Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi na kuwa wa kwanza kwenye kuchangia hotuba ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira. Ofisi ambayo Ndugu yangu Mzee wa Mzenga anaiwakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze yeye na viongozi wote ambao wako Wizarani kwake kwa namna ambavyo wanatekeleza majukumu ya Serikali. Kwa kuwa, muda ni mchache sana naomba akubaliane nami kwamba, nilichokitamka kama pongezi kinatoka ndani ya nafsi ya moyo wangu.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu leo nimeomba nichangie kwenye eneo hili kwa sababu ya kutaka kuzungumza suala moja ambalo nililielewa wakati Mheshimiwa Rais anafanya uapishaji wa Baraza la Mawaziri, alipowaambia Mawaziri na Taasisi za Serikali kwa lengo la kuwahudumia Watanzania ni vizuri wakawa na mawasiliano ili kumaliza kero na changamoto ambazo Watanzania zinawakabili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa jinsi nilivyomuelewa Mheshimiwa Rais na nia yake ilivyo njema ya kutaka vyombo vya Serikali viisaidie nchi hii na hasa kwenye kuondoa changamoto ambazo Watanzania wanazo, nimeona nianzie hapo kwenye kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ambayo ndugu yangu Mzee wa Mzenga, Jirani yangu pale wa Jimbo yupo.

Mheshimiwa Spika, nimeamua nichangie hapa kwa kumkumbusha yeye na vingozi wengine…

SPIKA: Mheshimiwa Mwakamo, huyo Mzee wa Mizenga ndiyo nani?

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ni Mheshimiwa Waziri Jafo. Naomba… (Kicheko)

SPIKA: Basi tunamtambua namna hiyo humu ndani. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Sasa Mheshimiwa Waziri lipo jambo ambalo linaendelea ambalo Mkurugenzi wa NEMC na ninashukuru ametambulishwa yupo, pale Jimboni Kibaha vyombo hivi vimeshindwa kuwasiliana vizuri. TAMISEMI walitenga pesa kwa ajili ya kupeleka pale kuendesha mradi mkubwa wa ujenzi wa shule ya sekondari, pia TAMISEMI walitoa maagizo mbalimbali maeneo ya pale yalipimwa kwa utaratibu wa kisheria, lakini kwa masikito makubwa Wizara au Ofisi ya NEMC imetoa zuio kwa maana eneo lile lisiendelee na ujenzi.

Mheshimiwa Spika, kitu kinachosikitisha wananchi wamepata taharuki kubwa na taharuki hii imesababishwa na wao, kwa sababu hilo eneo lilishapimwa, limepimwa kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi, limepangiwa matumizi mbalimbali, bahati nzuri au mbaya Serikali wameuza viwanja kwenye maeneo hayo na wananchi wamenunua viwanja hivyo kwa shughuli mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vipo viwanda vimeshaanza kujengwa na vibali wanatoa haohao NEMC, lakini kinachosikitisha mwezi uliopita huu wametoa zuio la kutokuendelea na ujenzi wa shule ya sekondari, jambo ambalo limewashtua watu wengi, jambo ambalo limesababisha changamoto kubwa, mpaka hivi ninavyozungumza wale walionunua viwanja kwenye eneo lile wananipigia simu wakiwa wanataka kuweka utaratibu wa kwenda kuishtaki Halmashauri kwa sababu ndio ambao wamewauzia viwanja ambavyo vimezuiwa na NEMC.

Mheshimiwa Spika, sasa ninataka nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba awe makini na hawa NEMC kwa sababu, ni wao ambao wametoa vibali vya ujenzi, lakini hao hao tena waliotoa idhini ya eneo lile kupimwa, hao hao wenyewe ndiyo wanatoa idhini eneo hilo kuzuiwa lisijengwe.

Mheshimiwa Spika, kinachosikitisha sana wanaenda kuzuia miradi ambayo inajengwa ya Serikali lakini ile miradi ambayo watu wanakwenda kuomba vibali kwao wanawapa pasipo mashaka, sasa wanaleta taharuki kwa jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo hilo ambalo wanalizuia tayari kuna jengo la Halmashauri limejengwa pale, limejengwa kwa gharama kubwa ya pesa za Serikali. Sasa sijaelewa zuio hili ni kwa ajili ya sekondari tu au zuio hili na lile jengo la Serikali linavunjwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia sijaelewa, kwa zuio hili walilolitoa na vile viwanda walivyotoa kibali wao wanaenda kuvibomoa? Kama watavibomoa, wale wenye viwanda ambavyo wameviendeleza watawapa fidia ya namna gani?

Mheshimiwa Spika, najua muda ni mchache, lakini ninaamini mengi nitazungumza na Mheshimiwa Waziri pale ambapo nitapata nafasi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)