Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii ya kwanza kabisa kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja za Kamati hizi mbili za Kudumu za Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayofanya ya kuiendeleza nchi yetu. Hakika ustawi wa nchi yetu sasa uko kwenye mikono salama, kutokana na jitihada anazozifanya Rais katika kujenga umoja wa kitaifa, kulinda muungano wetu, kutafuta uwezo kutoka nje na uwezo wa ndani ili kuleta ustawi wa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi Mheshimiwa Rais ameendelea kusaidia nchi yetu kuongozwa katika misingi ya kidemokrasia, misingi ya haki inayojali utu wa binadamu na ndio maana Mheshimiwa Rais amekataza watu wengine kufikishwa mahakamani, bila kesi zao kukamilika au upelelezi kukamilika, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuwapongeza Wenyeviti wote wawili wa Kamati zote za kudumu kwa taarifa zao nzuri pamoja na Wabunge wanaounda Kamati hizo zote mbili wamefanya kazi nzuri na taarifa zao zote ni nzuri na nitamke bayana kwamba ninaziunga mkono taarifa zote mbili za Kamati hizo mbili za kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee na hata pamoja na malalamiko mengi ambayo yametoka katika ukumbi huu leo asubuhi, kulalamikia baadhi ya maeneo ambayo mambo hayaendi vizuri na hasa baadhi ya taasisi ambazo zimekuwa zimepewa mamlaka ya kutunga sheria hizi ndogo na kwa bahati mbaya wakawa wanatunga sheria ambazo kimsingi zinakinzana na sheria za Bunge na hata wakati mwingine kupingana au kukinzana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali Jaji Feleshi, kwa kiwango kikubwa tangu ameingia katika ofisi hiyo, kwa kweli naona utulivu mkubwa na ushirikiano wake mkubwa sana wa kuishauri Serikali ipasavyo. (Makofi)

Sisi wengine tunaojua rekodi yake akiwa DPP, akiwa Jaji na hatimaye Jaji Kiongozi tunaamini kabisa ofisi hiyo iko salama na nampongeza yeye pamoja na DPP wa sasa. DPP wa sasa anafanya kazi nzuri na nina hakika haya ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyazungumza katika Bunge hili la leo zitarekebishwa na viongozi wetu hawa wawili ambao wanaongoza taasisi hizo muhimu sana. Pia kwa namna ya pekee nawapongeza pia Mawaziri wa Wizara hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nijielekeze sasa katika baadhi ya maeneo ambayo ni ya maana sana na ni ya msingi pia katika hoja za Kamati zilizowasilisha leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na malalamiko mengi juu ya baadhi ya mambo ambayo hayajakaa vizuri na hasa katika maeneo yale ambayo yanahusiana na dhamana tuliopewa Kikatiba kwamba Bunge lako tukufu lina mamlaka ya kutunga sheria, lakini bahati mbaya sana kwa jinsi ilivyo tena hizi sheria ndogo ndogo wakati mwingine zinatungwa na kutumika kabla hazijaingia katika Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaungana na Waheshimiwa Wabunge kwamba ipo haja ya kubadilisha sheria na kulitizama jambo hilo upya ili sheria hizi ambazo zimegeuka kuwa kero kwa wananchi ziwe zimepitia katika Bunge lako tukufu. Bunge lako tukufu halina nafasi ya kulalamika wala Serikali haina nafasi ya kulalamika. Mimi siamini katika kiongozi anayepewa dhamana au mamlaka yoyote inayopewa dhamana badala ya kukalia kile kiti walichopewa na kujaa, unakaa upande mmoja kama una jipu. Ni vizuri siku zote unapopewa dhamana ukajaa katika kiti chako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na Bunge lako tukufu halina nafasi ya kulalamika kwa sababu kwanza linaongozwa na Spika mahiri, makini, mwanasheria aliyebobea, kiongozi madhubuti na ni kijana ambaye bado akili yake iko vizuri zaidi. Pia ana Wenyeviti wasaidizi na Naibu Spika wa viwango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme hivi kwa sababu mamlaka ya kuisimamia na kuishauri Serikali ni ya kwetu kwa mujibu wa Katiba. Lakini Ibara ya 151(1) inaweka tafsiri bayana ya mamlaka ya nchi kwamba ni pamoja na Serikali na Bunge sisi tumetajwa bayana, Mahakama haikutajwa kinagaubaga katika Ibara ya 151 katika tafsiri ya mamlaka ya nchi. Kwa hiyo, sisi ni mamlaka ya nchi pamoja na executive. Sisi katika Ibara ya 63 tumepewa mamlaka ya kuisimamia na kuishauri Serikali ikiwa sisi ndio chombo kikuu kwa mujibu wa Katiba kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siamini katika Bunge ambalo linaona kuna tatizo pale mbele, tunashauri kupitia Kamati za Kudumu za Bunge, tunashauri kapitia Bunge, bado zipo taasisi na maafisa wa umma ambao wanaelekezwa kubadili sheria zinazokinzana na sheria za Bunge, wanaelekezwa kubadilisha sheria zinazokinzana na Katiba ambazo ni batili moja kwa moja kwa mujibu wa Katiba bado wanaendelea kunyamaza na kupuuza maelekezo ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kabisa kwamba siku 30 zilizotolewa na siku 60 zilizopendekezwa na Kamati tutaziheshimu na kuziunga mkono kupitisha maazimio hayo leo na baada ya hizo siku 60 ninaamini kabisa na wale waliopewa siku 30 watarekebisha madhaifu yaliyoonekana na Kamati zetu mbili za kudumu ambazo zimeshughulikia na hasa Kamati inayoshughulikia sheria ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kwamba Bunge hili ni Bunge madhubuti na kwa kweli halipaswi kulalamika. Miaka ya 1990 Bunge hili hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipokuwa imekuja na hoja ya Tanganyika ya G55 ambayo ilikuwa ni kinyume na sera za CCM, kinyume na Article of Union, lakini bado ndani ya muda mfupi wana-CCM walisimama na Wabunge walisimama wakakataa na Mkutano Mkuu wa Chimwaga ulikataa, lakini baadaye wakarudi tena na kuleta hoja hiyo kutokana na hasira walizokuwa nazo na kutaka kutuingiza katika muundo wa Serikali tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema hasira zenu zisielekezwe kwenye kutuundia jambo linalokinzana na sera, jambo linalokinzana na Article of Union ambayo ndio msingi wa Muungano wa nchi zetu mbili na Mwalimu alitumia maneno haya yafuatayo na mimi naomba niyanukuu katika kitabu cha Mwalimu cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania na hili nalisema kwa taasisi hii na nalisema kwa taasisi zingine zote naomba kunukuu; “Kukubali kufanywa vikaragosi vya viongozi ni dalili ya woga, si dalili ya heshima na woga na heshima ni vitu viwili mbalimbali. Maadili mema hayatudai tuwaogope viongozi wetu na viongozi makini hupenda kupata heshima ya wananchi wenzao, lakini hawapendi kuogopwa. Kuogopwa ni sifa na ada ya madikteta. Viongozi halisi hawapendi kuishiriki, kujenga mazoea ya kutii viongozi hata katika mambo haramu ni dalili ya woga ni kukaribisha udikteta.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayatumia maneno haya kwa sababu sifurahii kuona Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania likilalamika juu ya maamuzi ambayo mlikwishayafanya. Ningependa tutoke na maazimio kwamba wale walioagizwa wayafanye tuwajue ni akina nani walipaswa kusimamia katika sekta hizo na Bunge hili lielezwe ni nani hao wanaokaidi.

Kwa hiyo, sisi tuko hapa kwa niaba ya wananchi tuchukue hatua, kama hatuna mamlaka ya kuchukua hatua dhidi ya Waziri mmoja mmoja, dhidi ya mtendaji mmoja mmoja, tuchukue hatua kwa wale ambao tuna mamlaka nao ili wawasimamie hao ambao wamepewa dhamana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Edward Olelekaita, Mbunge wa Kiteto alibainisha juu ya dhahama wanazozipata wafugaji sasa kutokana na tafsiri ambazo hazijakaa vizuri. Nchi yetu au Bunge letu lipitie Sheria Namba 5 ya Uhifadhi ya Wanyamapori ya mwaka 2009 na marekebisho mengine ya mwaka 2022, yapo maeneo ambayo kwa mujibu wa sheria iliyokuwepo hayakuwa yanatajwa kama ni maeneo ya uhifadhi, lakini kwa sheria ya sasa ni maeneo yaliyohifadhiwa, ni ardhi ya hifadhi. Lakini unakuja kuhifadhi wakati tayari kuna binadamu walioko pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Ardhi, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali tukae pamoja kwa sababu ulindaji, uhifadhi na uendelezaji wa rasilimali za nchi ni jukumu la kila raia wa nchi hii, ni jukumu la kila Mbunge aliyeko katika ukumbi huu, ni jukumu la kila kiongozi. Tukae ili pale ambapo ardhi za vijiji ambazo sasa mnataka kufanya kwa Wildlife Migratory Route, Wildlife Dispersal Area, Breeding Areas mnataka kufanya kuwa Game Controlled Area, katika maeneo ambayo yako kwenye ardhi za vijiji hakuna namna unaweza kuichukua ardhi ya kijiji ambayo imekataliwa na sheria ukaifanya kuwa Game Controlled Area.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiacha hii kwa sababu yako mazungumzo na malalamiko niliyowasilisha nikiamini nitakaa na viongozi wenzangu tuyafikie mwisho, lakini kikubwa ninachosema hamuwezi kuendelea kutoza ng’ombe faini ya shilingi 100,000 badala ya ku-compound kama sheria inavyosema katika kifungu cha Sheria ya TANAPA (National Parks) kifungu cha 20A imeweka bayana kabisa juu ya ku- compound lile kosa na kwa yule muhusika ndio anayepigwa faini, ng’ombe hawezi kupigwa faini, anapigwa mmiliki wa ng’ombe.

Kwa hiyo. rai yangu ni vizuri tukazingatia ushauri uliotolewa na Wabunge ili kuepusha adha hii ya kuwatoza wananchi ada zisizokuwa na sababu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sisi sote ni mashahidi juu ya hukumu ya Mheshimiwa Elenina ambaye alimaliza kesi yake mwaka 2018 na akashinda, yule mfugaji ambaye amefilisiwa na mnamwona kwenye mitandao ambaye ameshinda kesi yake Mahakama Kuu. Bado DPP aliweza kung’ang’ania wale ng’ombe kwamba akate rufaa abaki na ng’ombe. Jaji wa Mahakama Kuu Jaji Kalombola alikataa na baada ya kukataa bado walikaidi na wale ng’ombe wamekufa na yule mfugaji alikuja kupewa ng’ombe 90 kati ya ng’ombe 265 ambao walikaa nao kwa muda wa miaka mitatu. Ng’ombe 265 wakizaa kila mwaka kwa miaka mitatu ni ng’ombe wangapi?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja, nakushukuru kwa kunipa nafasi hiyo, na kwa kweli naishauri Serikali iendelee kuwa sikivu katika eneo hilo, nakushukuru sana. (Makofi)