Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mezani, kwanza nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja hotuba ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ambayo imewasilishwa hapa mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuchangia tu jambo moja ambalo limejitokeza katika michango ya Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na suala la wastaafu. Kwanza wamezungumzia suala la wastaafu kuchelewa kupata malipo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niliambie Bunge lako tukufu kwamba, mifuko yetu imeweza kulipa mafao kwa wastaafu kati ya kipindi cha mwaka 2018 ambapo Mfuko wa PSSF ulianzishwa hadi Machi 2022 tumeweza kulipa mafao yenye thamani ya Shilingi Trilioni Sita na Bilioni Tisini na Moja na kila mwezi Serikali inalipa fedha Shilingi Bilioni 58.75 kwa wastaafu 148,868 kwa mwezi tarehe 25 bila kukosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakiri kwamba kulikuwa na changamoto hasa kwa wastaafu ambao walikuwa wameanza kazi kabla ya mwaka 1999 ambao walikuwa hawachangii lakini wakaingia kwenye mfuko. Kwa hiyo hao walisababisha Mfuko kuelemewa kwa sababu walikuwa hawachangii lakini walikuwa wanatakiwa kulipwa na ndiyo hiyo hela ambayo mdogo wangu Ester Bulaya anaizungumzia ya Shilingi Trilioni 4.62 ambayo ilitokana na watumishi ambao walikuwa hawachangii katika mifuko lakini Serikali iliona na wenyewe wapate mafao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali imetoa fedha Trilioni 2.17 ambayo imewezesha mifuko kupata nguvu na watu wote ambao malimbikizo yao yaliyokuwepo ya mifuko kwa wastaafu wamelipwa na sasa hivi watumishi wanaostaafu wanapata mafao yao ndani ya siku 60 tangu walipoleta taarifa zao za kustaafu yaani tangu tarehe ya kustaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna changamoto inawezekana kuna wachache ambao taarifa kama ambavyo kuna Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia mwingine anakuwa hana barua ya ajira kama nilivyosema, wale ambao walikuwepo kabla ya mwaka 1999 kweli kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshafuatilia kundi hili waliobaki ni wachache na tunaendelea kuweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba hata hao ambao waliingia kwenye mfuko wakati tayari wako kwenye utumishi na taarifa zao hazikuwa zimekuja rasmi, kwa kiasi kikubwa tumeshakamilisha kwa hiyo usumbufu huo hautakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uhakiki wa wastaafu, hili suala la uhakiki wa wastaafu niseme kwamba wastaafu wetu ni watu ambao wameitumikia nchi yetu kwa uadilifu na Serikali inawathamini wafanyakazi wanapokuwa kazini, na hata wanapostaafu Serikali inaendelea kuwathamini. Tayari Serikali imeshatoa maelekezo zoezi hili la wastaafu lisilete usumbufu kwa wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo napenda kuchukua nafasi hii kuwaelekeza PSSSF pamoja na NSSF zoezi la kuhakiki wastaafu lifanyike katika namna ambayo haitawalazimu wazee wetu kusafiri muda mrefu kwenda kwenye Makao Makuu ya Mikoa.

Kwa hiyo, hilo ni suala la usimamizi, tayari Serikali imetoa maelekezo kuhakikisha kwamba uhakiki wa wastaafu unafanyika katika namna ambayo haileti usumbufu kwa wazee wetu, lazima wazee waheshimiwe na lazima wazee walindwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo Waheshimiwa wanalizungumzia ni uhimilivu wa mifuko. Naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba mifuko hii bado ni himilivu bado itaendelea kulipa mafao kwa wastaafu na deni ambalo lilikuwepo la...

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi?

MHE. ESTER A. BULAYA: Hapa

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpe taarifa Mheshimiwa Waziri. Taarifa za Serikali ya Machi 2022 ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali amesema mifuko ina hali mbaya, siyo himilivu na iko kinyume na taratibu wa ukwasi wa asilimia 40, mlipolipa ile pre 99 Trilioni Mbili walau imefika asilimia 30 lakini ….

MWENYEKITI: Taarifa ya Serikali au taarifa ya CAG?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni taarifa ya CAG na ndiyo Serikali yenyewe.

MWENYEKITI: Basi rekebisha vizuri.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupa pia taarifa kwamba PSSSF kwa miaka hii ya karibuni mapato yake ya michango ni madogo kuliko mahitaji ya wazee wastaafu wanaotakiwa kulipwa, iko himilivu wapi?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Prof. Ndalichako unapokea taarifa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Ofisi ya Waziri Mkuu?

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siipokei hiyo taarifa kwa sababu taarifa ya CAG ni ya mpaka Juni, 2021.

(Hapa Mhe. Ester A. Bulaya alizungumza bila kutumia kipaza sauti)

MWENYEKITI: Nani amekuruhusu uzungumze Mheshimiwa Bulaya? Hili ni Bunge endelea Mheshimiwa Profesa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU KAZI AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimeeleza kwamba tayari Serikali imetoa fedha shilingi trilioni mbili na bilioni mia moja sabini kwa ajii ya kulipia fedha za mifuko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali imetoa fedha hizo ni dhahiri kwamba hata hizi ambazo zimebaki kiasi cha shilingi bilioni 2.45 Serikali itazitoa tu Serikali yetu ni sikivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hili ni deni la muda mrefu ambalo tangu mwaka 1999 lakini Serikali imeshalipia trilioni 2.17 na zilizobaki ni suala la muda tu. Kwa hiyo, suala hili litalipwa na wastaafu wataendelea kupata mafao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia, ahsante sana. (Makofi)