Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja zetu zilizoko mezani. Awali ya yote nikiri kwamba tumepokea maeneo ambayo yanahusu ushauri, tutayafanyia kazi ili kuweza kuboresha kama Waheshimiwa Wabunge walivyoshauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hoja zilizojitokeza nifafanue hoja mbili/tatu. Hoja ya kwanza, limejitokeza jambo la Taarifa ya CAG.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri sana kwenye hili pia tukazingatia taratibu zinazotumika. Utaratibu unaotumika ambao tulijiwekea wenyewe kwenye sheria ni kwamba baada ya CAG kufanya ukaguzi wake, cha kwanza anachotoa ni hii taarifa yake, na baada ya hapo kutakuwepo na utaratibu wa Serikali kujibu. Lakini kwa taratibu zilivyo akishatoa taarifa ile Waziri wa Fedha anaipeleka Bungeni. Sasa zikishapita taratibu hizo itachambuliwa, ikiwa kwenye hatua za kwanza inapokuwa imekamilika kunakuwepo na hoja za ukaguzi na baada ya uchambuzi kutakuwepo na wizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa hoja za kiukaguzi kuna vitu vingine vinakuwa vya kiuhasibu. Hata hapa tu sasa hivi ukituuliza tutoe risiti mara moja kwa watu wengi namna hii, tutoe risiti mara moja ya mafuta ya kujia hapa, hauwezi ukapata risiti hizo kwa mara moja. Kwa hiyo, aliyekagua mara ya kwanza anaweza akaona risiti aliyotumia Mheshimiwa Dotto haipo. Huu hautakuwa wizi mpaka pale ambapo itajulikana kwamba Mheshimiwa Dotto hakwenda Dodoma lakini mafuta yake yametoka. Kwa hiyo, kunakuwepo na hoja za ukaguzi ambazo Serikali itafanya reconciliation, ikishafanya reconciliation hatua inayofuata tunabainisha yale ambayo yanahusu criminality, yale ambayo ni ya wizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na utakumbuka kauli ya Mheshimiwa Rais; mara ya kwanza tu alipokuwa anapokea Ripoti ya CAG, alimwambia CAG usipepese macho, usifanye kuficha. Kauli ya aina hiyo ni mwongozo mkubwa ambao Waheshimiwa Wabunge hampaswi kutilia shaka utayari wa Serikali kuchukulia hatua masuala yanayohusu rasilimali za nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, sisi tumepokea taarifa ya CAG kama Serikali na hatua zinazofuata itafuata taratibu hizo za kiutawala bora kama inavyotaka, kukagua wapi pana hoja ya kiuhasibu na wapi pana upotevu. Pale ambapo pana upotevu hatua stahiki zitachukuliwa, wale waliohusika watafika kwenye mkono wa sheria na watawajibika kwa makosa ambayo wameyafanya.

Kwa hiyo, kwenu ninyi Waheshimiwa Wabunge tumepokea maelekezo yenu na Serikali itachukua hatua kwa yote yale ambayo yanahitaji hatua za kisheria kuchukuliwa; na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI ameongelea kwa upande wa TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, na si tu taarifa ya CAG, makosa yote yanayohusisha ukosefu wa maadili kazini yamekuwa yakichukuliwa hatua hata kabla ya Taarifa ya CAG kutolewa. Kuna watu wanafukuzwa kazi, kuna watu wanapelekwa mahakamani, kuna watu wako TAKUKURU, kuna watu wameshahukumiwa. Tuna kesi za kutosha, na ndiyo maana tukienda kwenye utawala bora tunakuwa kwenye rank za nchi ambazo zinafanya vizuri, ni kwa sababu tunafuata utaratibu wa utawala bora. Utaratibu wa utawala bora una gharama yake, gharama yake ni ufuate taratibu na wakati ule ule wakithibitika wanachukuliwa hatua. Kwa wale Wanasheria watasema kwamba ni namna gani ambavyo kwao kisheria ni kosa kubwa sana kumwonea ambaye hana hatia kuliko hata kuswaga wale ambao wana hatia ukaunganisha na wale wasio na hatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la mwisho lilikuwa linahusu suala la mfumo, Mheshimiwa Mbunge ame- generalize sana, anasema muda wote mnatudanganya, mnasema mifumo, mifumo, mifumo. Ndiyo haya ninayoyasema tuongee kama viongozi, panapokuwepo na tatizo tuliseme lile tatizo tu tusi-over generalize, unavyo-over generalize hivi tunaipaka matope nchi yetu, pia tunamvunja moyo Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge hawa wanatoka majimboni, katika kipindi ambacho fedha zimemiminika mikoani kuliko kipindi chochote ni wakati huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha zilizokwenda TARURA ni nyingi kuliko kipindi chochote tangu TARURA ianzishwe, namba hazidanganyi, ndivyo ilivyo. Ukienda kwenye Elimu hakuna mwaka tumewahi kujenga madarasa mengi kwa mpigo kuliko hii miaka miwili iliyopita, hizo ni fedha zinakwenda kwenye halmashauri zetu. Sio hivyo tu, ukienda kwenye elimu bure ambako na kwenyewe wanapokea watoto wetu, hakuna mwezi umepita kwamba fedha hazikwenda. Kwa hiyo, ikitokea mfumo umeleta hitilafu either kwenye mwezi, either kwenye halmashauri, either katika baadhi ya maeneo...

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba anavyosema Waziri wa Fedha hakuna wakati kama sasa fedha nyingi zimetengwa kwenda kwenye halmashauri. Shida kubwa iliyokuwepo kuanzia mwezi Oktoba mpaka Januari pamoja na uwepo wa hizo fedha nyingi, lakini fedha zilikuwa hazitoki. Kwa hiyo hazitoki kwa nini? Mfumo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yaani zipo nyingi na kwa kweli tunamshukuru kwa kutenga fedha hizo nyingi, lakini zilikuwa hazifanyi nini? Hazitoki, ndio shida iliyokuwepo. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri, taarifa hiyo.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge ameongea Kibunge ili na Watanzania waweze kuelewa nampongeza sana Mheshimiwa Kanyasu. Hilo likoje? Liko hivi unapokuwa na utekelezaji wa miradi mingi kwa wakati mmoja. Zimeiva certificate mathalani imeiva Busisi ina deadline, imeiva Bwawa la Mwalimu Nyerere ina deadline, imeiva ya reli lot mbili, tatu, nne, kwa utaratibu wowote ule imeangukia pamoja na mishahara, imeangukia pamoja na Deni la Taifa. Utaratibu wa malipo unaanza na first charge, baada ya hapo unaenda kwenye vyombo, baada ya hapo unaenda kwenye mikataba ambayo ukichelewa ina riba, baada ya hapo tunaendelea kutiririka na zingine, hivyo ndivyo tunavyofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwenye kipindi ambacho hutekelezi miradi mingi ni kawaida kwamba kila unachokipeleka kitakuwa kinatoka tu. Kwa mfano, sisi tu hapa tukiambiwa tutoke kwa mara moja hapa, siku zingine tunavyotoka kwa utaratibu huu mlango ni mkubwa, lakini tukiambiwa tutoke kwa mara moja hapa hatutaweza kutoka kwa wote kwa mara moja. Sio kwamba humu ndani kutakuwa hakuna watu, tupo wengi wa kutosha, lakini hatuwezi tukatoka mara moja mlango ule pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, fikirieni Mheshimiwa Rais wakati anaingia Bwawa la Mwalimu Nyerere lilikuwa kama asilimia 34, 35 au 37 Wizara ya Kisekta inaweza ikaniweka sawa, lakini ndani ya miaka miwili tumeshapiga tunaitafuta asilimia 90; hebu waniambie mtiririko wa certificates ukoje, kuna wakati certificate zinaingia kwa mara moja. Kwa mfano mwezi ule uliopita aliotolea mfano hapa, certificate ya bwawa peke yake ilikuwa dola milioni 137, dola milioni 137 kwa mradi mmoja weka Busisi, weka reli, lot moja unakuta dola milioni 49 au 50 ukiziweka zote ni dola milioni 150 haya weka ya elimu bila malipo kuanzia chekechea mpaka form six. Ukishachanganya haya yote kuanzia tarehe 20 mpaka tarehe 24 au 25 kuna mishahara, baada ya hapo kuna deni la Taifa, ndugu yangu ni lazima tu mtiririko wa malipo lazima uwe na namna ya kuwa na utaratibu kwenye miradi ile mingine midogo tofauti na utaratibu ulivyokuwa mwanzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utaratibu huo, ushahidi ndio huo sasa, hakuna mradi wowote ambao umekosa malipo, yaani hakuna mradi ambao umekwama mikubwa kwa midogo. Kwa hiyo, ule utaratibu wa mtiririko kama alivyosema Mheshimiwa Kanyasu nadhani ni vizuri kuelewa majira ya utekelezaji wa miradi na kuweza kwenda sambamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, lile lingine alilosema Mheshimiwa Mbunge kama fedha zipo toeni. Narudia tena utaratibu wa utoaji wa fedha tunautoa kwa certificate na huu utaratibu umewekwa na Bunge, hatugawanyi fedha kufuatana na bajeti kwamba kwa sababu huyu ana bajeti ya kiwango hiki tunampatia akae nazo, hapana. Tunatoa kufuatana na certificate, tunatoa kufuatana na utekelezaji wa mradi, kazi zilizofanyika. Fedha ambazo tunazitoa ifikapo muda ni mishahara, ukifika muda wa mishahara tunatoa, lakini utekelezaji wa mradi, kama mradi wa ni trilioni 20, hatutoi trilioni 20 hizo zote zisubirie utekelezaji wake, tunatoa kufuatana na certificate, kwamba wametekeleza hapa, pameshakaguliwa na pameonekana panafaa kulipwa, ndio tunalipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na miradi hii yote kama ambavyo nimekuwa nikisema na huu ni ukweli...

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Hakuna nchi inatekeleza miradi mikubwa mingi kwa wakati mmoja kama Tanzania, kwa Afrika Mashariki na SADC, hakuna mradi ambao umelala kwa sababu tumeshindwa kuulipia hivyo hivyo na kwa miradi mingineā€¦

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maelezo mazuri ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha kinachozungumzwa na Mheshimiwa Kanyasu labda pengine hakukipata vizuri. Ni kwamba kule kwenye halmashauri zetu tunakuwa na pesa na zimeshaingia kwenye vitabu vyetu, sasa certificate inaletwa, lakini pesa haitoki kwenye mfumo, ndio hilo tu labda angetusaidia kufafanua, haviingiliani kabisa taarifa za Nzega Vijijini haziwezi kuingiliana na miradi mikubwa ya kimkakati kama Daraja la Kigongo - Busisi haviwezi kuingiliana, hiyo ni project tofauti na Nzega ni project tofauti. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, mtoa ruhusa wa malipo yoyote ni Mlipaji Mkuu wa Serikali, kama hilo litaingilia katika kipindi ambacho ni cha malipo ya mishahara definitely itasubiri, kitakachokuwa kimesubirisha ndio hicho kule mfumo utakuwa down kwa sababu mlipaji mkuu haja authorize, first charge lazima itoke kwanza ndio utaratibu ulivyo. (Kicheko)