Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nishukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kujibu au kuchangia hoja hizi zilizoko mezani, na hasa hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa au LAAC.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na hoja ya kwanza, kuhusiana na kutokupeleka taarifa ya utekelezaji wa maazimio ambayo yalitolewa tarehe 04 Novemba, mwaka jana; nipende tu kusema kwamba, tayari tulishapeleka na tumewasilisha Ofisi ya Bunge na tunaamini itaweza kuwasilishwa kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge kwa mujibu wa taratibu. Kwa hiyo, kwenye hilo tulishawasilisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, kumekuwa na hoja, na hususan changamoto ya nidhamu katika ukusanyaji na utumiaji wa mapato ya Serikali katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Kwenye hili nikubali, ni kweli changamoto hii ipo. Tumekuwa tukiendelea kuchukua hatua madhubuti kuhakikisha kwamba tunafuatilia, lakini vilevile kuhakikisha kwamba fedha hizi zote zilizoko katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, zilizokusanywa, zinatumika kama ambavyo inatakiwa kwa mujibu wa kanuni na sheria zetu za matumizi ya fedha za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kuimarisha udhibiti tumeendelea kuboresha pia ofisi za wakuu wa mikoa na hasa kupitia sekretarieti za mikoa yetu kwa kupitia na kuuangalia upya muundo wa sekretarieti zetu za mikoa. Kwenye eneo hili tumeendelea kuhakikisha kwamba, tunaanzisha section ya usimamizi, ufuatiliaji na ukaguzi ambayo pamoja na mambo mengine watakuwa pia na jukumu la kuweza kusimamia, kufuatilia, lakini pia kukagua shughuli mbalimbali ambazo zinatekelezwa katika mikoa, lakini pia katika Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizoko chini ya mikoa yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa wakuu wa sections katika mikoa 22 tayari wameshapatikana, lakini vilevile tunaendelea na taratibu za kujaza wakuu wa sections katika mikoa minne katika sekretarieti za mikoa, ili kuhakikisha kwamba zinakuwa zimekamilika na wanatimiza majukumu yao ipasavyo. Si hilo tu, tumeendelea pia kuongeza fedha za matumizi mengineyo katika sekretarieti za mikoa kutoka bilioni
57.44 hadi kufikia bilioni 79.09. Lengo ni kuhakikisha kwamba tunaziwezesha sekretarieti za mikoa na wataalam wetu katika sections hizo kuhakikisha kwamba wanaweza kutekeleza majukumu yao ipasavyo likiwemo jukumu kubwa na la msingi la ufuatiliaji na usimamizi wa shughuli mbalimbali za Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja ya kaguzi mbalimbali ambazo zimefanyika kupitia kwa Mkaguzi wetu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali. Ameweza kufanya kaguzi nyingi na nitagusia tu chache kama ambavyo na wenyewe kwenye Kamati wamegusia, hasa kuhusiana na ile kaguzi maalum ya Manispaa ya Ilemela, Manispaa ya Ubungo, Kigamboni, Iringa, na nikipata muda nitaweza kugusia au kujibia chache: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipende kusema kwamba baadhi ya maeneo kweli tunakubaliananayo na tunaendelea kuchukua hatua kwa kujibia hoja hizo za ukaguzi. Nipende tu kukuhakikishia Mheshimiwa Naibu Spika na Bunge lako, kwamba tayari kama Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, tumeshaanza kuchukua hatua mbalimbali, lakini vilevile tumeiweka Manispaa ya Ilemela kwenye uangalizi wa karibu sana. Tunaendelea kuziangalia Manispaa na Halmashauri mbalimbali ikiwemo Bunda, Ilemela, Kigamboni, vilevile Halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Tanga, Mkoa wa Morogoro pamoja na nyinginezo vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja kwamba, hatua hazichukuliwi. Watu wamekuwa wakiishia tu kuhamishwa. Nipende kukuhakikishia kwamba tunaendelea na hatua mbalimbali za kinidhamu, lakini vilevile za kijinai. Kwa yale ambayo yanatakiwa kuchukuliwa hatua mbalimbali za kiutumishi tayari tumeshatoa maelekezo katika sekretarieti zetu za mikoa kupitia makatibu tawala wa mikoa kuweza kuchukua hatua. Vilevile tayari kupitia kwa Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU hatua mbalimbali pia zimeendelea kuchukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tumepata mrejesho kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU. Takribani watumishi nna wazabuni 672 wameshafanyiwa uchunguzi, lakini vilevile watumishi na wazabuni 46 kati ya hao uchunguzi wao tayari umeshakamilika kutokana na kutothibitika kwa tuhuma dhidi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile watumishi na wazabuni 53 majalada yao yako katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka, kwa sababu ndio utaratibu, kwa ajili ya kuwaombea kibali cha kuweza kuwafikisha Mahakamani kwa ajili ya mshitaka ya jinai. Pia tayari watumishi na wazabuni 51 mashauri yao yako Mahakamani tunavyoendelea hivi sasa, lakini vilevile yako mashauri yanayowahusisha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru na nipende kusema naunga mkono hoja na yote yaliyopendekezwa hapa tutayatekeleza na kuhakikisha kwamba hatua stahiki zinachukuliwa. Hatutamfumbia macho yeyote atakayetumia fedha kwa kukiuka taratibu. Nakushukuru. (Makofi)