Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuweza kunipa nafasi ya kuchangia jioni hii ya leo katika hotuba hii muhimu yenye maslahi mapana kwa Taifa letu na kwa Muungano wetu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Kaka yangu Mheshimiwa Suleiman Jafo kwa kuja Jimboni kwangu na Wilayani kwangu kuja kunitembelea katika Mkoa wa Kaskazini Unguja. Bila shaka Mheshimiwa Waziri uliweza kuona uhalisia wa athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, hususan katika Kijiji cha Nungwi na Matemwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kunako tarehe 26 Julai, 2021, Wizara ya Madini ilikutana na Wizara ya Maji na Nishati ya Zanzibar, kukaa na kujadili baadhi ya mambo. Licha ya kwamba, taasisi hizi mbili siyo za kimuungano, lakini kwa nini zimekaa na kujadili mustakabali wa Watanzania? Sababu kubwa ni kulinda na kudumisha mahusiano yaliyokuwepo baina ya pande mbili hizi za Muungano.

Mheshimiwa Spika, hii inatupa picha ya wazi kwamba, kuna masuala mengine ambayo yana maslahi mapana kwa Watanzania hata kama siyo ya kimuungano yanaweza kujadiliwa kwa maslahi ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hivyo? Mkoa wa Kaskazini Unguja, hususan katika Vijiji vya Pwani Mchangani, Kijini na Jimbo la Nungwi kwa ujumla ni vijiji ambavyo vimetawaliwa na ukame. Ukame ambao unasababishwa na maji ya bahari kuvamia maeneo yale, kitu ambacho wananchi wa kule wamekuwa wanapata shida kubwa katika kuyatafuta maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, jambo lile limesababisha wananchi wa maeneo yale kuathirika kwa sababu ya kimaumbile kwa upande wa maji, vilevile wameathirika kutokana na athari nyingine za mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ione haja ya kukaa na Taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuandaa miradi maalum ya kwenda kunusuru maisha ya wananchi wa maeneo yale. Kwa sababu, suala la mabadiliko ya tabianchi ni suala la kimuungano na suala la mazingira siku zote lina element ya masuala ya kimuungano, wale wananchi kwa kuwa wameathirika na sababu za kimazingira na athari zinzotokana na mabadiliko ya tabianchi hakuna haja ya kusema labda kwa nini yazungumziwe masuala ya maji katika suala ambalo ni la kimuungano? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hali kama hii maji ya maeneo yale yameathirika kutokana na athari ya mabadiliko ya tabianchi. Mwanzoni historia inaonekana wazi kwamba tulikuwa tunapata maji safi na salama mnamo mwaka 2010, nafikiri Wizara ya Muungano na Mazingira ilitupa miradi kwa kuona ule uzito, lakini miradi ile imeshakuwa michache kulinganisha na ongezeko kubwa la wananchi wa maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ziara yako uliyokuja wananchi wanatarajia mambo makubwa mno kutokana na ziara yako, lakini bado wana hamu ya kukuona unarejea tena na tena kwa sababu athari zile mkiendelea kukaa kimya bado zinaendelea kuathiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu cha msisitizo kikubwa Wizara hii ione haja na kila sababu ya kufanya mambo mawili kupitia miradi hii ya kimuungano.

Mheshimiwa Spika, kwanza Zanzibar kuongezewa fungu kwa sababu, athari kubwa ya mabadiliko ya tabianchi licha ya kwamba, huku maeneo ya Ukerewe na maeneo mengine zinapatikana, lakini athari kubwa ya mabadiliko ya tabianchi zinaonekana katika Visiwa vya Unguja na Pemba.

Mheshimiwa Spika, hata kule Pemba kulikuwa na mabonde 18 wananchi wa kule walikuwa wanalima mihogo, mbaazi, kunde, lakini leo hii hatuzungumzii tena maeneo yale yote yameshaliwa na bahari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ndio maana nasisitiza…

(Hapa kuengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji )

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)