake ya Twiga Stars. Twiga Stars ilikuwa inafanya vizuri sana na mara zote ilikuwa inafika hatua ambayo kama kungekuwa na uwekezaji wa maana, kama ingekuwa inatafutiwa wafadhili kama ambavyo zinatafutiwa timu za wanaume, naamini timu hii ingekuwa imeshafika katika fainali za Afrika. (Makofi)
Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri na wenzetu wa TFF, Mheshimiwa Kadutu yuko humu ndani, kwamba tujaribu kuweka uwekezaji kwenye timu ya Twiga Stars. Timu hii inaweza ikatutoa kwenye suala la crash program, kwa muda mfupi tunaweza tukaenda mahali fulani na tukafanikiwa. (Makofi)
Suala lingine ni kuhusu Baraza la Sanaa la Taifa. Baraza hili linafanya kazi kama wenzetu wa TFDA kwamba wanasubiri bidhaa ziko sokoni ndiyo wanaenda kukamata wauzaji wa zile bidhaa. Nawaomba wasifanye kazi kwa namna hiyo. Tumeona video ya chura ambayo imekuwa kwa kweli inadhalilisha, nashangaa bado hatujapata matamko kutoka kwa akina mama, lakini video ile haistahili kuangaliwa na Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna tamaduni zetu. Ni vizuri Baraza la Sanaa la Taifa likasimamia wasanii wetu kuhakikisha kazi wanazofanya lazima ziwe zinazingatia maadili na tamaduni zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uandishi na utangazaji; ni kweli kabisa kwamba waandishi wetu wanafanya kazi katika mazingira magumu, wakati mwingine habari hizi wanazozitafuta hasa habari za uchunguzi, zikiwemo za mauaji ya vikongwe, albino pamoja na habari za huko mikoani, nyingi wanazifanya katika mazingira hatarishi. Ni vizuri Wizara ikaja na sera maalum ya kuweza kuwalinda waandishi wa habari ili waweze kupata bima ili wanapokuwa katika kazi zao, waweze kuwa na uhakika wa maisha yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine pia tuhakikishe kwamba kuna chombo cha kupima weledi wa waandishi wa habari, kwa sababu wapo wenzetu waandishi wanageuza baadhi ya watu kuwa bidhaa. Unashangaa gazeti kila siku linaandika habari za mtu mmoja ambazo ni habari za kutunga, wakati mwingine hazina uhakika wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, weledi katika uandishi uzingatiwe, tuepuke uchochezi. Watangazaji nao siku hizi kunakuwa na mipasho mingi kwenye vyombo vyetu vya habari, hawaongei mambo ya msingi, hasa katika vipindi vya taarabu, wanazungumzia mambo ya mitaani ambayo hayana tija sana kwa Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, suala lingine ndugu zangu, nilikuwa naongelea suala zima la deni la Serikali. Serikali imekuwa inakwenda pale TFF na kuingia kwenye akaunti zao na kuchukua pesa. Mwanzo wa mambo yote haya ni katika mechi ile ya Tanzania na Brazil. Mechi ile kwa tunaofahamu ni kwamba iliandaliwa chini ya Serikali ya Awamu ya Nne kupitia Ikulu na zilitolewa takribani shilingi bilioni tatu kwa maandalizi ya mechi ile. Mapato yaliyopatikana kwenye mechi, nadhani ni kama shilingi bilioni 1.8, hizo nyingine hatujui kwamba Mheshimiwa Rais alizitoa wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo TRA walikuwa mara kwa mara wanaingia katika akaunti za TFF na kuchukua pesa. Sasa msingi ni kwamba mechi ile iliandaliwa na Kamati maalum, haikuandaliwa na TFF. TFF walikuwa tu ni waendeshaji wa mpira lakini katika mechi ile hawakuhusika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine katika hilo hilo, ni kwamba kulikuwa na mshahara wa kocha ambaye aliletwa na Serikali ya Awamu ya Nne, Marcio Maximo. Kwanza tunamshukuru sana kocha huyu kwa sababu alileta hamasa kubwa sana katika mpira wa Tanzania, aliifanya TFF ya Rais Leonard Chila Tenga kuwa taasisi ambayo iliheshimika sana na mwamko katika nchi uliongezeka sana. Kocha huyu alikuwa analipwa pia kupitia Serikali. Sasa tunashangaa baada ya muda TRA wanadai kodi ya mapato ya mshahara wa kocha wa TFF. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishauri Serikali kwamba hebu ilifanyie kazi suala hili TFF inajiendesha yenyewe kupitia mapato ya mlangoni, haina ufadhili wa kutosha. Sasa hivi tumeiachia pia jukumu la kuandaa timu ya Taifa ambapo kimsingi wenzetu wa Afrika Magharibi timu hizi zinaandaliwa na Serikali. Bila Serikali kuweka mkono katika timu ya Taifa, tusitarajie miujiza yoyote kama tunaweza tukaenda huko ambako tunatabiri kwenda. Ni lazima Serikali iweke uwekezaji wa kutosha lakini wakati huo huo iwa-support wenzetu wa TFF, wanayo kazi ngumu, zipo timu zaidi ya nne ambazo wanatakiwa kuziandaa, wao peke yao hawatoshi. Hiki kidogo ambacho tunakipata, bado Serikali inaenda inakichukua ilhali suala la mshahara wa kocha lilikuwa limetokana na mshahara ambao Rais aliahidi kwamba atatoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine naomba kwa mara ya kwanza leo nimpongeze Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Mheshimiwa Sugu, amezungumzia suala zima la miziki ya ndani kupigwa kwa asilimia 80. Mimi nasema, isiwe 80, twende hata mpaka 90. Sasa hivi hata hao wasanii wetu wanakuwa wa Marekani zaidi ama wa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, ahsante sana na naunga mkono hoja