Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kuipongeza Wizara kwa hotuba yao nzuri na kwa kazi nzuri wanazozifanya pamoja na ushirikiano wanaotupatia sisi Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na wenzangu kuishukuru Serikali kwa namna inavyotekeleza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi. Katika mwaka huu wa fedha ajira 44,000 zinaendelea kutekelezwa, na tayari ajira 11,000 zimeshatolewa lakini pia watumishi 92, 619 watapandisha vyeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nilikuwa nashauri kipaumbele kiangaliwe kwenye halmashauri zenye upungufu mkubwa wa watumishi ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Meatu ambayo upungufu wake upo juu sana kwa asilimia ikilinganishwa na upungufu wa kitaifa.

Mheshimiwa Spika, katika miaka mitano Halmashauri ya Meatu imekumbwa na uhaba mkubwa wa watumishi kwa sababu watumishi wengi wamekuwa wakihama. Ndani ya miaka mitano walimu 232 walihama huku halmashauri tukipokea walimu 39 tu. Vilevile waliokoma utumishi ikiwemo kustaafu ni walimu 156. Shule za Msingi Halmashauri ya Wilaya ya Meatu tuna upungufu wa walimu 930 sawa na upungufu wa asilimia 47 huku sekondari tukiwa na upungufu wa walimu 199 sawa na asilimia 42. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nishukuru kwa tangazo la Wizara ya Afya lililotolewa na Professor Abel Makubi kwamba angalau watumishi waweze kudumu kwa miaka mitatu kabla hawajaanza kuomba kwenda katika halmashauri nyingine kwa kuwa sisi halmashauri za pembezoni tumekuwa tukiathirika kabisa; na watumishi wanaporipoti na kuomba uhamisho. Kwa hiyo sisi halmashauri tunakuwa daraja la kupitia watumishi katika kupata ajira.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa afya Halmashauri ya Wilaya ya Meatu tuna upungufu wa watumishi 675 sawa na upungufu wa asilimia 68. Hospitali ya Wilaya ya Meatu peke yake tuna upungufu wa watumishi 201 sawa na upungufu wa asilimia 64 huku zahanati zaidi ya nane zikiwa na mtumishi mmoja mmoja. Mtumishi akihama, akistaafu au akijifungua ile zahanati inafungwa.

Mheshimiwa Spika, tuiangalie kwa jicho la huruma Wilaya ya Meatu ambapo kama nilivyotaja zahanati nane zina mtumishi mmoja mmoja. Hospitali ya Wilaya ya Meatu zaidi ya miaka sita hatuna mtalaamu wa mionzi, (X-RAY) kiasi kwamba inawalazimu wananchi kusafiri kwenda Shinyanga, Mwanza, na Bariadi. Hii inasababisha wananchi hao wanapata gharama na wengine kupata ajali wanapoelekea kwenda kupata kipimo cha X-RAY.

Mheshimiwa Spika, pia Wilaya ya Meatu hatuna Mhandisi wa Vifaa Tiba na hivyo kuisababisha halmashauri kuingia gharama kubwa kwa kuwaleta watalaamu kutengeneza vifaa hivyo. Mathalani kiliharibika kifaa cha kutoa dawa ya uzingizi, kiligharimu shilingi milioni nne kumleta fundi kuja kukitengeneza kifaa hicho. Kwa hiyo kama halmashauri tunaingia gharama kubwa na kutokutekeleza majukumu ya kutibu kwa sababu ya kukosa watalaamu hao. Kwenye ajira nimeona wahandisi wapo naomba Halmashauri ya Meatu tupatiwe mtaalamu mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali katika mfumo wake mpya wa taarifa za utumishi na mishahara. Mifumo hii inatengenezwa na Watanzania wenzetu na wazalendo wenzetu. Mfumo huu ukitumiwa vizuri utasaidia kupunguza tatizo la watumishi hewa kwa sababu mtumishi akistaafu ataondolewa moja kwa moja na mfumo.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Waziri kuna changamoto ya mawasiliano kati ya Wizara ya Utumishi na Wizara ya Fedha. Mfumo wa Lawson unaonesha wage bill ipo chini lakini fedha inayotolewa hazina ipo juu ukilinganisha na wage bill. Kwa mfano; katika ripoti ya CAG iliyopita Halmashauri ya Wilaya ya Uyui ilipelekewa zaidi ya shilingi milioni 309 katika mishahara kutoka hazina zaidi ya Lawson, Kaliua milioni 209.9, Urambo milioni 149. Ni ukweli usiopingika, sababu ya msingi inayosababishwa hivi ni kufuta majina ya watumishi waliokoma utumishi ambapo tunachelewa kupeleka taarifa hazina. Udhaifu huu usipodhibitiwa utaibua upya mishahara hewa Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kwamba mwaka 2016 Serikali ilipoanzisha zoezi la kutafuta watumishi hewa kuna watumishi waliokuwa wamepata barua za kupandishwa madaraja ya mishahara yao na asilimia ndogo waliweza kubadilishiwa; lakini kundi kubwa lilisitishwa kusubiri zoezi la kusafisha watumishi. Kundi hili lilikaa hadi mwaka 2017 na wengine mwaka 2018 ambapo walipewa barua mpya zikafutwa zile za zamani; kwa hiyo wamechelewa miaka miwili wakilinganishwa na wale wenzao waliopandishwa mwaka 2016. Waliopandishwa mwaka 2016 walipandishwa tena mwaka 2021 ilhali lile kundi la pili limeendelea kubaki hivyo hivyo na kusababisha manung’uniko kutoka kwa watumishi kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali sasa, kwamba, kwakuwa hawa watumishi hawakuwa na makosa isipokuwa lilikuwa ni zoezi zuri; watakapokuja kupandishwa wale wa 2021 wawachukue na wale wengine lile kundi lingine ili waweze kuwa-balance, maana yake athari yake itakuwa pia katika kiwango cha mshahara ambacho wanatakiwa kustaafu nacho.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili lilisababisha pia wengine waliostaafu wasiweze kurekebishiwa mishahara yao. Kuna wengine walirekebishiwa mishahara yao lakini hawakuweza kulipwa mapunjo yao na hivyo kusababisha mafao yao kupigiwa hesabu kwa mishahara ya zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niiombe Serikali yetu Sikivu, Wizara ya Fedha itoe mapunjo ya mishahara kwa waliostaafu. Tunafahamu sasa hivi hawana faili kwa Mkurugenzi na pia hawana faili popote; ni wao wenyewe kutafuta wabunge wao ili waweze kuwasaidia. Serikali iangalie kwa pamoja na iwalipe mapunjo yao ili yawekwe katika mafao na hivyo stahiki ya mafao yao wanayotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)