Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Aloyce Andrew Kwezi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kaliua

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami naomba niwe ni miongoni mwa wale watu ambao wanatoa pongezi kwa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Jenista Mhagama, nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri Ndugu yangu Deo na nisisahau timu nzima inayoongozwa na Katibu Mkuu wa Utumishi Dkt. Ndumbaro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kuchangia lakini nianze kuwasilisha kero ambazo wananchi na watumishi wa Jimbo la Kaliua wamenituma. Awali ya yote wamenituma nianze kwa kuwashukuru sana Wizara hii ya Utumishi kwa kuanza kulipa malimbikizo ya mishahara kwa kiwango kikubwa sana. Tunawashukuru sana kwa kweli kwa mwezi Februari peke yake watumishi wa Jimbo la Kaliua mmelipa milioni 400. Pia mmelipa baadhi ya fedha ya uhamisho, nilikuwa napenda nikumbushe hapo Serikali yangu sikivu kwamba Halmashauri ya Kaliua pesa ambazo tunadai arrears pamoja na madai mengine ya utumishi yanafika shilingi bilioni 1.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba tuangalie jinsi gani tunavyokwenda tulipe awamu kwa awamu ili wale watumishi wawe na mazingira mazuri sana ya kufanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nakuja na ushauri na ushauri wangu nataka kidogo tuelewane sehemu moja na kwenda ku-challenge sehemu ya harmony. Ninawashauri wa- harmonize scheme kwa maana ya kwamba tofauti ya mishahara kati ya Serikali Kuu, Serikali za Mitaa pamoja na Taasisi za Serikali. Mishahara ya Taasisi imekuwa ni mikubwa sana tofauti kabisa na mishahara ya watumishi wa Serikali Kuu au watumishi wa Serikali za Mitaa, sasa Wizara ambayo inaandaa hii Scheme of Service ni hii moja, hivi inakuwaje Afisa Utumishi au Mchumi aliyeko kwenye Halmashauri wanahudumia karibu watumishi 3000, 4,000 na huku wamesoma pengine miaka mitatu Degree yao, wanafanya kazi vizuri, inakuwaje mtu wa kwenye taasisi ambaye anasimamia watumishi 100 hawa wa Serikali Kuu na Halmashauri wanalipwa mshahara wanaanzia kima cha chini cha 750,000 wale graduate, lakini wale wa taasisi kule wanakwenda kuanzia 2,000,000 na kidogo huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashauri hapa hebu fanyeni job evaluation, ukubwa wa majukumu, yaani mimi niongoze watumishi 100, nilipwe mshahara mara mbili ya huyu ambaye anaanza, tulisoma UDSM pamoja au Mzumbe au whatever na ninafanyakazi vizuri na pengine mimi niko kwenye mazingira magumu zaidi. Hiki kitu nawashauri mkiangalie kwa kina kwa sababu madhara yake ni makubwa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wengi kutoka Local Government Halmashauri zetu wanakimbia kwenda kwenye Taasisi wakifuata keki nzuri. Hili jambo lazima tuwaambie vizuri kwa sababu tusipowashauri sisi tunakosea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kasinge alichangia vizuri pale nimemwelewa sana, alikuwa anagomba hii miundo kwa sababu huyo ni Afisa Utumishi zaidi ya miaka kumi, sasa haya tunayowaambia ndiyo ambayo tunayaona tunayaishi. Kwa hiyo, tunaomba mliangalie jambo hili hii tofauti ya mishahara imekuwa ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nilikuwa najiuliza hivi sasa hivi tunapoajiri tumeacha kufuata muundo wa utumishi wa umma? Kama tunafuata muundo wa utumishi wa umma nilikuwa najiuliza juzi juzi, mimi najua mtendaji wa kata kwa mfano anapoajiriwa utakuta pengine awe na Diploma au Shahada ya Maendeleo ya Jamii ya Fedha, Usimamizi wa Fedha, Utumishi, Mipango na mambo mengine. Lakini sasa hivi hapa katikati unachukua mtu ambaye kamaliza Education unamuweka Mtendaji wa Kata, Sekondari zetu huku ziko wazi hivi huu muundo! Nawaambia hili la wazi ndugu zangu sitaki kuwaficha, muundo tunaosimamia hapa nadhani mmeuboresha ni wa 2002 maboresho yakafanyika 2013 kwa wale WEOs hawa Watendaji wa Kata na Vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi nilikuwa nashauri hivi tutawapandishaje vyeo hawa maana yake akitoka WEO II anategemea kwenda WEO I, au kwenda Senior or whatever huko mbele, sasa anapokwenda lazima kuna sifa zinakuwepo pale, hiki kitu ni nini? Nadhani hatu-utilize resources vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashauri muangalie mapema ili huko mbele tusije tukawekeana kelele zisizokuwa na sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nalishauri linahusiana na uhamisho. Utumishi wanapozunguka kwenye maeneo ya kwetu wanatuambia kwamba Mkurugenzi, Afisa Utumishi sijui taasisi gani, pitisha ila shauri kwamba lina upungufu wa hivi na hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta watumishi wanapoleta zile barua Mkurugenzi anapitisha anashauri kwamba nashauri hapa watumishi ni wachache, wakifika huku mna-authorize wanaondoka, sasa wanaondoka kwa wimbi kubwa matokeo yake Mjini ni wengi, Halmashauri zetu ziko hoi! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaambia hili jambo ni la kweli. Muundo kwa mfano, Maendeleo ya Jamii kwenye Wilaya Ikama inataka pale Makao Makuu wawepo angalau wanne au watano. Jimbo la Kaliua Kata hata moja sina Maendeleo ya Jamii hata Mmoja, hawa wananchi wanaelimishwaje hebu niambieni? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kaliua ina Kata 28, hakuna Afisa Maendeleo ya Jamii kwenye Kata hata mmoja! Hii mikopo tunawafanyaje? Ni nani anahamasisha shughuli za maendeleo? Waje kwenye kamati hizi huku za LAAC sijui USEMI sijui wapi tunawabana, ooh! sijui nini, lakini Ikama huku kwa nini hatuifuati vizuri, kwa nini hatujaajiri vizuri huko?

Mheshimiwa Naibu Spika, ajira nyingi Mheshimiwa Waziri zimekuwa zinakuja sasa hivi ni karibu mimi nasema ni ajira mbadala (replacement), ndiyo zimetoka nyingi lakini zile ajira zenyewe kwa mujibu wa Ikama mimi nina watumishi labda 2,000 lakini mahitaji yangu ni watumishi 4,000, hawa watumishi fuateni kutoka kwenye source kule, sisi ndiyo tunapata shida kule kwamba ukizunguka hapa Mganga Mkuu yuko wapi, ukizunguka hapa Mhudumu hamna, ukizunguka zahanati fulani ameenda kujifungua, miezi mitatu wananchi wa Kaliua wanahudumiwa na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa kulishauri na naliona ni la msingi sana mimi nilikuwa naomba mafunzo, hebu tufanye mafunzo kwa watumishi hasa wale waajiriwa wa mara ya kwanza. Nafasi zenu zile za uteuzi unamteua Mkurugenzi hajui hata mail box hajui kwamba inatakiwa itoke siku hiyo, anaanza kujifunza folio ni nini, anaanza kufanya hiviā€¦

(Hapa Mhe. Aloyce A. Kwelizi alionesha mfano)

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ni vitu gani? Hebu tuweke watu ambao ama wapelekeni mafunzo jamani kama zamani, wiki mbili, wiki tatu, akitoka kule anajua kwamba huyu Mkuu wa Wiaya ni mkubwa kwangu, huyu ni mdogo wangu, chain of command ikoje, haya ya shuleni ya moja kwa moja, haya yanakuja kufanya huku anaonekana anapwaya sasa, kwa sababu wale Wakuu wa Idara walioko pale wako imara kuliko Mkurugenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mmoja nawapa mfano wa kweli mimi sitaki kuwadanganya, kuna mmoja alipoambiwa yeye Mkurugenzi ni mamlaka ya uteuzi alichokifanya, kwanza akawaandikia Wakuu wa Idara wote anawatengua Vyeo! si mamlaka ya uteuzi? Kumbe amesahau mamlaka ya uteuzi lazima a-consider Madiwani huko, alipopiga simu nikamwambia futa hizo barua haraka Mzee unatuaibisha, sijui mnanielewa? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hayo mambo mngekuwa mnawapa kozi haya yangetokea haya? Wanaingia mle wanafikiri wenyewe pengine ni wakubwa hata kuliko Mwenyekiti wa Halmashauri, wakubwa kuliko DC lakini hawajui kwamba hii ni chain leo wa juu anaongea na wa chini vizuri, wa chini anaongea na hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kulishauri jambo moja kubwa sana, pale kwenye ule mlundikano wa vyeo, sasa hivi wanafurahi Watumishi wamepanda vyeo sana ni kweli, lakini ule mlundikano ambao umetokea sasa iko hivi, yaani Mtumishi ambaye alikuwa amepanda mara ya mwisho 2013 anakuja kupanda 2017 au 2018 anakutana na yule junior ambaye amekuja amemfundisha kazi kakaa naye na nini, sasa hivi wote wako kwenye class moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashauri muangalie kama possible mnaweza mkarudi kwenye ule mfumo wa zamani kurekebisha hili tatizo kwa kutumia accelerated promotion kwamba, wewe hapa kwa kweli hata unajua na ingine ni aibu.

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)