Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami kutoa mchango wangu mdogo kwenye Wizara hii ya Utumishi ili nami mawazo yangu yachukuliwe.

Mheshimiwa Spika, moja, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunisimamisha kwa siku ya leo. Pili, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anatuangaikia Watanzania ili kuleta maendeleo ya nchi yetu. Pamoja na shukrani hizo, nitachangia katika sehemu tatu. Sehemu ya kwanza ni suala la menejimenti kwa maana ya TAKUKURU, sehemu ya pili itakuwa ni TASAF, ya mwisho nitaungana na wenzangu kuomba suala la ajira.

Mheshimiwa Spika, utendaji wa TAKUKURU na ripoti yake sina mashaka nayo, lakini utendaji wake unakutana na vikwazo ambavyo tusipoviangalia kwa fedha nyingi zilizokwenda vijijini, usimamizi wake ni mdogo, kiasi kwamba ubadhirifu unaendelea kuwepo katika Halmashauri zetu katika nyanja mbili. Moja, TAKUKURU hawana watumishi wa kutosha katika maeneo yetu, ukizingatia maeneo yalivyokuwa makubwa, kunakuwa na watumishi watatu mpaka wanne. Kama ilivyo Tunduru na vijiji vyake, TAKUKURU wanashinda kutembelea miradi yote ya maendeleo ili kufuatilia kama utaratibu wa manunuzi na force account unatumika kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na tatizo la watumishi, hawana magari. Huwezi kutembea zaidi ya kilometa 18,776 kufuatilia miradi ambayo inatekelezwa na Halmashauri kama magari hakuna. Kwa kweli jambo hili linafifisha jitihada za kujenga uchumi kwa maana ya miradi kutekelezwa kwa kiwango kinachotakiwa. Force account ina utaratibu wake, lakini wajumbe wengi kutoka vijijini hawaelewi. Inatakiwa procedure zile zifuatiliwe, zisipofuatiliwa, tunaweka nyanja kwa upande wa watumishi wa Halmashauri kufanya yale wanayoyataka, matokeo yake wale Wajumbe wanachofanya hakieleweki. Kama TAKUKURU watakuwa wanapitia miradi hii, hayo mambo mengine yatashindwa kufanyika kwa urahisi zaidi kwa sababu watakuwa wanaogopa muda wote watu wa TAKUKURU watakuja kuangalia utaratibu wa manunuzi unaendaje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali, pamoja na kazi nzuri wanayoifanya lakini bado kazi hii inatakiwa ifanywe kwa hali ya juu ili malalamiko yaliyoko vijijini yaweze kupungua na miradi yetu iende kwa kiwango kile ambacho kinatakiwa. Katika usimamizi wa miradi hii kwa upande mwingine maeneo yetu, malalamiko ya wananchi ni mengi, TAKUKURU wanakaa ofisini, hawatembei maeneo ya vijijini wakajue hizi changamoto kutokana na tatizo la magari na uchache wa wafanyakazi. Kwa hiyo, naomba ufuatiliaji ukamilike kwa maana ya kuongeza watumishi TAKUKURU pamoja na magari ili waweze kusimamia miradi ya maendeleo vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilipenda nizungumzie ni suala la TASAF. Kwanza tumshukuru Rais kuendelea kuwasaidia wananchi wetu masikini, lakini mwaka huu utaratibu umebadilika kidogo ambao unaleta malalamiko na hauna tija kwa wanufaika wa TASAF. Tumesema hawa uwezo wao ni mdogo, most of them wanakuwa wanapata mlo mmoja au hakuna kabisa. Tunawaambia watalipwa kutumia simu. Kama ameshindwa kula kwa siku mara tatu, atakuwa na simu ya kupokelea hiyo pesa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jambo hili limekuwa ni changamoto sana. Naomba ule utaratibu wa kupeleka fedha moja kwa moja kwa walengwa kwa kutumia magari, basi uendelee, kwa sababu gharama yake ni ndogo kuliko kumwambia alete akaunti namba. Matokea yake analeta akaunti namba ya jirani yake; wakati wanaposti, jina linatofautiana ile pesa inakuwa haiendi. Jambo hili kwa kweli limekuwa ni kero kwa wanufaika wengi, hela zao zinachelewa kwa sababu ya kuambiwa apeleke akaunti namba.

Mheshimiwa Spika, pamoja na akaunti namba, mmeanzisha utaratibu wa kulipa benki. Benki hiyo kwa shilingi 27,000/= au shilingi 40,000/= unamtumia benki, mtu anakaa zaidi ya kilometa 100, anachukuwa nauli kwenda na kurudi shilingi 15,000/= mpaka shilingi 30,000/= anafuata shilingi 40,000/=, tunawasaidia au tunawatesa?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Wizara iangalie suala la malipo ya TASAF kupitia simu yasitishwe na suala la kupitia benki halina manufaa kwa wanufaika kwa sababu hata benki yenyewe ina makato ambayo inayolazimisha yule mnufaika naye mapato yake yaweze kupungua. Nadhani gharama ya benki ni kubwa zaidi kuliko kuwatuma watu kupeleka cash na risk yote iliyokuwepo, lakini ni nafuu zaidi kuliko kutumia benki na simu.

Mheshimiwa Spika, bado tunatakiwa tutoe elimu kwa hao wanufaika wa TASAF, wale wanaofanya kazi za kujitolea. Kama sio mnufaika, anapewa shilingi 24,000/=. Akienda kufanya kazi, kama kazini analipwa shilingi 12,000/=, siku anapokea huku, anapata shilingi 12,000/= na mwenzake anapopokea shilingi 24,000/= anapewa shilingi 12,000/=. Hii inaleta malalamiko. Kwa hiyo, naomba waendelee kutoa elimu kwa maeneo yote, kwamba anayefanya kazi tofauti ya thamani, atalipwa kutokana na ile kama wanavyofanya wenzake ili kuhakikisha kwamba watu wanaendelea.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, kwenye TASAF, sifa kwa kweli imekuwa ni changamoto kubwa sana. Bado kuna malalamiko, wenye sifa wengi wameachwa katika wanufaika hawa. Kwa hiyo, naomba hizi sifa mzingatie kwa hali ya juu kwa sababu sifa hizi ni umasikini, lakini walio wengi ukienda kwa wanufaika, wanaoenda kupokea, unajua kabisa huyu ana uwezo wa kufanya kazi. Bado hatujawa makini kwa asilimia kubwa kuhakikishwa kwamba wanufaika halali ambao ndiyo tunaokusudia hawapati; wanapata wale wajanja wajanja ambao kwa kweli wana uwezo wa kufanya kazi kwa namna moja au nyingine.

Mheshimiwa Spika, suala la ajira. Naipongeza Serikali kwa kutangaza ajira, lakini bado manunguniko ya hawa walimu au manesi ni makubwa. Kila wanapoomba huko vijijini, hawapati, wanapata wa mjini tu. Kama sheria inaruhusu, tugawe kama wanavyofanya wanajeshi. Mwezanagu ameongea vizuri sana pale, Jeshi la Wananchi, Polisi, Magereza, wanazigawa nafasi hizi kulingana na mikoa na Wilaya. Hizi nafasi ukizigawa kwa wilaya, nchi nzima hii wasomi wamejaa. Walimu siku hizi vijijini huko wanajitolea kwa hali ya juu, Wahudumu wa Afya, wako wengi, wamesoma, lakini inapotokea kuomba kwenye mtandao wanapata wa mjini tu, hawa wa vijijini sifa hawana?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba sana Serikali iliangalie kwa hali ya juu kwa sababu huko vijijini tunakotoka wasomi wamejaa, walimu wamejaa. Tunaomba mwangalie; hizo kompyuta ziangalieni, zina macho. Wale tuliosoma kompyuta tunasema garbage in garbage out. Sasa isiwe ikawa inatokea garbage in, garbage out, wanatengwa; watu wa vijijini hawapati hizi kazi. Tunaomba mliangalie mtutengee hizo nafasi kila mkoa kila wilaya ipate. Kila mtu hapa ana barua mifukoni mwao, tuwasaidie hawa watu tupunguze malalamiko ya ajira katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, sheria hizo kama haziruhusu, basi leteni turekebishe. Hao wenzetu wanaofanya kazi ya bodaboda wengi hata ukienda Bolt, sijui wapi, utakuta wasomi kabisa, watu wenye degree wanafanya kazi hiyo. Wameshakata tamaa, ndiyo maana wanaendesha bodaboda. Sasa tunaomba mjitahidi sana, katika hali ya kawaida, kwa kweli tuwajali watu wetu, hizi nafasi zigawiwe kwa uwiano ili kila eneo lipatikane wasomi ambao wanafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, hii itasaidia kitu kimoja; huko vijijini sasa hivi wasomi wenye Degree na Diploma wanachekwa kwamba wewe umepoteza muda wako, umenikuta hapa mimi na jambo fulani, kwa sababu amemaliza Degree yake, anarudi kijijini, naye analima au anaendesha bodaboda. Kuna faida gani? Kwa hiyo, wenzetu, wale wanavijiji wengine wanaona kama model ile siyo sahihi, kwamba kusoma unapoteza muda.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuwajali hawa watu wa vijijini ili waonekane kusoma ni mali. Waangalieni, waliomaliza 2015, 2016 na 2017 waajiriwe, kwa sababu hao ndio waliokuwa wengi na wengi wako vijijini. Hiyo mitandao kule inasumbua kidogo. Kama anashindwa kupata nauli ya kwenda mjini, atapataje hela ya kuweza kununua mtandao?

Mheshimiwa Spika, naomba sana Wizara iliangalie hili, kilio hiki ni kikubwa sana kwa wale wahitimu ambao wako vijijini.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)