Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Mwantumu Mzamili Zodo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nami kwa kupata fursa hii ya kuweza kuchangia Wizara hii nyeti, Wizara ya TAMISEMI. Kwanza kabisa kabla sijaanza kuchangia naomba niwapongeze Mawaziri wote wa TAMISEMI wanafanya kazi nzuri, Mheshimiwa Bashungwa, Mheshimiwa Dugange na Mheshimiwa Silinde.

Pia naomba niwapongeze watendaji wote wa TAMISEMI wakiongozwa na Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Prof. Shemdoe wanafanya kazi nzuri na ni wa sikivu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sintomshukuru Mheshimiwa Rais. Kama sintamshukuru Mheshimiwa Rais na kumpongeza kwa kutupatia fedha za UVIKO na kujenga madarasa ya kisasa Tanzania nzima, na kwa muda mfupi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sintomshukuru Rais kwa kutupatia fedha za tozo kuhakikisha tunajenga vituo vya afya; kuna baadhi ya vituo vya afya tulipata Milioni 250 za awali kwa ajili ya vituo vya tozo kwa Mkoa wetu wa Tanga, pia ni juzi tu zimeingizwa Milioni 250 tena kwa ajili ya umaliziaji wa vituo hivi vya tozo, tunamshukuru sana Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu sasa kwa TAMISEMI ni kuhakikisha wanatoa maelekezo kwa Wakurugenzi, vituo hivi vya tozo vinakwenda kukamilika kwa wakati kwa sababu fedha zake zote Milioni 500 baadhi ya maeneo imekamilika na imeshapelekwa. Kwa hiyo, naomba sana TAMISEMI muongeze nguvu muendelee kuwa-puSh Wakurugenzi ili vituo hivi vikamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivyo mtoe maelekezo kwa Wakurugenzi. Baadhi ya Wakurugenzi wanafanya kazi nzuri sana, lakini baadhi ya Wakurugenzi kwa kweli ni tatizo na wanawaangusha sana TAMISEMI. Sasa hivi tupo safarini tupo baharini kwa hiyo tukiona mtu yeyote ana dalili ya kutoboa mtumbwi ni vizuri Mheshimiwa Waziri mapema tukamtosa yeye baharini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, zipo baadhi ya Halmashauri ambazo hazikutekeleza kabisa miradi ambayo tuliwapitishia mwaka jana kwa ajili ya bajeti na badala yake wamejificha kwenye madarasa ya UVIKO na vituo vya afya vya tozo. Kwa hiyo, kila unapokwenda kwenye ukaguzi kwenye Halmashauri wanakuonesha miradi ya UVIKO na miradi ya tozo lakini wao hawakutekeleza miradi yao kwa mapato yao ya ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano zipo baadhi ya Halmashauri ambazo zimeishaingiziwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya, zipo nazifahamu, naomba Mheshimiwa Waziri baada ya wachangiaji utakapokuja kukamilisha hotuba yako utoe tamko kuhusiana na Wakurugenzi ambao wamepelekewa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi, fedha zipo kwenye akaunti lakini mpaka sasa wengine wapo kwenye hatua za msingi, wengine wanamwaga jamvi! Wakurugenzi hawa wanawaangusha Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba Wizara yako, madarasa yamejengwa ni mazuri na ni mwaka jana tu baadhi ya shule wameongezewa shule za Kidato cha Tano na cha Sita, lakini shule hizi hazina uzio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano shule ya Tanga Tech pale Tanga Mjini ni shule kubwa na ni shule kongwe. Zamani ile shule ilikuwa ipo mbali sana na makazi ya watu lakini kadri mji unavyokua makazi ya watu yamekuwa yapo karibu sana na ile shule na shule ile haina uzio ni hatari sana kwa vijana wetu lakini hata shule ya Galanosi, Maramba High School na baadhi ya shule nyingine nyingi za Tanzania. Kwa hiyo, naombeni pia mje na mkakati wa kuzijengea uzio hasa shule zetu za bweni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitakuwa mchoyo fadhila kama sintaungana na wenzangu kuhusu posho za Madiwani. Mheshimiwa Waziri Madiwani wanafanya kazi kubwa ya kusimamia miradi yetu lakini pia Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji, Watendaji Kata, Watendaji wa Mitaa na Watendaji wa Vijiji. Kwa hiyo, naomba nao pia waangaliwe kwa jicho la huruma. Madiwani wajaribu kuongezewa posho lakini Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Watendaji…

MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hawa Mchafu taarifa.

T A A R I F A

MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nasimama kwa Kanuni ya 77(1). Napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Mzungumzaji aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Ummy Mwalimu alisema hapa kwamba taratibu au mchakato kuhusiana na posho za Madiwani tayari ulishaanza. Kwa hiyo, Wizara ni ileile, Naibu Mawaziri ni wale wale pengine aliyebadilika ni Waziri. Tulikuwa tunaomba sasa waanzie pale alipoishia Mheshimiwa Ummy Mwalimu na kuendelea mbele kuhusiana na hii posho ya Madiwani. Naomba nimpe taarifa mzungumzaji. Ahsante.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Hawa kwa taarifa ambayo inaboresha mchango wake. Taarifa inatakiwa iwe uelekeo kama huo, kuna kitu kina-miss unakiongezea. Ahsante endelea Mheshimiwa unaipokea taarifa?

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na nashukuru sana kwa taarifa naipokea. Naomba Watendaji Kata, Vijiji na Mitaa hasa ukizingatia mwaka huu tunakwenda kwenye Sensa ya Watu na Makazi wapewe mafunzo. Tunacho Chuo chetu cha Utumishi ambacho kazi yake hasa ni kuendelea kuwajengea uwezo Watumishi wetu wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watendaji hawa wanafanya kazi kubwa na mwananchi wa kawaida kabisa Serikali yake ya kwanza anayokutana nao ni hii. Tulishuhudia baadhi ya miradi tukiwa tunakwenda kukagua miradi, wananchi wanamsikiliza Mtendaji wa Kijiji kuliko Mkurugenzi. Wananchi wanamsikiliza Mtendaji wa Kijiji kuliko hata Mkuu wa Wilaya (DC), kwa hiyo watu hawa ni muhimu sana tusiwaache wapewe mafunzo ya muda mfupi wakiwa kazini kupitia Chuo chetu cha Utumishi ambacho kina matawi yake kila Kanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna chuo hiki Tabora kwa ajili ya Kanda Ziwa na Kanda ya Magharibi, lakini kipo Chuo hiki Dar es Salaam kwa ajili ya Kanda ya Mashariki, pia kuna branch nyingine ipo Tanga kwa Kanda ya Kaskazini, kipo Chuo hiki Singida kwa ajili ya Kanda ya Kati, pia kipo Mtwara kwa ajili ya Kanda ya Kusini na kipo Mbeya kwa ajili ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana TAMISEMI na Katibu Mkuu najua atalibeba hili, Naomba Katibu Mkuu hangaika nalo hili kutafuta fedha kwa ajili ya hawa watu kupatiwa mafunzo ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)