Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia maoni na mawazo kuhusiana na taarifa ya Kamati mbili; Kamati ya Katiba na Sheria na Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuzishukuru Kamati hizi mbili kwa namna ambavyo inatusaidia Serikali hususani sisi Wizara ya Katiba na Sheria. Kamati hizi zinafanya kazi nzuri ya kutoa ushauri na maelekezo ambayo wakati wote tumeyapokea na kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba naunga mkono taarifa za Kamati zote mbili. Tumepokea ushauri wa Kamati zote mbili na niahidi kwamba Serikali hii ni Serikali Sikivu, tutakwenda kuzifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niruhusu niseme mambo machache; la kwanza ni haki za binadamu ambazo zimeelezwa kwenye Katiba hasa Ibara ya 12 hadi 28.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulifanya mabadiliko ya Katiba mwaka 1984, tukaingiza haki hizi, lakini tunapozisoma hizi haki ni vizuri tusome sambamba na Ibra ya 29 pamoja na Ibara ya 30 ya Katiba ambayo sio tu inaelezea haki hizi unaweza ukazifurahia kwa kiasi gani, lakini inaelezea umuhimu na wajibu wa kulinda haki za watu wengine wakati unafurahia haki hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeelezwa hapa kwa mfano haki ya faragha ambayo imeelezwa kwenye Ibara ya 16 na hii imekuwa ikitamkwa sana. Ni kweli sheria imetoa haki ya faragha, lakini unapofanya faragha lazima uzingatie sheria za nchi, usije ukatumia faragha mle ndani kufanya uhalifu. Ukifanya uhalifu ile faragha yako itachukuliwa na tutaanza kufuatilia ule uhalifu ambao unaufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia limeongelewa suala la Shule ya Sheria (Law School) yameongelewa mengi, lakini Mheshimiwa Swalle ameongea suala moja muhimu sana kuhusiana na ajira za wanasheria kutakiwa kwamba kila mwanasheria lazima awe amepitia Law School.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tumelipokea na tunakwenda kufanya tathmini na tutarudi kwenye Bunge hili kuwaambia tathmini yetu ni nini ili kwa kazi ambazo hazihitaji Law School na mtu ana degree ya sheria tumruhusu akafanye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mathalani kwenye tume ya usuluhisho wa migogoro ya kazi, ajira inataka watu ambao wamesomea fani za sosholojia waweze kuajiriwa, watu waliosomea fani za sheria waweze kuajiriwa, lakini huyu wa sheria lazima aende Law School. Sasa unaona hapa mzani haujakaa sawia, tumelipokea na tunaenda kulifanyia kazi Serikali hii ni Sikivu, tutarudi katika Bunge hili tukufu kuomba ridhaa yenu ili tuweze kuondoa tatizo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limeongelewa hapa ni matumizi ya lugha ya Kiswahili katika kutafsiri sheria zetu. Hivi sasa tuna sheria 446 kati ya hizo, sheria 216 zimekwishatafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili. Kazi hiyo ni endelevu na Serikali inaendelea kupambana ili kuhakikisha kwamba sheria zote hizi zinatafsiriwa katika lugha ya Kiswahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho, ningependa kuongelea kuhusiana na Ofisi ya Mwendesha Mashtaka ya Taifa (National Prosecution Services Office).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya mabadiliko makubwa kwenye sheria hii na hivi sasa baada ya kumpata Mwendesha Mashtaka Mkuu, Bwana Sylivester Mwakitalu, amefanya mabadiliko makubwa, amefanya ugatuzi, anafanya usimamizi na sasa hivi uendeshaji wa mashtaka umebadilika sana, hasa chini ya Awamu ya Sita kwa sababu ya mabadiliko hayo. Hii tume ambayo Mheshimiwa Rais ameiunda, inakwenda kuangalia mfumo mzima wa sheria za jinai ambao ulikuwepo toka wakati wa ukoloni na tunaamini sasa itasaidia kwenye maboresho haya ambayo Ofisi ya NPS imekuwa ikiyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)