Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako hili linafanya kazi kwa mujibu wa Ibara ya (63) (2), (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaipa mamlaka na madaraka kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Spika, nimesikiliza kwa makini sana hotuba ya bajeti iliyosomwa hapa Bungeni leo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa bajeti ya Mwaka wa Fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, nimegundua yapo mambo makubwa ambayo Serikali Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameyafanya kwenye utumishi wa umma. Mambo haya yamefanyika katika kipindi hiki cha mwaka mmoja ambapo Serikali Awamu ya Sita imekuwa madarakani.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana naamini si watumishi wa umma pekee lakini Watanzania wote walipata mshtuko kwa msiba wa kuondokewa na Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Mheshimiwa Spika, kazi iliyofanywa na Serikali ya Mheshimiwa Samia kwa mwaka mmoja, naamini imeleta matumaini makubwa kwenye sekta ya Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako maandiko kwenye Quran Tukufu iko sura alishushiwa Mtume Muhammad (S.A.W) Mwenyezi Mungu akitaka kumtia moyo na sura hii nitaisema hapa. Sura inasema walaak ahkirut kairulaka minaluula. Bila shaka wakati ujao utakuwa ni bora zaidi kuliko wakati uliotangulia. Serikali ya Awamu ya Sita imefanya kazi kubwa. (Makofi/Vicheko)

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Jerry Silaa ukae kuna Wabunge wawili wamesimama hapa. Mheshimiwa Mohamed.

T A A R I F A

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba hii aya ambayo ameinukuu, ameinukuu vibaya. Sasa kwa mujibu wa Quran Tukufu na kwa mujibu wa dini yetu ya Kiislam ukibadilisha herufi moja, umebadilisha maana. Kwa hiyo naomba kumpa taarifa kwamba aya hii inatamkwa walal- akhiratu khairulaka minal uula. (Makofi)

SPIKA: Haya sasa, Mheshimiwa Jerry Silaa hiyo ilikuwa ni taarifa ambayo nafikiri sasa hili jambo ili likae vizuri chukua yeye alivyoinukuu halafu iseme kwa tafsiri. (Vicheko/Makofi)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana mtoa taarifa, Kiiarabu changu kidogo kimechanganyika. Kwa hiyo niombe kumbukumbu sahihi za Bunge zichukue kiarabu cha mtoa taarifa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema wakati huu umekuwa bora kuliko wakati uliotangulia? Ni kwa mambo makubwa ambayo yamefanyika kwenye utumishi wa umma. Kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri tumeona watumishi 190,781 wamepandishwa madaraja na Mheshimiwa Waziri ametueleza hapa kwamba watumishi wengine 92,619 watapandishwa madaraja kabla ya mwezi Juni mwaka huu 2022, ni kazi kubwa sana, tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri vile vile kwenye Hotuba yake ameeleza kwamba wako watumishi 13,495 wamepata ajira mpya, maana yake nini? Wako Watanzania 13,495 waliokuwa tegemezi na leo nao wamekuwa wanategemewa kwa kupata mishahara kupitia utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako watumishi 21,127 wamefanyiwa recategorization kwenye kada zao za utumishi. Sasa maana sahihi ya recategorization nadhani Mheshimiwa Dullo utamtafsiria Babu Talle ili aelewe kazi kubwa iliyofanywa na Serikali hii ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mambo Serikali imefanya, siyo kwenye Wizara hii lakini yana impact kwenye Wizara ya Utumishi wa Umma. Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imetoa non cash bond ya trilioni mbili kwa Mfuko wa Pensheni wa PSSSF ambayo imefanya Mfuko huu kuweza kulipa pensheni kwa wakati. Jana nimezungumza na Mkurugenzi Mashimba, leo tunavyozungumza hapa wastaafu wa mwezi wa tatu tayari wanalipwa pensheni zao, ni kazi kubwa sana imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alitoa agizo la kuongeza wanufaikaji wa Mfuko wa Bima ya Afya, wale wategemezi toka umri wa miaka 18 mpaka umri wa miaka
21. Hivi tunavyozungumza wako watu 77,345 ambao walikuwa wamevuka miaka 18 na ilimpasa mtumishi kama ni mtoto wake atoe pesa mfukoni kumuhudumia matibabu, leo wanahudumiwa na Mfuko wa Bima ya Afya na yenyewe ni jambo kubwa kwenye utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mambo mengi kwa sababu ya muda niseme tu, Mheshimiwa Rais kwa kuthibitisha mapenzi yake na watumishi wa umma wa nchi hii amemteua mtu bingwa kabisa, mwanamke aliyehudumu ndani ya Bunge hili kwa muda mrefu kuliko akinamama wengin,e amekuwa Mbunge wa Viti Maalum lakini amekuwa Mbunge mbobezi wa Jimbo la Peramiho. Amepita Wizara ya Elimu anajua matatizo ya watumishi Walimu. Amekuwa Chief Whip hapa Bungeni na tumeona wote kazi yake. Amekuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi, siyo mwingine ni binti wa Katekista wa Peramiho, Mheshimiwa Jenista Joakim Magigi Mhagama ambaye watu wa namna hii ndiyo wale King Kiba (Ally Kiba) aliwaimba kwenye kibao chake cha utu. Pamoja na upole na uzuri wake lakini amejaliwa utu na utulivu wa hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali imetangaza ajira mpya 32,604. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, niiombe Serikali ajira hizi ziende kuajiriwa kwa haki. Ningetamani sana ajira hizi 32,604 kama vile zigawanywe kama zile pesa za TARURA kila Jimbo lingepata. Nafahamu ziko sheria za Utumishi wa Umma, nia yetu ni kuona kwamba ajira hizi zikitoka maana nadhani kila Mheshimiwa Mbunge hapa ana meseji ya ajira hizi za 32,000. Ni ombi langu, ama ni ushauri wangu kwa Serikali ajira hizi zikitoka tuzione zimetapakaa nchi nzima kwa usawa. Tuone kwenye Majimbo yetu kama kweli ajira 32,604 basi kila Jimbo takribani watu 100 wawe wamepata ajira. Ikifanyika hivyo italeta usawa kwa Taifa, italeta uhimilivu kwa Taifa na itaondoa ile kero ya unemployment kwetu sisi sote kwa umoja wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, nilipita Tabora tarehe 12 Aprili nilikutana na mzee Ramadhani Ally Mkwande, yeye ni mstaafu wa TTCL. TTCL ilikuwa na mkataba na NSSF kulipa pensheni za watumishi wake na wao ni moja kati ya wale watumishi ambao bado wanalipwa shilingi 50,000 kwa mwezi, aliniomba nije kusema Bungeni na nimeona nimtendee haki. Tunaiomba Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ijaribu ku-standardize watumishi wote wafike kile kiwango cha shilingi 100,000 wanachopata pensioners wengine ili na wenyewe waweze kuendesha maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda la mwisho la kusema, niliongea kidogo pale kwenye Mfuko wa PSSSF kwenye ile bond ya two trillion aliyoitoa Mheshimiwa Rais kupitia Serikali yake. Niseme tu Kamati ambayo Bunge lako limekasimia kazi ya uwekezaji inasimamia Mifuko hii, kazi kubwa imefanyika lazima tuseme. Kazi kubwa imefanywa na Serikali kuweza kutengeneza liquidity kwenye Mifuko hii na kazi kubwa inaendelea kufanyika. Nikuombe na niliombe Bunge lako Tukufu, tuendelee kuwatia moyo, tuendelee kuikumbusha Serikali kwa adabu, lakini mwisho wa siku naamini pensioners wa nchi hii wataendelea kupata pensheni zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)