Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi kuweza kunipa fursa ya kuwa mchangiaji siku hii ya leo. Mchango wangu mimi nitauelekeza zaidi katika kuangalia utekelezaji wa Maazimio ya Bunge yaliyotolewa wakati wa Mkutano wa Tano, Sita na Mkutano wa Saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ieleweke ya kwamba Bunge ndicho chombo kinachohusika katika utaratibu wa kutunga sheria za nchi hii. Ila, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, kipengele namba 97 (5), sambamba na Sheria ya Tafsiri ya Sheria (The Interpretation of Law Act) Bunge hili limepewa mamlaka ya kukasimu mamlaka yake kwa taasisi nyingine za Serikali ili kuweza kutunga sheria. Kwa hiyo ni wajibu wa Bunge kuhakikisha mamlaka ilizozikasimu kwa idara au taasisi nyingine zinatumia mamlaka hayo kama inavyostahili. Ili kutimiza wajibu huo, ni jukumu la Bunge kufuatilia kwa karibu namna taasisi au Wizara hizo zinavyotumia mamlaka hayo. Kwa maana ya kwamba au kwa maneno mengine ni kwamba Bunge haliishii katika kuainisha au kubainisha tu dosari zilizotekea katika kanuni au sheria kwa njia ya maazimio, isipokuwa linatakiwa lifuatilie kwa karibu namna maazimio hayo yalovyoenda kutekelezwa na Wizara husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Kamati tulijaribu kufanya ufuatiliaji wa karibu sana wa Maazimio ya Bunge. Ni ukweli kabisa usiopingika kwamba tuliweza kubaini mambo mengi mno. Kuna Wizara ambazo zimeweza kukamilisha utaratibu mzima wa kutekeleza Maazimio ya Bunge yaliyotolewa. Nisingependa nizizungumzie Wizara hizo kwa sababu hizo zimetekeleza wajibu na taratibu zilizowekwa na Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna Wizara nyingine ambazo zimejaribu kutekeleza Maazimio ya Bunge kwa kiwango fulani; kwa maana ya kwamba wapo katika michakato hawajakamilisha utekelezaji wote. Ila, cha kusikitisha ni kwamba muda tuliotoa, kwa sababu tuzingatie sheria hizo ziliwasilishwa hapa na maazimio hayo yalitolewa hapa tangu wakati wa Mkutano wa Tano na wa Sita maana yake ni muda mrefu. Kutokukamilisha kwao kwa utekelezaji wa Maazimio ya Bunge maana yake nini, sheria zile bado zinaendelea kuwakandamiza wananchi kule chini. Wananchi bado wanaendelea kulalamika. Tunawaomba waweze kukamilisha jitihada zile za ukamilishaji wa Maazimio ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo linalohuzunisha zaidi ni kundi la tatu. Kamati ya Sheria Ndogo katika ufuatiliaji wa Maazimio ya Bunge ilibaini wazi kwamba zipo Wizara ambazo hazijatekeleza hata kwa kiwango chochote Maazimio ya Bunge hili. Ni jambo ambalo linasikitisha sana. Masuala tumeweza kuyapitisha katika Bunge hili, yakajadiliwa katika Bunge hili, sote kwa umoja wetu tuliokuwepo hapa tukatoka na azimio moja. Leo hii unaita Wizara mbele ya Kamati kujibu kwanini wameshindwa kutekeleza azimio hili, wanakwambia kwamba Bunge wakati linaazimia halikuwa sahihi na usahihi wake badala ya kukaa sisi tuliona upo hivi; kitu ambacho kilitakiwa kifanyike hata kabla ya kuletwa kama azimio; kwa sababu kabla ya kuletwa azimio tunakutana na Wizara, tunakutana na Serikali kujadiliana, tunakutana nao kubadilishana nao mawazo, tunaleta hapa kama ni azimio. Inakuwaje yale tunayo yaazimia Bunge bado yaendelee kuwa na mjadala kwa Wizara za Serikali? Hii inasikitisha sana na inawezekana Serikali inafanya hivi kwa kuwa katika kanuni zetu za kudumu za Bunge wanajihisi pengine hatuna kipengele cha kuweza kuwaadhibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine kama maamuzi ama Maazimio ya Bunge hayakutekelezwa, inawezekana kanuni zetu zipo wazi, hazisemi kitu gani kitafuta kwa Waziri au kwa Wizara ambayo haikutekeleza Maazimio ya Bunge. Labda tubadilike na tuige kwa wenzetu. Wenzetu wao wana utaratibu kwamba kama maazimio yaliyotolewa na Bunge kwa Wizara fulani na Wizara badala yake haikutekeleza maazimio hayo basi bajeti yao haiwezi ikajadiliwa mpaka waende wakakamilishe. Labda tuende katika mfumo huo. Kwa sababu chombo hiki kieleweke ni chombo ambacho kina ukubwa wa aina yake, ni chombo ambacho kina umuhimu wa aina yake na kina hadhi na heshima, sawa sawa na Mihimili mingine ya dola. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifurahishwa sana juzi na kauli ya kaka yangu Mwiguli Nchemba. Kusema kweli alinifurahisha sana aliposema kwamba chombo hiki akiwa anaashiria Bunge, chombo hiki kina nafasi kubwa sana. Hakina jukumu la kujadili matukio tu, lakini kina wajibu wa kuishauri Serikali namna gani ya kuweka utaratibu wa kuhakikisha Watanzania wanaondokana na umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana nisieleweke nini ninamaanisha, lakini kiukweli kabisa duniani kote sababu kubwa ya umaskini inaanza na kuwa na kanuni na sheria mbovu. Yule tunayemwita maskini, maana yake ni maskini kwa mujibu wa sheria, yule tunayemwita tajiri, huyo ni tajiri kwa mujibu wa sheria. Tanzania tumekuwa na maskini wengi kwa sababu tumekuwa na kanuni nyingi na sheria nyingi ambazo zinahubiri zaidi umaskini kuliko utajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutakuwa na utaratibu wa kuendelea kutunga sheria ambazo zaidi zinaenda kuwakandamiza watu wa tabaka la chini, tukitunga sheria za ku-deal zaidi na masuala ya mafungu ya mihogo, basi tusitarajie kwamba lengo na dhamira ya Serikali ina uwezo wa kufikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa Bunge kazi yake kubwa ni kutunga sheria na kuzipa mamlaka nyingine kukasimu madaraka hayo, na tumekasimu madaraka kwa halmashauri zitunge sheria lakini halmashauri zinatunga sheria kinyume na taratibu. Ieleweke kwa mujibu wa taratibu za kisheria yeyote anayetoa mamlaka ya kufanyika jambo fulani basi jambo hilo likifanyika inahesabika sawa sawa limefanywa na aliyetoa mamlaka hayo. Bunge limetoa mamlaka kwa halmashauri kutunga sheria, halmashauri zimetunga kanuni mbovu, maana yake Bunge limehusika katika kanuni hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msisitizo wangu kwa upande wa Serikali, nashauri tuzidishe umakini kwa taasisi zetu, kwa Wizara zetu, wakati ambapo tunaenda kutekeleza Maazimio ya Bunge; lakini vile tuzidishe umakini wakati ambapo tunakaa na kutengeneza sheria mpya. Kwa sababu sheria ndogo hizi za halmashauri ndizo automatically, directly zinaenda kugusa maisha ya Watanzania… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)