Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kufunga dimba siku ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote na mimi niungane na Wabunge wenzangu kuishukuru sana Serikali hii ya Awamu ya Sita kwa kazi nzuri inayoendelea kufanya katika nchi yetu. Ninamshukuru sana na nimpongeze Waziri Dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama, amekuja muda mfupi katika Wizara hii lakini sasa hivi amejenga matumaini makubwa kwa watumishi. Watumishi wengi wanayo imani sana, ninamshukuru Naibu wake lakini nimshukuru pia Katibu Mkuu Dkt. Laurine Ndumbaro pamoja na Wasaidizi wake wanafanyakazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuishukuru na kuipongeza Serikali kwa kibali kile cha ajira 32,000. Nina uhakika wamsema wenzangu hapa na hasa wale wa Majimbo ya vijijini na mimi natoka kijijini, hali yetu kule tunaijua watumishi wako pungufu sana, tuna uhaba mkubwa sana wa watumishi. Nitolee mfano tu, iko shule ina Walimu Watatu na miongoni wao mmoja anaondoka, shule hiyo inabaki na Walimu Wawili. Kwa hiyo, nina uhakika sasa kwa kibali hiki cha watumishi 32,000 na mimi shule zangu kule zitapata watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia na zahanati zangu zitapata watumishi, lakini pia na hospitali itapata watumishi, naishukuru sana na ninaipongeza Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Mheshimiwa Kasinge, nchi yetu inaongozwa kwa Katiba na Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa haki kwa Watanzania wote, haki ya kushiriki siasa, kwa maana ya kuchagua na kuchaguliwa, vilevile imetoa haki ya kufanya kazi na imetoa haki ya kuajiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2020 tulikuwa na Uchaguzi Mkuu katika nchi yetu, kuna Watumishi ambao walienda kushiriki kwenye uchaguzi ule, baadhi ya watumishi hawa walikuwa wateule wa Rais, kulikuwa na Wakuu wa Mikoa, kulikuwa na Wakuu wa Wilaya, lakini kulikuwa na watumishi wasiokuwa wanasiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Katiba hii hakuna raia wa Tanzania aliyezuiwa kushiriki siasa hakuna! Wananchi wote wameruhusiwa kwa mujibu wa Katiba hii kushiriki siasa. Kwa bahati mbaya sana mwaka ule wako wananchi raia wa nchi hii baada ya kuingia kwenye siasa walisitishwa haki yao ya kufanya kazi. Utaratibu ule haukubaliki kabisa kwa mujibu wa Katiba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali hii ya Awamu ya Sita ilichukua hatua baada ya kusikia kilimo cha Wabunge wa Bunge hili kwamba utaratibu ule ulikuwa siyo sahihi, watumishi wale wengi kama siyo wote wamerejeshwa kwenye nafasi na sasa wanaendelea na kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uko Waraka wa mwaka 2014 unaosema uko wazi kabisa kwamba, mtumishi wa umma ataondolewa kwenye utumishi atakapoteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwamba yeye ni nani sasa anashiriki uteuzi au uchaguzi wa katika maeneo yake ya siasa. Upo ule waraka umeeleza vizuri sana, lakini lililofanyika mwaka ule limeenda tofauti sana na waraka ule.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu kuchukua fomu tu alisitishiwa ajira, alisitishiwa kufanyakazi, tulikiuka sana Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wale wamerudi, walirudi baada ya kukaa nje ya kazi kwa zaidi ya miezi wengine Saba, wengine Sita, wengine Nane. Mwenzangu amehoji hapa wale watumishi walikuwa likizo ipi? Kwa sababu bado wana haki zao, kushiriki siasa hakumuondolei mtu haki ya kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami naungana na mwenzangu Serikali kwa vile tayari tumewarudisha wale watumishi kazini, tunafahamu miezi kadhaa walikuwa hatuelewi kama walikuwa likizo au ilikuwa ni kitu gani lakini miezi kadhaa wana madai yao, kwa hiyo ningeomba maelezo yatolewe hapa na Serikali ule muda ulikuwa ni kitu gani. Nadhani kwa sababu Serikali hii sikivu na Mheshimiwa Jenista wewe ni msikivu utakuwa na majibu mazuri yanayoenda kuwatia moyo wale watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ni suala la hii recategorization. Recategorization ni kitu kizuri sana kina manufaa pande zote. Kina manufaa kwa mtumishi lakini kina manufaa pia kwa upande wa Serikali. Imekuwa hivyo vizuri inafanyika lakini kwa bahati mbaya sana kuna baadhi ya Taasisi inapofanyika hii recategorization ina wanyanyasa au inawaonea watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtumishi ameenda kusoma, mtumishi yuko kwenye nafasi fulani mahala Fulani, Taasisi inaona upungufu wa Idara Fulani, inamtoa mtumishi kutoka Idara aliyokuwa anafanyia kazi, anarudi kufanyakazi hapa kuimarisha ile Idara lakini mwisho wa siku anapunguzwa mshahara anakuja kuanza as if anaanza leo ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili siyo sahihi sijui, lakini ikibidi kama kweli mtumishi yule ameomba mwenyewe sawa, lakini sasa Idara au Taasisi inamhamisha kutoka Idara fulani inamrudisha hapa ili aendane na muundo wanamuondolea mshahara aanze tena upya! Ningependa Serikali itoe tamko hapa watumishi ambao Idara au Taasisi ndiyo iliyohitaji abadilishwe mfumo basi wale wasianze upya wasianze katika level ile ya kwamba anaanza ajira, wahame na mishahara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Waziri atakapokuja kusema hapa na mimi nitashika shilingi kama hiyo kauli sitaisikia. Kuna orodha ya watumishi wako hapa, wameondoka kwenye Idara fulani wamepelekwa kwenye Idara fulani wakaenda wakawashushia mishahara yao. Leo hii yule mtumishi alikuwa na mkopo, ana mkopo wa Loan Board anaenda kufanyakazi anarudi hana kitu kabisa! Si ndiyo tunafundisha watu kuiba hapa, tunafundisha watu ufisadi si ndiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali tuliangalie hili, suala hili la recategorization ni zuri mno likifanyika na mtu akahama na kamshahara kake hivi nani anaumia? Hakuna kitu cha kuumia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona niseme hili na nalisema kwa uchungu sana kwa sababu lina maumivu mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine ni ile ya uhakiki wa wale watumishi Darasa la Saba na hii naomba niliseme kwa upole. Ninatambua tuliwaondoa baadhi ya watumishi kwenye ajira, lakini ukienda kuwasikiliza baadhi ya watumishi hao sababu inayoonekana kwamba wali-forge vyeti, baadhi ya watumishi hawa ni Walinzi, anakuambia kabisa mimi sikuwahi sign hicho kitu, mimi nimekikuta tu kwenye file yangu mimi sihusiki, ninaorodha ya watumishi 12 wana malalamiko hayo kwamba wao kama wao na ukiangalia zile documents zao unaona kabisa miandiko iko tofauti, sasa ni nani alibadilisha taarifa zile?

Ninaomba Serikali kwa unyenyekevu mkubwa na kwa sababu Rais wetu anasimamia haki na mara kadhaa amesema yeye ni mpenda haki, ningeomba sana kwa unyenyekevu mkubwa, tufanye uhakiki wa watumishi hawa, ikithibitika siyo basi warejeshwe kazini, yapo malalamiko ya wazi kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.(Makofi)