Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara hii. Naomba nianze kwa kumpongeza Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuifungua nchi yetu Kimataifa, vilevile kwa nia yake ya dhati aliyotuonesha Watanzania kwa kutuletea maendeleo kwenye hili tumeona kabisa amegusa huduma muhimu zile za msingi ambazo zinagusa wananchi moja kwa moja kama huduma za afya, elimu, barabara, pamoja na maji safi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia, niendelee kuwapongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inaweza kuendelea na kwa ufanisi mkubwa. Vilevile niwapongeze Watendaji wote wa Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa wakiongozwa na Waziri wetu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa usikivu wao wa hali ya juu pamoja pia na kuendelea kufuata ushauri wa Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita kwenye kushauri mambo kadhaa ambayo basi yataweza kuendeleza Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Naomba nianze kuchangia kwenye utekelezaji wa program ya kuwarudisha wanafunzi wetu mashuleni, hasa wale waliopata changamoto mbalimbali hususan ujauzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa kwenye hili naomba nianze kwa kumpongeza na kumshukuru Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu basi wa kuwarudisha wanafunzi wetu shuleni na kuwapa fursa nyingine mabinti wetu waweze kupata fursa ya kuendelea kielimu na baadaye kuweza kujikwamua kiuchumi. Kwenye program hii changamoto bado ni kubwa katika utekelezaji wake. Kwenye Halmashauri zetu nyingi hakuna miongozo madhubuti ya kuweza kufuatilia masuala haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Halmashauri zetu nyingi hakuna taarifa rasmi za wanafunzi hawa, wanafunzi ambao wamekatiza masomo yao, wanafunzi ambao wamerudishwa shuleni kwa kipindi chote hiki. Na ukiangalia taarifa ya Mheshimiwa Waziri hapa katika ukurasa wa 21 hadi wa 27 kwenye hotuba yake utaona ametueleza data mbalimbali za uandikishwaji wa wanafunzi kuanzia elimu za awali mpaka kidato cha tano, idadi ya wanafunzi waliohitimu, elimu ya watu wazima na taarifa za wanafunzi waliopata elimu nje ya mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa hatujaona taarifa za wanafunzi hawa waliokatisha masomo yao katikati na vilevile wakarudishwa katika mfumo huu rasmi wa elimu. Hapa tunawanyima sana fursa mabinti zetu waliokatisha masomo na wenye hamu bado ya kuendelea kusoma. Tunawanyima fursa kwa sababu, hawana taarifa ya jinsi gani waweze kurudi kwenye mfumo rasmi. Nikichukulia mfano tu kwenye Mkoa wangu wa Arusha, Halmashauri zetu nyingi ikiwemo Longido, Ngorongoro, Meru, Arumeru, hakuna taarifa hizi, nimefuatilia binafsi, lakini sijapata taarifa hizi.

Naomba nitoe ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hapa basi aweze kutuambia mikakati yake aliyonayo, mikakati ya Wizara iliyonayo kwa ajili ya kuhakikisha taarifa hizi zinapatikana rasmi na kunakuwa na miongozo rasmi kwa ajili ya kufuata kwenye Halmashauri zetu ili basi wanafunzi wetu hawa waweze kupata nafasi nyingine ya kurudi katika mfumo rasmi wa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine naomba nichangie na kutoa ushauri wangu ni kuhusiana na mikopo ya asilimia 10 ambayo inatolewa na Halmashauri zetu. Changamoto za mikopo hii bado ni nyingi sana, kama Kamati ya Serikali za Mitaa ilivyoainisha hapa changamoto hizi ni nyingi na ushauri wake kwa Serikali basi Serikali inabidi ije na mikakati madhubuti kwa ajili ya kuweza kufuatilia utekelezaji wa mikopo hii ili iweze kuleta ufanisi kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Kamati inaonesha kuna Halmashauri zaidi ya 24 ambazo zimekopesha chini ya asilimia 50 ya mapato ya fedha zilizotengwa hadi kufikia Februari 20/22.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutenga kwa asilimia 10 ya mikopo ya Halmashauri ni takwa la kisheria kwa hiyo sioni sababu ya kwa nini Halmashauri zetu zinaacha kutenga asilimia 100 ya fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya mikopo ya Halmashauri kwa makundi yale tajwa ya wanawake, vijana na walemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia changamoto nyingine ya marejesho wamesema wenzangu hapa hii ni changamoto kubwa sana ukiangalia kwenye taarifa tumeona kwamba kuna zaidi ya asilimia 50 ya fedha zote zilizokopeshwa kwa wananchi kuanzia mwaka 2018 hadi Februari, 2022 bado ziko mikononi kwa wananchi hawajaweza kurudisha na hakuna mikakati madhubuti basi ya Serikali kufatilia marejesho ya mikopo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utoaji wa mikopo ni takwa la kisheria basi tunaomba pia tuweke kanuni kali na miongozo ya kufuatillia marejesho ya mikopo hii ili basi ziweze kurudi kwenye mfumo ule revolving fund na wananchi wengi zaidi waweze kukopeshwa mikopo hii. Ukiangalia tu katika Mkoa wa Arusha tokea mwaka 2018 tumeweza kutoa mikopo takribani bilioni 12.7 lakini ni bilioni tano tu ambazo zimerejeshwa zaidi ya Bilioni Saba bado zipo mikononi mwa wananchi na hakuna kanuni maalum ya kuweza kuifuatilia hii mikopo iweze kurudishwa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto zote hizo nimeona kamati pia imetoa ushauri mzuri mojawapo ni kuwepo kwa mifumo imara ya TEHAMA ili kuweze kufuatilia mikopo hii vilevile Mheshimiwa Waziri hapa wakati anatoa hotuba yake alitueleza hapa kwamba wataweka kigezo cha kuwapima Wakurugenzi wetu kutokana na ufanisi wa mikopo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakurugenzi wetu tayari wana kazi za kuwatosha na kazi hizo ndiyo zinapelekea mpaka tumefika leo hapa mikopo hii imeshindwa kufanyakazi kwa ufanisi. Kwa hiyo naomba kwa sababu changamoto hizi za mikopo zinajulikana kwenye Halmashauri zote 124 ni changamoto ambazo ziko common tuwatafutie Halmashauri zetu solution ambazo ni common pia ili basi Halmashauri zetu zote ziweze kufuata ili mikopo hii iweze kuwa na ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)