Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Amb. Dr. Bashiru Ally Kakurwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma hotuba ya bajeti ya TAMISEMI iliyowasilishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Mheshimiwa Bashungwa kwa umakini. Kwa kiasi kikubwa TAMISEMI imefanya kazi ya utekelezaji wa mpango wa bajeti ya mwaka 2021/2022 kwa ufanisi na hasa katika maeneo ya utoaji bora wa huduma katika sekta za miundombinu ya barabara za mijini na vijijini kupitia TARURA, elimu ya msingi na sekondari na sekta ya afya. Aidha, utekelezaji wa mpango wa mapambano dhidi ya UVIKO kwa ufanisi umechangiwa kwa kiasi kikubwa na usimamizi na uongozi bora wa watendaji na viongozi walioko TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kufanya tathmini ya utekelezaji wa mpango huo wa kudhibiti UVIKO ili tuainishe maeneo ambayo tunaweza kujifunza. Kwa maoni yangu, baadhi ya mafunzo yaliyojitokeza waziwazi kutokana na mpango huo ni kiwango cha hali ya juu cha utashi wa kisiasa wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ubunifu katika uandaaji wa mipango ya maendeleo na ushirikishaji wa wananchi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti,pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa bajeti iliyopita, napenda kutoa ushauri kwa ufupi kwa TAMISEMI katika maeneo mawili kama ifuatavyo: -

(a) Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ziwe kitovu cha uzalishaji katika sekta za viwanda, kilimo, mifugo na uvuvi kwa kuwa wazalishaji wadogo wako chini ya mamlaka hizo. Fursa nyingi za uzalishaji bado hazijatumiwa kikamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki kigumu kiuchumi duniani kote, mamlaka zilizoko chini ya TAMISEMI zinatarajiwa kuchangia katika kutafuta suluhu ya matatizo ya ajira kwa vijana, tishio la mabadiliko ya tabianchi linaloweza kusababisha upungufu wa chakula, tija duni katika sekta za kilimo, uvuvi na mifugo na ukosefu wa viwanda vidogo vya kusindika mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi.

(b) Ushirikishaji wa wananchi katika kuongeza kiwango cha uzalishaji na kupambana na umaskini unategemea uwezo wa kiuongozi na kiutendaji wa vyombo vya wananchi hasa vyama vya ushirika vya wazalishaji na vyama vya akiba na mikopo. Pamoja na kwamba kisheria na kisera, vyama vya ushirika viko chini ya Wizara ya Kilimo, TAMISEMI ina jukumu la kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya kuboresha utendaji na uongozi wa vyama vya ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naunga mkono hoja.