Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa inayofanyika Serikalini ya kutatua matatizo ya wananchi. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Innocent Waziri wetu wa TAMISEMI na timu nzima Manaibu, Katibu Mkuu wa TAMISEMI na Mtendaji Mkuu wa TARURA pia na Watendaji wote wa Wizara hii walioko chini ya Wizara hii. Mimi ni Mjumbe wa Kamati kwa hiyo mchango wangu ni sehemu tu ya nyongeza kwenye taarifa ya Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru Serikali kwa mradi wa maboresho ya Miji Tanzania (TSCP) kwa Mji wa Mbulu ni mradi mzuri. Mradi huu ndiyo unakuja kugusa wananchi wa Mji wa Mbulu na Miji mingine nchini na kwa kuwa miradi hii inagusa soko, stendi, barabara za lami, dampo na machinjio, vyote vilivyotajwa kwenye mji wa Mbulu haviko. Kwa hiyo naishukuru sana Serikali. Rai yangu kwa Serikali ni kwamba waangalie Miji yenye changamoto nyingi ya miradi hii kwa maana ya kama Mbulu kwa sababu changamoto ni kubwa na inaweza ikagusa maisha ya mafanikio ya wananchi kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ni eneo la ufunguzi wa zahanati kwa kuwa dakika zenyewe ni chache niseme tu kwamba wananchi wana hamu kubwa na haiba kubwa ya kujenga miradi ya zahanati. Katika mji wa Mbulu tuna zahanati nne zilizo tayari kwa maana ya Halmashauri ya Mji wa Mbulu, lakini zahanati hizo zilianzishwa siyo mwaka huu zilianzishwa miaka minne iliyopita, kwa sababu hiyo basi, tungeiomba Wizara waangalie zahanati zote zilizo tayari kwa kuwa wameandika kwenye taarifa ya mpango wa bajeti basi ziweze kufunguliwa baada ya Julai ya mwaka huu kwa ajili ya mwaka huu wa bajeti ili tuweze kuona wananchi walioanzisha zahanati miaka saba, miaka tano, miaka nne basi waweze kuona manufaa ya miradi walioanzisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyingine ni ahadi za Viongozi Wakuu hasa zinazogusa eneo letu la TARURA. Mheshimiwa Rais Hayati Magufuli aliahidi lami kilomita tano katika Mji wa Mbulu, hadi sasa ni kilomita 2.5 zinazotekelezwa inaonyesha kama vile chini ya mita 500 kwa mwaka kwa bajeti ya mwaka kwa barabara hizo. Kwa hiyo, sababu yake hapa ni kwamba Viongozi hawa Wakuu wanaporudi wananchi wanaanza kuhofu na kufikiri kwa nini miradi hii au ahadi hizi za viongozi wakubwa zinachelewa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani TARURA kupitia TAMISEMI waende waratibu upya ahadi za Viongozi Wakuu halafu baada ya hapo waweze kuweka kwenye vipaumbele kadri ya miaka inavyokwenda ili kuondoa madeni ya ahadi za viogozi wetu wa ngazi zile za nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni posho za Waheshimiwa Madiwani. Bahati nzuri mimi nilianza kuwa Diwani posho za 350,000 zilitolewa kwa miaka karibu 10 sasa na kwa kweli hali ni mbaya sana kwa Waheshimiwa Madiwani mimi niungane na wale Wabunge wenzangu waliozungumzia jambo hili kwa upana isitoshe hiyo hata posho za vikao wanapewa 40,000 wakati nikiwa Diwani posho ya kikao kimoja ilikuwa sitting ni 70,000 lakini wakati huo huo night za kutoka kwenda kwenye vikao ni siku tatu maana 65,000 x 3 = 195,000 + 70,000 sasa hivi ni 40,000 hata ungekuwa unaenda wapi na vikao vinapoisha Waheshimiwa Madiwani wanatembelea bajaji, wanatembelea boda boda wanalala katika mazingira magumu huko vijijini ndiyo wao wanasimamia shughuli za maendeleo na watendaji wanaosimamiwa wana mishahara mikubwa sana. Kwa hiyo siyo rahisi mtu anayesimamia watendaji wengine yeye anakuwa na posho kidogo kiasi hicho. Mimi ninafikiri ni muda muafaka wa sisi kutazama upya ili kuona ni namna gani kwa kadri ya mapendekezo ya Kamati yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji hawa ni watu muhimu sana nao tusiwaache kwa kweli, kwa sababu Mheshimiwa Waziri Innocent sina mamlaka ya kushika mshahara wako lakini hatutarajii kwamba mshahara wako unakwenda kushikwa kwa ajili ya jambo hili limezungumzwa kwa upana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ni kwamba naishukuru Serikali wameweka daraja la Unyoda lililokuwa kikwazo na limetenganisha Halmashauri mbili katika mpango. Ninaomba wasiondoe iendelee na baada ya Julai tuanze utekelezaji wake. Eneo jingine ni ukarabati wa shule kongwe nchini, Halmashauri ya mji wa Mbulu au Mji wa Mbulu ni Mji ulioanzishwa na wakoloni kwa takribani sasa shule asilimia 60 ya Mji wa Mbulu ni shule kongwe kwa sababu ndiyo Makao Makuu ya Wilaya ya Mbulu ambayo imezaa Karatu, imezaa Babati, imezaa Hanang na sasa Mbulu Vijijini. Kwa hiyo eneo hili nalo ni muhimu sana kwetu sisi tunaiomba Serikali iangalie kwa mapana yake namna ambavyo itaweza kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nichangie eneo la Milioni 500 kwa kilomita moja, Mheshimiwa Waziri na watu wa TARURA, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara kwenye Jimbo la Mbulu Mji alikuta mradi wa kilomita moja bado haujatekelezwa, ulitangazwa mara tatu hauna Mkandarasi, hebu tujiridhishe tatizo ni Watendaji hawatimizi wajibu wao, ama ni fedha hazitoshi za Milioni 500 kwa sababu kilomita moja ina mifereji, kilomita moja ina lami, kilomita moja ina taa za barabarani, kilomita moja kuna culvert huko huko tuangalie na kama tatizo siyo hilo basi hata sasa huo mradi ndiyo unaanza kutekelezwa utakamilika lini huu wa kilomita moja ili fedha hizi ziweze kutazamwa na ikidhi haja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla tunaishukuru Serikali kwa kazi kubwa inayofanya. Watutolee pia fedha za ukamilishaji wa miamala kwa ajili ya vituo vya afya ili walau miradi iendane na mwaka wa bajeti na tuweze kukamilisha miradi yetu kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri nyingi zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa Wahandisi kadiri tunavyopeleka fedha nyingi vijijini, fedha nyingi kwenye Halmashauri hatuna Wahandisi, mimi nadhani tufanye tathmini ya mapitio tuna Wahandisi wangapi wako eneo gani Halmashauri gani haina Mhandisi nini kifanyike kwa hatua ya dharura ili miradi iende kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana nimechangia kwa muhtasari kwa sababu mimi ni Mjumbe wa Kamati nayarudia kuyakumbusha yale tuliyojadili, naunga hoja mkono kwa asilimia mia moja, naomba kuwasilisha.