Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. JERRY W. SILAA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa kuja kuhitimisha hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua fursa hii kuwapongeza sana wachangiaji wote waliochangia hoja zote tatu mezani. Tumetambua wachangiaji 24 ambao waamechangia kwenye maeneo mbalimbali ya hoja hizi tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati hii ni mtambuka. Katika wachangiaji waliochangia zipo taaisi zimetajwa ambazo zinasimamiwa na Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma. Taasisi hizo ni Mamlaka ya Viwanja vya ndege (TAA), Mamlaka ya barabara kwa maana ya TANROADS, TANAPA, TAMESA, Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF), Kiwanda cha Ngozi Kilimanjaro (KLICL), Mamlaka ya Bandari (TPA), Mamlaka ya Mapato (TRA) na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya wachangiaji wamezungumzia suala la uhamishaji wa Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja vya Ndege toka TANROAD kwenda TAA. Naomba nilikumbushe Bunge lako Tukufu kwamba katika kikao chake cha tarehe 4 Novemba, 2022, katika Mkutano wake wa Tisa, Bunge lilikuwa na Azimio mbalo lilitokana na Mapendekezo ya Kamati yetu Na. 9, kwamba Serikali ihamishie Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja vya Ndege kutoka TANROAD Kwenda TAA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuthibitishie, kama alivyosema Naibu Waziri wa Ujenzi, tayari Serikali imeanza mchakato wa kuhamishia na wameleta utekelezaji wa azimio hili kwenye kamati na utekelezaji wake unaridhisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kwa kifupi maeneo Matano. Eneo la kwanza ni Mfuko Maalum wa Uwekezaji (Investment Fund). Kamati imeleta pendekezo la kuiomba Serikali ianzishe mfuko huu ili kusaidia mashirika na taasisi yenye kuhitaji fedha za uwekezaji kuweza kupata fedha kwa urahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya, ipo Bodi ya Mazao Mchanganyiko (CPB) chini ya Wizara ya Kilimo. Bodi hii ikiwezeshwa fedha za kutosha ina uwezo wa kununua mazao, kwa maana ya mazao ya nafaka na inaweza ikasaidia huko mbele ya safari hata hili tatizo ambalo Waheshimiwa Wabunge leo wamesema la mfumuko wa bei.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaamini kama Bunge lako litapitisha azimio hili, basi Investment Fund hii itasaidia siyo tu taasisi za kiuwekezaji za biashara, bali hata taasisi kama CBP ambayo inaweza ikasaidia kwenye mifumuko ya bei ya chakula nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni eneo la Mifumo ya TEHAMA. Namshukuru sana Mheshimiwa Simbachawene, amemnukuu Mheshimiwa Rais katika kikao chake cha tarehe 28 Machi, 2021 akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Hata hivyo, pale alipoishia kunukuu, yapo maneno ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anasema, “kama mifumo imewashinda, basi ombeni misaada kwa wataalamu.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili la mifumo limesemwa hapa na Wabunge wengi, na maelezo yake ukitoa majibu yake hapa, hakuna anayeelewa. Ipo mifumo mingi ambayo haieleweki. Leo wafanyabiashara ikifika muda wanaweka return zao TRA, mfumo uko down. Yaani mtu anataka kulipa kodi, anaambiwa mfumo uko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumezungumzia Mamlaka ya Bandari (TPA). Pale TRA wana mfumo wao wa TANCIS wa kulipa custom duty; huku bandarini nao wana mfumo wao wa cargo system. Ukishalipa kodi, uende bandarini na wakati mwingine kodi mfumo uko chini. Ukienda bandarini wanaku- charge storage. Kule bandarini nako, ingawa wanaweza kuingia kwenye TANCIS na kwenyewe kuna matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Mheshimiwa Rais anasema, siyo lazima kila jambo ujidai wewe Masoud Mwamba unaliweza. Kama limewashinda, tafuteni wataalamu waliobobea kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi tukizungumzia mifumo, tunatoa mifano. Sisi wote hapa tuna simu za mikononi, na wote hapa tukifanya miamala ya simu za mikononi, hakuna siku muamala unazidiwa, hakuna siku unatuma pesa ambayo hauna; hakuna siku unadhulumu muamala unaenda kushughulikia mahali unaambiwa jambo limeshindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mifumo ya kitaalamu ikijengwa vizuri; ndiyo maana Kamati inashauri Bunge kwamba uanzishwe mfumo wa single integrated information management system and network ambao utajumuisha mambo yote haya. Ukisikia mtu ana NIDA basi itambulike maeneo yote. Sio mtu wa Halmashauri hii anakopa, halafu anaenda Halmashauri nyingine; au unasikia kuna POS Halmashauri, mtu anaingiza anachokitaka yeye. Leo kuna Halmashauri fedha hazionekani, nyingine zinakusanywa haziendi Benki halafu unaambiwa huo ni mfumo. Hakuna mfumo wenye tabia kama hizo. Hicho ni kitu kingine, labda kitafutiwe jina lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaipongeza Serikali na Mheshimiwa Simbachawene kwa kauli hiyo aliyoisema ya Mheshimiwa Rais. Tunaiomba Serikali iende ikawe serious kwenye mifumo ili Watanzania hawa, watu wanaotumia bandari yetu waweze ku-clear mIzigo yao wakiwa Congo. Unaweza ku-trace mzigo kuanzia Congo mpaka unafika Bandari ya Dar es Salaam, lakini ukifika pale ni nenda rudi, mfumo uko chini, baadaye unachelewa kulipa kodi, ukilipa kodi, unakuwa charged kwenye storage, mwisho wa siku bandari inakosa wateja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni la utalii. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa sana kwenye eneo hili. Filamu yake ya Royal Tour imeongeza watalii kwa kiasi kikubwa. Leo Ngorongoro mpaka kufikia Desemba wamekusanya zaidi ya shilingi bilioni 98. Leo TANAPA mpaka kufikia Januari 23, wamekuja kwenye Kamati wamekusanya shilingi bilioni 233. Tunategemea hawa kufikia mwezi Juni mwaka huu 2023 watakuwa wamevunja rekodi ya ukusanyaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nenda huko Ngorongoro, pita hiyo barabara, ukienda likizo Serengeti kupumzika na mkeo, zile rasta utakazopiga njia nzima mpaka ufike hotelini, hata hiyo sababu yenyewe ya kwenda kufanya na mkeo inaweza ikakushinda kwenye kufanya huko. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ngorongoro waliomba Shilingi bilioni 160 tu kujenga barabara inayoendana na mazingira, na walipata kibali UNESCO, mpaka leo hawajapewa fedha hizo. TANAPA walikuwa na hifadhi 16 zenye jumla ya Kilomita za mraba 57,000, wameongezewa hifadhi sita zenye jumla ya Kilomita za mraba 47,000, karibia mara mbili ya eneo lao. Fedha za maendeleo ni hizo hizo, fedha za matumizi ya kawaida ni hizo hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiendelea hivyo, alisema mchangiaji mmoja hapa, fedha za utalii ni Non-Tax Revenue. Ni pesa ambazo tunazipata kwa kile ambacho Mwenyezi Mungu alitujalia kama Rasilimali zetu. Tukiwekeza vizuri TANAPA, Ngorongoro na TAWA, tutapata mapato makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa watalii 1,500,000 tunaozungumzia ni wale tu wenye kiu ya kwenda kuona The Eighth Wonder of the World, Serengeti. Akifika pale, zile rasta atakazopiga saa ya kwenda na kurudi, harudi tena. Kwa hiyo, tunaomba sana Bunge lako Tukufu lipitishe azimio na TANAPA itengewe fedha za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, ule utaratibu wa kukusanya fedha kupitia TRA siyo mbaya, lakini utengenezwe utaratibu mzuri wa Revenue Disbursement Automated System wa kurejesha fedha kwa wakati. Wanakusanya fedha nyingi, wanaomba pesa za maendeleo, mtu akae Hazina apeleke kwa muda anaotaka yeye. Kuhusu mifumo ameleezea vizuri sana kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwamba wakati mwingine inakuwa na first track na mambo mengine mengi ya miradi mikubwa ambayo yanafanya fedha zisiende kwa wakati. Kwa hiyo, tunaliomba sana Bunge lako liazimie fedha ziende kwa wakati. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la nne, ni deni la Pamba. Tunaishukuru Serikali imeonesha jitihada kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tano na la mwisho, ni sheria ambazo zimepitwa na wakati, alisema Mheshimiwa Dkt. Kikoyo kuhusu Sheria ya TR, Sheria ya TBS, Sheria ya TRA ya Stamp Duty, tunaiomba Serikali iharakishe mchakato ilete sheria hizi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba kutoa hoja.

MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.