Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana Mwenyekiti kwa kunipa nafasi. Mimi nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya lakini hasa kwa kuangalia maslahi ya watumishi na kwa kumteuwa Mheshimiwa Waziri kwenye nafasi ya kuwaangalia watumishi wa nchi hii. Watanzania wana imani naye watumishi wana imani naye na uthibitisho ni jinsi alivyopigiwa makofi hapa ndani wakati anaenda kusoma hotuba yake ya bajeti jana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niwapongeze na wasaidizi wake Naibu Waziri, na watumishi wengine wizarani kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Vilevile tuipongeze sana Serikali yetu kwa kutoa ajira ya watumishi 32,000, hii itapunguza upungufu wa watumishi kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Tabasamu aliongelea kidogo jambo la mazingira magumu ya watumishi kwenye baadhi ya maeneo yetu. Tuna maeneo nchi hii ukimpeleka mtumishi hakuna nyumba hata za kupanga, acha zile ambazo zimejengwa kwa ajili ya watumishi. Ninachoiomba Serikali yangu maeneo kama hayo watumishi hawa wapewe posho ya mazingira magumu ili watumishi waweze kubaki kwenye maeneo hayo ili wawe tofauti na wale ambao wako mijin. Wakipewa fedha kwa kuangalia mazingira magumu wanayoishi watumishi hawa watabaki kwenye mazingira hayo. Kuwe na tofauti kati ya wanaokaa mjini na wale ambao wanaenda kwenye mazingira ambako hata nyumba za kupanga hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye utumishi wa umma kumekuwa na changamoto mtumishi anapoenda kusoma. Kwanza Serikali haisomeshi watumishi wengi kwa sababu ya kibajeti, lakini watumishi hawa wanajilipia ada wenyewe hakisharudi kwenye eneo lake la kazi ile elimu yake aliyopata kutambuliwa kwa wakati inachukuwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wengine utakuta mtu ana nafasi, either Mkuu wa Idara au yawezekana ni Mwalimu Mkuu, akirudi kazini nafasi yake hiyo imeshachukuliwa na mtu mwingine, yeye atakaa benchi na wala hakuna consideration kwamba huyu amesoma. Ile elimu aliyopata badala ya kuhitumia ana kaa miaka mitatu yuko bench au yuko frustrated. Hatutumii watumishi wetu vizuri. Kwahiyo naomba eneo hili tuliangalie vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limeongelewa sana suala la mafunzo kazini. Kumekuwa na utamaduni tu kwamba walioko ngazi za juu kila siku wanatoa maelekezo. Sasa badala ya kuwa tuwe na utaratibu wakutoa tu maelekezo hasa sekta ya elimu tuwe na utaratibu wa kukaa na hao watumishi kufanya mafunzo kazini ya namna ya kuboresha utendaji wao. Si lazima mafunzo hayo yawe ya gharama kubwa lakini yakatengenezwa mfumo wa angalau hata kwenye ngazi ya kata kila mwaka wanakuwa na mafunzo ya namna gani wanaweza wakaboresha utendaji wao wa kazi ili kuwapa motisha watumishi hao, kwamba wao wanafanya kazi lakini tunawaangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu watumishi wetu wanaoelekea kustaaafu. Unakuta mtumishi amepandishwa daraja lakini mshahara wake haanzi kulipwa kwa wakati, ule ambao ni wa daraja husika. Mtumishi huyo anastaafu tofauti ile haijawahi kulipwa, anaanza kudai sasa mafao yake na anakuta mafao hayo yamepunjwa sana. Mtumishi huyo atahangaika atazunguka kote ili kupata haki yake, nah apo inakuwa ni usumbufu mkubwa na sisi Wabunge tunapata changamoto kubwa sana kwenye eneo hilo. Naomba tuangalie na tutengeneze mifumo ambayo inawezesha kujua kwamba mtumishi huyu baada ya muda fulani atastaafu na hivyo taratibu zake zote ziandaliwe ili anapostaafu mishahara yake yote iwe imekuwa sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kumekuwa na changamoto ya kuwalipa mafao yao kwa wakati. Mtu amezoea kupokea mshahara labda tuseme laki tano kwa mwezi, anastaafu halafu anakuta mwezi wa kwanza hamna kitu, wa pili hamna kitu na hata mwezi wa tatu hamna kitu. Tunawatesha watumishi wetu wanaostaafu. Na hata malipo yale ya kila mwezi baada ya kustaafu hayaanzi kwa wakati. Kwa hiyo hili eneo tuliangalie kwa umakini mkubwa kwasababu tunawatesa watumishi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao watumishi ambao wamestaafu siku za nyuma, posho wanazolipwa au mafao yao ni madogo mno na kazi walizofanya ni sawasawa na watumishi ambao wanastaafu siku za hivi karibuni. Tuwaangalie, kwasababu fedha tunazowapa haziwasaidii kitu chochote kwa hali ya maisha iliyopo sasa. Wale wastaafu wetu ambao wamestaafu siku za nyuma tuwaangalie namna ya kuwaboreshea mafao yao ili nao waweze kuishi kama watu waliotumikia nchi yao kwa uhaminifu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kumekuwa na suala hili la uhakiki wa wastaafu. Uhakiki huu utakuwa unafanyika mara nyingi Makoa Makuu ya Mkoa ambako ni mbali. Mtu kwenda kuhakikiwa anaingia gharama kubwa ilhali malipo yenyewe anayolipwa ni kidogo. Kwa namna hii tunawatesa wastaafu wetu, wengine wameshaanza kuwa wazee. Sasa, tuwasaidie kwenye kuwahakiki maeneo karibu na wanakoishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi baada ya kusema hayo niendelee kupongeza, watumishi wa Tanzania wanayo matumaini makubwa, na mimi ninaamini Waziri wakati wa Mei Mosi watumishi watacheka ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)