Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. DANIEL B. SILLO – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kwa kushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuhitimisha hoja ambayo iko mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamechangia Waheshimiwa Wabunge 15 na Waheshimiwa Mawaziri watu; Mheshimiwa Waziri wa kilimo, Mheshimiwa Bashe, Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi Mheshimiwa Bashungwa pamoja Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote pamoja na Mawaziri kwa sababu wote wameunga mkono hoja. Nawapongeza na ninawashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni mengi yamechukuliwa na Serikali katika kuyafanyia kazi lakini ningependa kuongeza mambo machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, limezungumzwa sana kuhusu Deni la Serikali. Naomba niwahakikishie na niwatoe wasi wasi Waheshimiwa Wabunge kwamba, Deni la Serikali kwa Biashara zote za kimataifa liko himilivu kwa viwango vyote vya kimataifa. kwa hiyo, tusiwe na wasi wasi Deni liko salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Kamati ya Bajeti tumejiridhisha, tumepitia hii mikopo yote inayokuja na tumehakikisha kwamba hakuna kifungu chochote cha Sheria ya Mikopo, Misaada na Dhamana ya Serikali Sura ya 130 ambacho kimevunjwa. Kwa hiyo, mikopo imekopwa katika uhalali wake na iko ndani ya Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha Tano cha Sheria ya Matumizi, kinampa Mamlaka Waziri wa Fedha kukopa kiwango chochote cha Fedha ambacho kimeidhinishwa na Bunge lako Tukufu. Kwa hiyo mikopo yote imekopwa kutokana na sheria ambayo imetu-guide, Sheria ya Matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye deni hilo hilo mwezi Juni, 2022 deni lilikuwa trilioni 71.56 lakini kufika Disemba, 2022 deni lilikuwa ni shilingi trilioni 74.64, ongezeko la shilingi trilioni 3.08 ambayo ni growth rate ya asilimia 4.3.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yupo Mjumbe alichangia limekuwa kwa asilimia 12,13 lakini uhalali ni kwamba imekua kwa asilimia 4.3, kwa hiyo deni liko salama na liko himilivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu mfumuko wa bei. Kwa nchi za Afrika Mashariki, Tanzania ndiyo nchi pekee ambayo iko na asilimia tano mpaka sasa. Ukiangalia nchi kama Rwanda asilimia 23.7, Kenya asilimia 9.7 na Uganda asilimia 9. 7. Kwa hiyo sisi tuko salama kwa maana ya mfumuko wa bei pamoja na changamoto ambazo zipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna uhusiano wa moja kwa moja wa kwamba mfumuko wa bei unatokana na usimamizi mbovu wa sera za fedha pamoja na Bajeti. Kwa hiyo, naomba niwatoe wasi wasi Waheshimiwa Wabunge, kwamba nchi iko salama katika suala hili la mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka kuzungumzia ni eneo la mifumo ya TEHAMA ya kukusanyia mapato. Mifumo ya TRA tuna mifumo ya TANCIS Pamoja na Mfumo wa IDRAS. Mifumo hii haisomani na Mfumo wa TPA wala Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa hiyo niombe sana Serikali katika eneo hili, Mheshimiwa Waziri wa Fedha unanisikia, naombeni sana mkaboreshe mifumo ya ukusanyaji wa Mapato. Mifumo inapokuwa haisomi na ni ya taasisi moja ni changamoto. TRA wenyewe kuna Mfumo wa Forodha wa TANSIC lakini kuna kodi za ndani wa IDRAS hii yote yenyewe haisomani. Kuna changamoto na Mapato yanapotea. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri hili mlichukue mboreshe sana maeneo haya mifumo iweze kusomana ili tuweze kukusanya mapato yetu ya Serikali kwa ajili ya kusaidia shughuli za maendeleo pamoja na huduma za Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kuiwezesha kampuni ya Mbolea. Kampuni ya mbolea imeomba ipatiwe mtaji wa bilioni 60 ili iweze kusambaza mbolea kwa wakulima wetu. Tuiombe sana Wizara ya Kilimo kampuni hii ya mbolea muiwezeshe ili iweze kuagiza mbolea moja kwa moja kutoka kwa ma-supplier. Hivi sasa wananunua kwa mawakala kwa hiyo hawawezi kushindana na wauzaji wengine wa mbolea hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ufafanuzi kwenye huu Mkopo wa ECF ambao ni trilioni 2.4. Mkopo huu wa trilioni 2.4 si wa mwaka mmoja, huu ni mkopo wa miezi 40 kuanzia Julai, 2022 hadi Julai, 2025. Kwa mwaka wa fedha 2022/2023 na ambao tumepitisha ndani ya Bunge lako Tukufu, kwenye bajeti tumetenga shilingi bilioni 760; na mwezi Agosti, 2022 tumepokea awamu ya kwanza ya bilioni 349.8 na awamu ya pili mwaka wa fedha 2023 tutapokea mwezi machi, 2023. Kwa hiyo mkopo huu si kwamba wote umepokelewa kwa mara moja. Maana kuna Mjumbe ameongea kuwa kuna hela zinaingia nje ya bajeti, hapana. Ndani ya bajeti mwaka wa fedha 2022/2023 ni bilioni 720 na awamu ya kwanza kama nilivyosema ni bilioni 349. Niiombe tu Serikali, kule ambako mkopo umeelekezwa muweze kuusimamia vizuri hasa zile za uzalishaji. Umeenda kilimo, nishati na mifugo na uvuvi, hizi zote ni sekta za uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la mkopo huu ni katika kuboresha urali wa malipo na urali wa biashara kati ya nchi yetu na nchi nyingine hapa duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja pia nizungumze, kuhusu reallocation ndani ya mafungu na pia nje ya mafungu. Kifungu cha 41(8) cha Sheria ya Bajeti Sura ya 439 na Kanuni zake zinamtaka Waziri wa Fedha kuwasilisha taarifa ya uhamisho wa ndani (within the votes) au nje au between votes mara baada ya nusu mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilihakikishie Bunge lako Tukufu, kwamba uhamisho kwa mwaka wa fedha 2021/2022 uliwasilishwa kwenye Ofisi ya Bunge tarehe 1o Novemba, 2022. Hata hivyo, kwa nusu mwaka hii ya mwaka wa fedha ambao tunaendelea nao, wa 2022/2023, ripoti hii itawasilisha kwenye Ofisi ya Bunge Mwezi Machi 2023. Taarifa hii inapatikana kwenye ukurasa wa 72 wa taarifa ya Kamati ya Bajeti kipengele cha 7.7 na kiambatisho (B) ambacho pia kimeambatishwa kwenye taarifa yetu ya Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa pia kulizungumzia ni eneo la Sheria yetu ya Manunuzi. Sheria yetu ya manunuzi ina changamoto, wote tunakubali; kwamba Sheria yetu ya Manunuzi inachukua muda mrefu sana. Kamati ya Bajeti ilipata fursa ya kuishauri Serikali na Serikali ilikubali, kwamba sheria hii itafanyiwa marekebisho. Sasa tuiombe Serikali iwaishe muswada wa sheria katika mwaka huu wa fedha wa 2023/2024 ili Sheria ya Manunuzi tuibadilishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna miradi mingi sana, Mheshimiwa Bashe amezungumza hapa, kwa mfano kwenye Tume ya Umwagiliaji tumetengea shilingi bilioni 215 lakini utoaji wa fedha mpaka sasa ni asilimia kidogo sana. Hata hivyo ukiongea na Serikali wanasema tayari fedha ziko kwenye commitment.

Mheshimiwa Mwenyekiti, commitment hii inacheleweshwa na Sheria hii ya Manunuzi. Kwa hiyo naomba muswada huu uletwe haraka iwezekananvyo ili Sheria hii ya Manunuzi tuibadilishe. Tusiicheleweshe wenyewe, nchi hii ni yetu sote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja la mwisho, si kwa umuhimu, ni miradi ya muda mrefu; amezungumza Mheshimiwa Waziri Kiongozi Mstaafu, Mheshimiwa Shamsi Vuai Naohodha, kuhusu Miradi ya Mchuchuma na Liganga pamoja na gesi asilia. Miradi hii ikikamilika itaokoa sana fedha za kigeni tunazoagiza chuma kutoka nje pamoja na maeneo mengine. Kwa hiyo niombe sana Serikali iharakishe majadiliano ya miradi hii ili iweze kukamilika kwa wakati ili kuokoa fedha za kigeni ambazo zinatumika kuagiza chuma na bidhaa nyingine nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya ninaomba sasa Maoni, Ushauri na Mapendekezo ya Kamati ya Bajeti yawe Maazimio ya Bunge zima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. OMAR M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.