Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa juhudi ya kazi ambayo anaendelea kuifanya, na kubwa zaidi kwa kutuletea dada yetu mahiri katika Wizara hii ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora; akisaidiana na mdogo wangu Mheshimiwa Ndejembi, ambaye ninamfahamu kikazi yuko vizuri na kwa maana hiyo, Wizara hii imepata watu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza kuchangia nikumbushe waliopewa dhamana ya Wizara hii ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora; kwamba, ofisi hii ni ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kwa kingereza Public Service Management. Kwa Kiswahili fasaha kabisa hii management ni usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa masikitiko sana niseme kwamba, maeneo yafuatayo yanaharibu taswira ya ofisi hii au ya Wizara hii ya eneo lake la usimamizi, badala yake inaonekana kana kwamba, ni Wizara ya kuleta shida kwa watumishi wa umma. Nikianza nae neo la wanaopata nafasi za uteuzi wa Rais, maafisa wakuu ndani ya Serikali na maafisa waandamizi ndani ya Serikali; wanatekeleza majukumu yao mpaka pale mamlaka ya uteuzi inaposema basi, wakapumzishwa kwenye majukumu hayo, ofisi hii imeendelea kuwatelekeza kwa muda usiojulikana. Huu ni msiba mkubwa na inasikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais Kikatiba ana mamlaka ya kufanya uteuzi maeneo mbalimbali katika idara na taasisi mbalimbali ikiwemo kwenye majeshi, lakini ikiwemo hata humu Bungeni anateuwa humu Bungeni. Na pale ambapo uteuzi wa Rais unapokoma taasisi husika inawarudisha kwenye majukumu yao mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kama ingekuwa Waheshimiwa Wabunge wanaopata bahati ya kuteuliwa na Rais kuwa Mawaziri au Manaibu Waziri na pale ambapo utumishi wao wa uwaziri au unaibu Waziri unakoma ikaonekana kwamba, na Ubunge wao umekoma hapo ingekuwa msiba mkubwa, lakini kwa utumishi wa umma imekuwa ni kinyume chake. Utumishi wao wa uteuzi unapokoma wamebaki wakitelekezwa kwa muda usiojulikana. Nalizungumza hili kwa masikitiko makubwa na ionekane sasa kupitia Bunge hili mabadiliko na marekebisho na maboresho yafanyike katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alipofanya mabadiliko katika kada za wakurugenzi, watendaji wa Halmashauri, makatibu tawala wa wilaya kwa maana ya ma- DAS, pamoja na wakuu wa wilaya, wateule hawa walioachwa kwenye majukumu yao wapo ambao wamekaa bila majukumu yoyote kwa miezi mitatu, wengine miezi mitano, wengine miezi nane, wengine miezi tisa. Sasa kiutumishi huku kupumzishwa kwao kwa miezi mitatu, minne, mitano, mpaka tis ani nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kanuni za utumishi wa umma za mwaka 2003, kanuni ya 96 na ya 97, likizo inatajwa kama vile likizo ya mwaka, likizo ya uzazi, sabbatical leave na likizo nyinginezo. Sasa hawa waliokaa miezi tisa nje ya majukumu walikuwa kwenye likizo gani, watwambie?

Mheshimiwa Naibu Spika, na katika eneo hili nipongeze Mheshimiwa Dada yangu Mheshimiwa Jenista alivyoingia tu kwenye ofisi ameanza kushughulikia tatizo hili. Na ninayo amani kupata taarifa kwamba, watumishi wote sasa hivi wamerudi kwenye majukumu yao ikiwemo wakurugenzi, ma-DAS, pamoja na wakuu wa wilaya, lakini itakapofika wakati wa kupitisha mafungu hapa nitamuhitaji Mheshimiwa Waziri aje atoe maelezo hawa watumishi walikuwa kwenye likizo ipi na stahili zao ni zipi kwa muda wote ambao walikuwa nje ya utumishi wa umma? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo linaharibu taswira ya Wizara hii ni kucheleweshwa kwa mafao ya wastaafu pamoja na kucheleweshwa kwa kulipwa stahiki za wastaafu, gharama za kufungasha mizigo kwenda makwao. Vilevile wapo watumishi ambao wanastaafu kinyume na madaraja ambayo wanatakiwa wastaafie na kwa maana hiyo, wanakuwa wanaidai Serikali mapunjo. Mbaya zaidi unalipwa kwa mshahara wa nyuma kuliko ule ambao walitakiwa staafie. (Makofi).

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati nachangia bajeti mwaka jana nilieleza kilio cha walimu wangu wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, nilitaja wachache kwa uwakilishi wa wengine, na ninarudia tena kuwataja. Walimu haw ani pamoja na Hadija Nasoro Bungurumo, Salima Khamis Kaisi, Omari Ahamadi Mcheluya. Watumishi hawa wamestaafu tangu mwaka 2020 bado pamoja na kuwasemea hapa hawajalipwa mafao yao ya kufungasha mizigo, hawajalipwa tofauti zao za mshahara, kwa maana ya mapunjo ya malimbikizo au arrears.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi ni Serikali Sikivu ni Serikali makini. Inakuwaje wanyonge hawa tunawasemea hapa Bungeni halafu Serikali haichukui hatua? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, matarajio yangu hii itakuwa ni mara ya mwisho ya kuwasmea watumishi hawa. Kwa umahiri wako Mheshimiwa Waziri uliyepewa dhamana…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nilitaka nimpe Taarifa mzungumzaji kwamba, sio wastaafu tu ndio hawapewi fedha za kufungasha na kwenda, bali hata ambao bado wanaendelea na kazi wanaohamishwa kituo kimoja kwenda kingine hawalipwi, wanaweza wakahamishwa hata vituo vitatu bila kulipwa mpaka wanastaafu hawajalipwa hizo hela ambazo walikuwa wanahamishwa wakati wakiendelea kufanya kazi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ally, Taarifa unaipokea?

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeipokea. Na ni maeneo ya kurekebisha katika Ofisi hii ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala lingine ni kuchelewa kufanyika kwa maamuzi kwa watumishi wenye mashauri ya kinidhamu. Ukiangalia sheria na kanuni za utumishi wa umma, ndani ya miezi mitatu inatakiwa mashauri ya kinidhamu yawe yamehitimishwa, mtumishi awe amejua kwamba, anayo hatia na kwa maana hiyo atatumikia adhabu yake au hana hatia, atarudishwa kwenye majukumu yake. Lakini kwa masikitiko makubwa niseme tu kwamba, wapo baadhi ya watumishi wamekaa zaidi ya mwaka mashauri yao ya kinidhamu hayajaamuliwa. Sasa hii ni kinyume kabisa na sheria ambazo tunazitunga hapahapa Bungeni na Serikali ina jukumu la kuzisimamia sheria hizi. Kama tunazitunga na Serikali ndio msimamizi tunatagemea nani akazisimamie? Nani atatoa haki kama si Serikali ambayo ndio inaleta miswada ya kurekebisha au kutunga sheria hapa Bungeni? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe taarifa tu kwamba, kuna walimu 48 Tanzania Bara waliombewa kibali cha kurudi kazini tangu mwezi Juni, 2021. Narudia, walimu 48 wameombewa kibali cha kurudi kazini baada ya mashauri yao kuwa yamehitimishwa tangu mwezi Juni mwaka 2021 lakini mpaka leo mashauri haya yako kwenye ofisi hii ambayo bajeti yake tunaendelea kuijadili. Niombe, mtakapochukua hatua za kuwarudisha kazini watumishi hawa kwa upungufu mkubwa wa watumishi, hasa kada ya walimu tulionao, hawa waleteni Kilwa, mimi nitawapokea. Narudia, waleteni Kilwa tukawapangie majukumu tuna upungufu mkubwa wa walimu kule wakatumikie Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho ni kuhusu motisha kwa kada ya walimu. Walimu, hebu tuangalie ugumu na uzito wa majukumu yao; katika hali ya kawaida inaonekana kama walimu kazi yao kubwa ni kufundisha tu, lakini hapana, walimu hawa kwanza ni walezi wa watoto wetu. Hata pale ambapo watoto wameshindikana kule kwa walimu watoto wananyooshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni nani hajapitia mikononi mwa walimu katika Bunge hili? Hakuna; lakini walimu hawa tumewakumbuka kwa utaratibu gani katika motisha?

Mheshimiwa Naibu Spika, kada zingine wana allowance kulingana na majukumu na uzito wa kazi zao kama vile responsibility allowance, on call allowance pamoja na rational allowance. Sasa hawa walimu ambao wanatumia muda wa ziada kuandaa masomo, kuandaa scheme of service ya muhula mzima au mwaka mzima na shughuli hizi wanazifanya nyumbani. Kama ni mama anaacha baba amelala yeye anaandaa scheme of work, kama ni baba anaacha mama amelala yeye anaandaa scheme of work. Tunachukua hatua gani za kufikiria kuwapa motisha hawa walimu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna kuandaa lesson plan, nje kabisa ya ufundishaji wenyewe. Baada ya hapo unaandaa lesson notice, baada ya hapo unaanza kumfuatilia mwanafunzi mmoja baada ya mwingine. Hebu tufike mahali tupime majukumu mazito ya kazi ya walimu wetu hawa ambao kwa uzalendo mkubwa wanaitumikia nchi yetu na ndio zao la sisi sote na kwa maana hiyo, tuwakumbuke katika motisha. Kama madaktari na sekta ya afya wanapata on call allowance wanapofanya kazi ya ziada…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Ahsante. (Makofi)

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa muda. Na ninaunga mkono hoja. (Makofi)