Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na mimi naomba nijielekeze katika kuchangia hoja za Kamati mbili ambazo zimewasilishwa hapa; Kamati ya Katiba na Sheria na Kamati ya Sheria Ndogo ambayo mimi pia ni Mjumbe wa Kamati hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti,nizipongeze Kamati hizo kwa kazi nzuri sana ambazo zimefanya katika kupitia na kujadili kazi zake ambazo zinaonesha moja kwa moja Bunge liko serious katika kuisimamia Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye mjadala wa Kamati ambao mimi ninahudumu ya Sheria Ndogo. Kama ambavyo wazungumzaji wengi wamezungumza hapa, ukiangalia kwa undani nchi yetu na sheria za nchi yetu zinaeleza kwamba Bunge ndio chombo cha kutunga sheria, lakini utaratibu wa kutunga sheria nchini kwetu umepelekea Bunge kukasimisha kwenye mamlaka mbalimbali kwa ajili ya kulisaidia Bunge kutunga sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzoefu ambao nimeuona kwenye sheria ndogo mbalimbali ni kwamba hawa wenzetu ambao tumewakasimisha kazi ya kutunga sheria na kanuni na miongozo mbalimbali kwa niaba ya Bunge wamekuwa wakifanya mambo haya kama vile hawako kwenye nchi hii hii ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia asilimia kubwa ya sheria ambazo tumekuwa tukikutana nazo kwenye Kamati ya Sheria Ndogo, ukiiangalia unajiuliza hii sheria wakati wanaitunga walishirikisha kweli wadau? Kwa sababu sheria kabla hujaitunga inayoenda kutumika kwa watu ni vizuri ukawashirikisha, kwa sababu haiwezekani kwamba watu wa Misungwi wawe wameshirikishwa kwenye sheria ndogo za Halmashauri ya Misungwi ambazo zinasema kwamba wafunge maduka kuanzia asubuhi mpaka saa tano siku ya Jumamosi. Unakuta Sheria hizi zinatengenezwa na watu wachache, wanajifungia, wanatengeneza vitu ambavyo vinaleta kero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo sababu ya msingi sana ya Bunge letu kama ambavyo baadhi ya wasemaji wameshauri, sheria hizi ndogo ambazo zinatungwa kabla hazijaanza kutumika na kuleta kero kwa wananchi na kuleta usumbufu lazima ziwe na baraka ya Bunge, kwa sababu sisi ndio tunaotunga hizi sheria. Haiwezekani katika uzoefu wangu wa kukaa kwenye Kamati ya Sheria Ndogo nilishakutana na Sheria ya LATRA ambayo ilielekeza kwamba bodaboda zifungwe ving’amuzi, nikawahi kujiuliza hivi aliyekuwa anafikiria kwamba ili kuleta usalama, kuondoa wizi kila bodaboda ifungwe king’amuzi na king’amuzi unakuta kinauzwa zaidi ya shilingi 200,000 alikuwa anafikiria, akifikiria bodaboda za Dar es Salaam peke yake au alikuwa anafikiria na bodaboda za Sumve. (Makofi)

Kwa hiyo, unakuta wenzetu wanafikiria katika wigo mdogo sana na wakati mwingine katika wigo wa upigaji wanatengeneza kanuni ambazo zinatuletea shida kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu mimi kwa Bunge, tuchukue nafasi yetu sisi kama watungaji sheria, tusiruhusu mamlaka yetu ya kutunga sheria yatumike kunyanyasa wananchi kwa sababu ya nafasi tuliyowatolea wenzetu ya kutunga sheria ndogo na kanuni. Mawaziri wanamamlaka ya kutunga sheria kwa kupitia Bunge. Tumewapa kazi yetu tu hawa watusaidie, sasa wanapotunga kanuni ambazo zinanyanyasa wapiga kura wetu ni lazima Bunge lichukue nafasi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maazimio, azimio la kwamba sheria ndogo kabla hazijaanza kazi zije hapa Bungeni, naomba liongezwe ili kuwe kuna tija kwenye utekelezaji wa sheria tunazotunga humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia kidogo pia suala la ajira; nadhani sote hapa tunafahamu, Wabunge wenzangu ni mashahidi mimi nina makablasha na CV za watu wengi sana wanaomba wasaidiwe kupata kazi. Hii ni alama kwamba Watanzania wengi hawana imani na mfumo wa ajira wa nchi hii. Wangekuwa wana imani na mfumo huo wasingekuwa wanataka kupitia mlango wa nyuma kusaidiwa na Wabunge kupata ajira. (Makofi)

Kwa hiyo, Mwenyekiti nakurudisha...

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa tu mzungumzaji Sheria za Ajira katika nchi hii kupitia katika mfumo, siku ya kutangaza kwamba ajira zinatangazwa kwa siku 21 au siku 14; siku moja inakuwa wazi siku 14 zote mifumo inazimwa, halafu wanaajiriwa watu kutoka sehemu moja au watu wenye ndugu muhimu, haiwezekani katika nchi hii. Wabunge tusilikubali jambo hili ahsante, endelea na mchango wako. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mageni unaipokea taarifa hiyo? Sina hakika kama ina ukweli kiasi gani.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo naipokea na ninaomba unitunzie muda wangu, Mheshimiwa Tabasam ametoa taarifa moja nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mifumo ya ajira kama kuna wakati fulani hapa nilisikia Waziri wa Fedha anasema mifumo haina shida. Mfumo wa ajira una shida, watu wanapoomba kazi namna ya kuomba kazi ule mfumo wanasema umezidiwa, lakini wewe Mwenyekiti ni shahidi wote hapa tunatumia mitandao ya simu, inatumiwa na Watanzania wote, kwa nini mifumo ya mitandao ya simu haizidiwi, lakini mifumo ya ajira peke yake ndio inazidiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nafasi za ajira mfano zinaweza zikatangazwa 100; watakuja wanafanya interview, unakuta interview inafanyika kwa watu laki, watu wanakusanywa, wanapoteza muda wao, na baadae inapofika wakati wa kuajiri unakuta hata hizo nafasi 100, ukienda kuangalia kwenye tangazo unakuta wameajiri watu 60, lakini watu walioambiwa wanasifa ya kuajiriwa labda ni watu 300. Kwa hiyo, hapa kuna namna fulani ya upigaji deal kwenye mambo ya ajira. Wale wanaomba kazi wanaona huo upigaji deal, wanaona watu wengi wanapewa wengine hawapewi na hizi ajira kama alivyosema Mheshimiwa Tabasam zimekuwa ni watu fulani tu wa Dar es Salaam, Dar es Salaam hivi, sisi watu wa Bujingwa, wa Mwashilalage hatuhusiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili na sisi tuhusike rudisha kwenye halmashauri huko nafasi za ajira kila halmashauri ipewe, kwa nini majeshi yanaweza, wanaleta kwa mshauri wa mgambo kwenye Wilaya zetu…

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Haya ya ajira yame…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kasalali hebu hitimisha hoja yako.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti okay.

Haya mambo ya ajira kwa nini yameng’ang’ania makao makuu? Ajira zinatolewa mikoani huko watu wa ku interview wanatoka huku kwenda kule wanaenda na majina yao. Watu wa Kwimba wanaomba kazi hawapewi wale wanaokuja kusimamia hizo ajira wanakuja na majina kutoka Dodoma na sisi watu wa Chanza tunataka ajira hatujaja kusindikiza kwenye hii nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba niunge mkono hoja za Kamati zote mbili na ninaomba maoni ya kwangu yazingatiwe kwenye…

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)