Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Naghenjwa Livingstone Kaboyoka

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuhitimisha hoja yetu ya PAC. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchangia hoja ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na kutambua maelezo ya Serikali kuhusu hoja mbalimbali za Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya Waheshimiwa Wabunge waliochangia ni saba na maeneo waliyowekea msisitizo na Wajumbe ni kama ifuatavyo: -

(a) Kukosekana kwa thamani ya fedha (value for money) katika baadhi ya miradi ya maendeleo;

(b) Upotevu wa fedha za umma zinazolipwa katika riba kwa wakandarasi;

(c) Ukiukwaji wa Sheria ya manunuzi na kanuni zake na kanuni zake katika utekelezaji wa baadhi ya miradi;

(d) Kuongezeka kwa gharama za utekelezaji katika baadhi ya miradi, (variations).

(e) Kutofanyika kwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kabla ya kutekeleza kwa baadhi ya miradi;

(f) Kukosekana kwa master plan katika utekelezaji wa miradi ya maji nchini na dosari katika usimamizi wa mikataba;

(g) Uwepo wa mwingiliano wa majukumu baina ya taasisi ya Serikali kama vile TAA na TANROADS.

(h) Mifuko ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kutofikia malengo ya uwanzishwaji wake kutokana na fedha kupelekwa kwa watu ambao sio walengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati inaendelea kusisitiza Serikali kutekeleza kikamilifu mapendekezo yote ya CAG na Kamati. Aidha, katika kipindi cha kila robo mwaka sekta husika zilizokaguliwa ziwasilishe kwa CAG taarifa ya utekelezaji wa mapendekezo ya ukaguzi ambapo itafanyiwa uhakiki na kisha kuwasilishwa Bungeni kupitia kwenye Kamati kwa ajili ya ufuatiliaji na tathmini ya mwendelezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yetu sisi Kamati kwamba Serikali itatimiza wajibu wake ili kuongeza uwajibikaji katika fedha za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijahitimisha hoja yangu. Nieleze kutoridhika na majibu ya Waziri wa Fedha aliyoyatoa. Kwa kweli mifano aliyoitoa inanipa wasiwasi na nafikiri inaipa wasiwasi na Bunge hili kwamba Serikali itakuwa tayari kusimamia fedha za umma inavyotakiwa. Hakuna justification; upeleke fedha nyingi kwenye miradi ambayo huwezi kui-monitor na ambayo huwezi kujua kwamba certificate hii inatakiwa ilipwe kipindi hiki, kwa hiyo, lazima ilipwe kwa wakati. Uko tayari fedha za mikopo upeleke fedha nyingi na riba ziwe kubwa kuliko hata mradi wenyewe. Hiyo, nafikiri Bunge halitakubaliana na maelezo ya Mheshimiwa Waziri wa fedha. Tunaomba aende akasimamie kikamilifu ulipaji wa hizi certificate. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii kusema fedha zimepelekwa nyingi, na mifano ya kwamba tutajazana wote tukiambiwa tutoke kwenye mlango huo, hakuna fedha ya Serikali inaweza kutolewa kwa emergence namna hiyo, kwamba iende tu, halafu isiangaliwe itatumikaje; halafu izuie kwamba zile certificate ambazo zimefikia wakati wake zisilipwe kwa wakati maana kuna hela nyingi bado zinashughulikiwa huku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kwa mawazo hayo, nina wasi wasi sana kwamba hata hizi fedha ambazo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anazozileta, kama mtazamo ndiyo huo, hatuna imani kwamba kweli fedha hizo zitatutumika kwa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, licha tu ya kulipa riba kubwa ambayo mkiangalia ni mabilioni ya fedha, matrilioni ya fedha, bado miradi ile haitekelezwi kwa wakati. Sasa kama haitekelezwi kwa wakati tunafanya nini? Ina maana fedha ya mlipa kodi, fedha ya mkulima huyu tulikuwa tunamsemea hapa, ambapo hata kule kwetu kwenye Jimbo la Same Mashariki, Tangawizi iliyokuwa inauzwa kilo shilingi 1,000, au shilingi 2,000, sasa hivi inauzwa kilo shilingi 400 kutokana na changamoto mbalimbali. Sasa uniambie kwamba walipa kodi hao wanaohangaika, wananchi fedha zinaletwa za mikopo nyingi, halafu uambiwe kwa vile zimepelekwa nyingi lazima ucheleshwaji utatokea! Hakuna kitu kama hicho!

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hela ni nyingi lazima iwe na mpangilio, ina maana gani ukakope hela nyingi ambayo hakutakuwa na uwajibikaji? naomba nitahadharishe hilo, nimshukuru sana Mheshimiwa Simbachawene kwa maelezo yake ambayo yametia moyo kidogo, kwamba kwa kweli Serikali itasimamia hayo yote, na tunasema kwamba kunapokuwa na exit meetings za CAG hatuwezi kukaa tena hapa tukaambiwa longolongo zile kwamba hapa ilikuwa hivi hapa ilikuwa hivi, hapa siyo mahali pa ku-justify uzembe ni mahali pa kuwajibisha watendaji wazembe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Mheshimiwa Simbachawene nimefurahishwa na majibu yako ya kuonesha ukomavu na kuonesha kwamba kweli utasimamia Serikali ipasavyo kuhakikisha kwamba inatumia fedha za umma vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja kwamba sasa Bunge hili likubali maoni na mapendekezo yaliyotolewa na Kamati yetu hii ya PAC yawe maazimio ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.