Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi. Nataka nianze kuchangia ripoti iliyotolewa hapa na Ndugu zetu wa PAC.

Mheshimiwa Naibu Spika, msimu wa pamba wa mwaka 2019/2020 Serikali kama kawaida yake ilifanya yale ambayo yalifanywa kwenye msimu wa korosho mwaka 2019/2020. Bodi ya Pamba imekwenda kutengeneza deni la zaidi ya shilingi bilioni 102.5. Bodi ya Pamba kwa maelekezo ya Serikali ya kwamba wanunuzi wanunue tu pamba Serikali itawafidia, wanunuzi tu peke yake wanadai zaidi ya shilingi bilioni 21, lakini wazabuni wetu wa pembejeo, wazalendo, Watanzania wa ndani wanadai zaidi ya shilingi bilioni 80 na ilitamkwa la Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakumbuka hapa kwenye korosho mlivyofanya maamuzi hivyo hivyo kwamba Serikali iende ikanunue korosho kule, madeni kwenye Serikali hii bado ni makubwa. Leo PAC wamesema hapa na walitoa mapendekezo ambayo mpaka leo watu hawa hawajalipwa. Nini kinataka kutokea? Projection yako Mheshimiwa Bashe Waziri wa Kilimo ya kwamba mwaka 2025 unakwenda kuzalisha pamba tani Milioni Moja, Mheshimiwa Katani nipo hapa! Ukizalisha hata tani Laki Saba mimi na Ubunge wangu nikakae Tandahimba kule. Ukizalisha tani Laki Saba nikakae Tandahimba kule nilime korosho. Hakuna projection ya hovyo namna hii! Wazabuni hamjawalipa fedha, benki ambako mnasema kwamba agricultural input mnakopesha single digit ya asilimia tisa, mnakopesha fedha kwa zaidi ya asilimia 14. Unasema unaenda kumsaidia mkulima! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mnasimama watu hapa, mimi nashangaa mnasema mnawasemea wakulima, mnalalamika bei imepanda, bei imepanda, bei ya vyakula iliyopanda mbona mkulima wa korosho ameuza korosho shilingi 1,700 hakuna aliyemtetea hapa, sijasikia! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mkulima gani Wabunge wenzangu mnayemtetea, mnamtetea mlaji au mkulima? Hebu tujiangalie Wabunge wa Vijijini hapa. Nani anamtetea mkulima? Yupi anamtetea mkulima? Tunauza mazao bei ya chini kule ya mashambani, wanaoleta mchele Mjini hao ni wafanyabiashara tu! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mnamtetea mlaji hapa...

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa Kaka yangu Mheshimiwa Katani hapa kuwa ni kweli kwamba mkulima anatakiwa kulindwa, lakini sasa alindwe ahakikishe anauzwa kwa bei ambayo anapata faida. Nikupe tu taarifa kwamba kule kijijini kwetu Nyabiromo - Tarime debe la mahindi ni shilingi 10,000 ambalo halijakobolewa wala kusagwa, huku au ukienda mtaani au ukiuliza hapa Dodoma ni kati ya shilingi 22,000 mpaka Shilingi 28,000. Sasa huyo mkulima wa kule umemtetea vipi? Debe la mahindi ina maana kwenye kusafirisha tu ndiyo shilingi 15,000 difference?

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Katani.

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa yake inaongezea nyama kwamba kweli mkulima kule hakuna anayemtetea, ndicho anachokisema na anathibitisha kile ninachokisema, nakushukuru sana na naipokea taarifa kwamba wakulima wa nchi hakuna wanaowatetea kwa kauli ya Mbunge pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kwanza Wizara ya Fedha mpo hapa, hapa mnaposema single digit kwenye bidhaa hizi za kilimo, pembejeo na vitu vingine muende mkasimamie. Waziri wa Kilimo Bashe uende ukasimamie, hayo maporojo yako utakuwa na vision kubwa na utakuwa na mission kubwa kwa trend tunayokwenda nayo huwezi kufanikiwa nakuambia kaka yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hapa mwaka 2025 ukipata tani laki saba za pamba mimi Katani nabaki Tandahimba na Ubunge wangu nauacha huko huko, nakuhakikishia leo hapa, kwa trend hii tunayokwenda nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninyi Wabunge wenzangu mmewahi kulima kweli au ninyi mnadhani garden mzoweka nyumbani kwenu ndiyo kilimo kile? Umeweka maua kidogo na nini, mnadhani ndiyo kilimo kile? Rudini mashambani sisi tunakotoka wakulima mkajaribu kulima, mtamtetea mkulima kwa uchungu kuliko haya tunayoyafanya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Bashe hii itakwenda kukutafuna, mission na vision zako ziko vizuri sana, lakini kama hutakuwa na mkakati thabiti kwa sababu fedha huna, hapo unakaa unajitetea hela zinakuja, zinakuja ziko wapi? Wakulima watalalamika hawa! Ziko wapi? Ziko wapi zinakokuja, ziko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mnatudanganya watu wazima hapa mfumo, mfumo, miezi Sita hakuna cha mfumo hakuna cha nini! Hela hatuna, semeni! Mfumo! Mnatudanganya mfumo. Waziri hapa anafanya kazi kubwa, maminara mpaka Kilimanjaro huko, mfumo upi? Mkatudanganya mfumo! Tuambieni ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuambieni ukweli, tunataka tumsaidie Mama, kila anayesimama anaona kazi inayofanywa na Mheshimiwa Rais, lakini ninyi wasaidizi wake, fanyeni tathmini ya kina. Mimi nawaambia, fanyeni tathmini ya kina tunakwenda wapi! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mambo unapaswa umwambie mtu mdogo sana, Mheshimiwa Mwigulu Kaka yangu na rafiki yangu, umetutukana Wabunge sana. Mimi nakuambia! umetutukana Wabunge sana, unapaswa ukae, utafakari, hapa hakuna anayeweza kujadili waganga wa kienyeji hapa, hamna, hamna. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya tunayojadili ni maisha ya Watanzania na tumeletwa Bungeni tuwasaidie Watanzania, hata wananchi wa Iramba kule wanataka uwasaidie Watanzania wa Taifa hili. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Kuhusu Utaratibu.

NAIBU SPIKA: Kuhusu Utaratibu.

KUHUSU UTARATIBU

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika....

NAIBU SPIKA: Kanuni?

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Kanuni ya 71 na kama utaruhusu nisome.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maslahi ya muda ninaomba Mbunge anapochangia, Kanuni yetu inazuia kusema jambo la uwongo. Sasa Mheshimiwa Mbunge anapo-generalize kwamba mimi nimewatukana Wabunge, hiyo ni allegation kubwa sana ambayo Bunge lako haliruhusu na mimi nisingeweza kutukana Wabunge na Kiti kikiwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa heshima zote ningemuomba Mbunge anapochangia pamoja na hoja kubwa aliyokuwa anaijenga, aepuka generalization kama ambavyo amejaribu ku-twist ili kuweza kuweka uhalali wa hoja anayoiweka.

NAIBU SPIKA: Haya Kanuni zetu zinasema kabisa kuwa Kiti kitaamua kuhusu Utaratibu au kuhusu Mwongozo kujibu hapo hapo au baadae. Kwa hivyo, baadae tutakaa na wahusika wa Sekretarieti ya Bunge kutazama maneno ya Mheshimiwa Mbunge anayoyasema. Mheshimiwa Mbunge endelea. (Makofi)

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nakuambia jambo la wakulima, nikasema Wabunge wote hapa kwenye nyumba zetu tumeweka gardens, wasiwasi wangu tunadhani ndiyo ukulima wenyewe gardens zile. Umewaka palm nyumbani kwako, umeweka sijui maua ya rose, sijui umeweka vitu gani! Tujaribu hata hekari mbili, mbili kila Mbunge na tuweke azimio hapa na kila Mbunge awe na heka mbili kule anakotoka muone adha ya wakulima wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwaombe sana Wabunge wenzangu, tuweke azimio hapa kila Mbunge awe na heka mbili, maana hapa wengi tunakaa na tunazungumza hapa, tunakaa Mijini tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mkulima ambaye Dada yangu Mheshimiwa Matiko alikuwa anamsema, anazungumza kile nilichokuwa nakisema cha kuwa anapata bei ndogo na hakuna anayemsemea. Korosho hapa nimesema hapa mwaka huu, average ya korosho tuliyouza bei ya juu haizidi shilingi 2,500.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kuangalia gharama tunazozitumia na bei anayopewa mkulima, hakuna siku tumekaa mkulima amepata bei ndogo, Bunge likakaa hapa kujadili wakulima kwa nini wanapata bei ndogo. Leo walaji sisi tunaokuja kununua mchele pale Majengo Sokoni, wananunua mchele Dar es Salaam ndiyo tunakaa leo, bei imepanda, bei imepanda! Tunapotaka kumsaidia mkulima tumsemee mkulima hata pale anapouza bei ndogo ndiyo tutaonekana wazalendo wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kaka yangu Bashe nikukumbushe tena kwenye kilimo na hili nishauri sana, ile export levy tuliyoipitisha uje na mabadiliko hapa, yote irudi kwenye tasnia ya korosho, yote. Utapona, utapona! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana mmeagiza pembejeo zenye zaidi ya thamani ya Shilingi Bilioni 98, lakini kukusanya fedha zenu zote hata ukichukua na export levy zote, ukasema ulipe wazabuni, una deni la Shilingi Bilioni 10, piga hesabu zako utaona, piga hesabu zako utaona! (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)