Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye hoja ya Waziri wa TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimpongeze Mheshimiwa Daktari Philipo Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimpongeze Mheshimiwa Kassim Majaliwa Waziri Mkuu wa Serikali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa iliyotukuka ya kutuletea maendeleo endelevu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wana Buhigwe tunawashukuru sana kwa miradi mingi ambayo Mama ameleta. Tumejenga madarasa 53 kutoka kwenye fedha ya UVIKO, tumepata fedha za vituo viwili, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi nyingine ya pekee kumpongeza na kumshukuru Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Innocent Lugha Bashungwa, lakini nimpongeze tena David Ernest Silinde Naibu Waziri wa TAMISEMI na Daktari Festo John Dugange kwa kazi kubwa wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwenye uchangiaji wa hoja. Nimesoma Hotuba yako mwanzo hadi mwisho, ninashukuru hotuba iko vizuri na mimi ninaiunga mkono. Ukurasa wa 46 kwenye miradi ya kimkakati Buhigwe ni Wilaya mpya ni Wilaya changa, bado tuna mapungufu makubwa sana. Mapato yetu ya ndani ni madogo sana, hatuna stendi ya Wilaya kwa ajili ya mabasi, hatuna stendi ya malori, hatuna soko la Makao Makuu la Wilaya. Ninamuomba sana Waziri wa TAMISEMI atukumbuke katika mpango wake, katika bajeti yake ya 2022/2023 kutupa mradi wa kimkakati utakaoweza kutuongezea mapato ikiwa ni pamoja na stendi ya mabasi, stendi ya malori na soko la Wilaya la kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 66 na ukurasa wa 105, nimeona pale kwenye upande wa TARURA kwenye bajeti yako umeeleza kinagaubaga kwamba kwa mwaka 2022/2023 madaraja na vivuko 322 vinaenda kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Buhigwe tuna matatizo makubwa sana ya kimawasiliano, tunalo daraja ambalo ni muhimu sana la kuunga Wilaya ya Buhigwe na Wilaya Kigoma Kaskazini, ukitokea daraja hilo lijengwe ukitokea kwenye Kijiji cha Kigogwe kwenda kwenye Gereza la Kwitanga. Kwenye bonde la mto huo kuna vijiji takribani Nane ambavyo vinalima sana zao la tangawizi na vimeitikia mwito wa zao la chikichi ambalo Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amelisimamia kweli. Vijiji hivi ni Kigogwe, Mrungu, Kishanga, Munzenze, vyote hivi vinahitaji viunganishwe, daraja hili ni kubwa nalo ni la mto Ruiche. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambasamba na hilo nichukue nafasi ya pekee kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Shilingi Milioni 500 alizotupatia, ninaomba tena kwa bajeti ijayo atupatie Milioni 500 kwa Majimbo ili tuweze kutengeneza tena barabara zetu huko Majimboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yangu wananchi wamefanya jitihada kubwa sana. Kuna maboma makubwa ya Zahanati, maboma hayo ya Zahanati yapo katika Kijiji cha Kitambuka, Msagala, Ndoha, Mulungu, Kimara, Mbanga, Chagwe, ninaomba na Waziri wa TAMISEMI ananisikia kwa dhati kabisa Wanabuhigwe wamenituma haya maboma ya Zahanati yana zaidi ya miaka saba yanahitaji kupauliwa tu, Milioni 50 zinatosha tungeomba utusaidie katika bajeti ijayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na maboma ya zahanati ni kwenye Elimu. Buhigwe kuna Kata ambazo zimefanya jitihada zimejenga zenyewe zinasubiri msaada wa kupaua, maboma yako tayari kwa ujenzi wa shule za sekondari nayo yamejengwa katika vijiji vifuatavyo, Kilelema, Mbanga, Chagwe, Kirungu na Songambele, tunahitaji katika bajeti ya mwaka ujao na Wizara hiyo ilione.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii ya pekee kuungana na Wabunge wenzangu kwa kutambua kazi kubwa wanayoifanya Madiwani, posho na mshahara wanaoupata hauwatoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo awali posho za Madiwani zilikuwa ikilipwa na Halmashauri, posho zao zilikuwa zikilipwa na Wakurugenzi, ninaomba ikiwezekana uelekeze sasa viwango vile vilivyokuwa vikilipwa na Halmashauri vikawaendee Wenyeviti wa Serikali za Mitaa, Wenyeviti wa Serikali ya Vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wanafanya kazi kubwa sambamba na Watendaji wa Vijiji lakini Serikali imewasahau wanaacha shughuli zao usiku na mchana wanafanya kazi za kusimamia miradi yetu, Serikali iwakumbuke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo machache ninaunga mkono hoja. (Makofi)