Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia. Awali ya yote nipokee maoni ambayo yametolewa na Waheshimiwa Wabunge, tumeyapokea, tutayafanyia kazi na mengine tutaendelea kupeana mrejesho kwa sababu, tukimaliza Bunge hili litakuja Bunge lingine ambalo litakuwa linahusisha bajeti, panapo Mungu akitujalia afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mambo ambayo niliona pamoja na kupokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge waliyoyatoa, ningependa nitolee ufafanuzi hoja chache. Hoja ya kwanza ambayo Waheshimiwa Wabunge wameongelea kwa sauti kubwa ni kuhusu uchache wa wafanyakazi wa Mamlaka ya Mapato (TRA). Kwanza kabisa niliombe Bunge lako tukufu liridhie tumpongeze Mheshimiwa Rais kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi wa TRA walikuwa hawajaajiriwa katika kipindi cha muda mrefu kidogo, miaka yapata mitano sita saba hivi, lakini tulipokuja kwenye mwaka wa fedha uliopita hapa Bunge lako lilielekeza Serikali kuweka uzito kwenye uajiri wa watumishi wa Mamlaka ya Mapato - TRA, hivi tunavyoongea ndani ya mwaka huu mmoja, kibali kilitolewa na Mheshimiwa Rais kuajiri watumishi kwa mpigo 2,100 wa Mamlaka ya Mapato Tanzania. Kwa taratibu za kiutumishi, sekta moja kupata watumishi 2,100 kwa mpigo siyo jambo dogo na hivi tunavyoongea 1,500 tayari walishaajiriwa na wengine 500 wako hatua za mwisho za taratibu za kiuajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii ni namna gani unaweza tukawaambia jinsi Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan inavyopokea na kuyafanyia kazi mapendekezo ya Bunge. Ni ndani ya mwaka huu wa fedha tupo nusu mwaka tu, wafanyakazi 2000 wameshaajiriwa na 170 wako hatua za mwisho kwenye taratibu za masuala ya vibali wakati wanakamilisha usaili wa hao wengine. Kwa hiyo, maoni yenu Serikali inayapokea na inayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalia kama mwaka mmoja wameajiriwa 2100 kama wangekuwa wanaajiriwa hivyo hivyo kwa miaka kumi tungekuwa na watumishi wangapi. Sasa pengo la Watumishi wa Umma wakiwa hawajaajiriwa kwa muda mrefu huwezi ukaliziba kwa mara moja, ukiajiri wengi kwa mara moja pia, kwa sababu watakuwa bado hawajazalisha utatengeneza tatizo tena kwenye upande wa mishahara, kwa sababu utakuwa umeajiri wengi ambao bado hawazalishi. Kwa hiyo, ninawaomba mridhie Serikali hatua hizi inazochukua, iwaajiri hawa waingie kazini waendelee kuzalisha, wakati huo tutakuwa tunaendelea pia kutekeleza masuala ya kimfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aliongea Mheshimiwa Esther Matiko nami nakubaliana naye, tatizo siyo watumishi peke yake, siyo idadi peke yake, tunayo maeneo mengine ambayo tunaendelea kuyafanyia kazi, masuala ya uadilifu, masuala ya matumizi ya EFD na masuala ya hamasa tu ya wananchi wenyewe kuwianisha kodi na maendeleo yao. Kwamba kila mmoja awiwe kulipa kodi anapo nunua bidhaa na anapofanya biashara nyingine yoyote ile. Kwa hiyo, hili tunaenda nalo lakini kama nilivyosema ni jambo ambalo linatakiwa liende hatua kwa hatua, niliona nilisemee hilo kwa sababu lilijitokeza lakini tunaendelea kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi ni mashahidi mtaona kwamba makusanyo yameongezeka siyo tu kwa kuwianisha malengo na makusanyo lakini hata kwa namba, Machi 2021 makusanyo ya mwezi yalikuwa trilioni 1.2 lakini Disemba hii tumepiga zaidi ya trilioni 2.7, kwa hiyo mnaweza mkaona kwamba hata kwa real terms makusanyo yameendelea kuongezeka. Niliona nilisemee hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili na ninaomba hapa tuelewane vizuri sana Waheshimiwa Wabunge, vinginevyo tutabadilisha Bunge hili kuwa platform ya kujadili matukio. Hiki chombo ni kikubwa sana siyo chombo cha kujadili matukio tu. Kinatakiwa kiishauri pia Serikali ni namna gani inaweza ikaweka mipango yake ya kuwatoa Watanzania kwenye umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini ninasema hivi, ukiangalia Hansard za Bunge letu hili, utaweza kuona michango ya Wabunge inavyokuwa tofauti Bunge moja na Bunge lingine linalofatia. Leo hii kwa sababu inasikika vizuri kwa watu ikionekana unasemea bei, kila mmoja anaongelea bei lakini twendeni katika hali ya uhalisia. Nchi hii ina wazalishaji na ina walaji lazima mara zote tukumbuke hilo. Nchi hii ina wazalishaji na walaji, na hivyo vyakula vinavyozalishwa havizalishwi kwa mashamba ya Vijiji vya Ujamaa ni watu binafsi wanaingia gharama zao kuzalisha, ni mtu binafsi anajipinda anahangaika anazalisha, kuna upande mmoja unazalisha kuna upande mmoja unatumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama watunga sera kama watunga sheria ni lazima tuwe makini sana ku-balance haya maeneo mawili. Tujiulize kwa nini nchi hii ina wakulima wengi sana halafu inakuwa ni nchi maskini na ardhi inayo! Tujiulize jibu sahihi utakalolipata ni kwa sababu wamekuwa wakizalisha wanapata hasara katika uzalishaji wao, ndiyo jibu sahihi hilo. Wanafanya kazi kwa bidii anazalisha magunia 400 anaambiwa usiuze popote halafu yanakutwa na mvua yananyeshewa yako hadharani. Wakati huo yananyeshewa yule aliyeelekeza kwamba usiuze popote hayupo kwenda kuyafidia yanakutana na mazao mengine, hii inatengeneza umaskini kwa wakulima wetu.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunachokifanya ni kipi, leo hii imetokea, mazao tunayotumia sasa hivi kama alivyosema Waziri wa Kilimo ni yale mazao ambayo uzalishaji wake mbolea ilikuwa zaidi ya shilingi 120,000. Bunge hili lilipiga kelele kubwa sana kuhusu bei ya juu sana ya mbolea mwaka jana! Haya ndiyo mazao yanayotumika sasa hivi, yamezalishwa kwa gharama za juu sana. Mafuta yalikuwa juu ilikuwa kabla ya ruzuku, mbolea ilikuwa juu ilikuwa kabla ya ruzuku, ndiyo yaliyozalishwa sasa hivi. Itakuwa ni ukatili sana kwa Serikali ukienda tu uweke maelekezo tu ya moja kwa moja kwamba wewe uza shilingi 100 debe hili hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya nini kwa kutambua hivyo? Serikali ndiyo hicho alichofanya Mheshimiwa Samia katika mwaka huu wa Fedha, katika haya mazao ambayo ndiyo tunatarajia kuyavuna, ameweka nusu bei ya mbolea kwenye kila mfuko Serikali ibebe, impunguzie gharama mzalishaji kwenye mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ikaweka ruzuku kwenye mafuta Bilioni 100 kila mwezi ili kupunguza gharama ya usafirishaji na gharama ya uzalishaji. Sasa mazao yatakayovunwa yaliyotumia ruzuku tunayatarajia yawe na bei ya chini. Hivyo ndivyo uchumi unavyopaswa kwenda lakini leo hii tukisema tu kwamba, mtu yuko pale kwenye uzalishaji anasema Serikali inajificha tu kwenye Ukraine, Sisi tumezalisha hapa hapa kwa nini bei iko juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmezalisha hapo kwenu ndiyo mmezalisha Mwanzugi lakini Mwanzugi hamtengenezi Mbolea. Mbolea mliyotumia kuzalishia ni ya bei ya juu, ndiyo hiyo iliyosababisha yale yatakayozalishwa kama mfuko ulitumia wa shilingi 140,000 au shilingi 120,000 ni lazima yale mazao hata kama umeyazalisha kijijini kwako yatakuwa ya bei ya juu. Bado usafiri, kama mafuta unayotumia kusafirisha yako juu utazalisha nyumbani kwako pale pale lakini bado yatakuwa na bei ya juu! Ndiyo maana Mheshimiwa Rais akasema tuweke ruzuku ili kupunguza pale mtu alipozalishia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu Serikali haijaishia hapo kushughulika na suala la mfumuko wa bei. Baada ya kuwa imefanya hivyo imetoa akiba yake kwenye maghala ya chakula kwenda kupeleka kwenye soko na kuwapelekea wale ambao ni kaya zenye uwezo mdogo kukabiliana na jambo la aina hii. Ni lazima tunapoelezea matatizo yaliyopo tuelezee na hatua zinazochukuliwa, tusioneshe ufahari katika kuwatajia Watanzania matatizo. Unawatajia tu bei kwamba kuna bei hii, bei hii iko juu wanazijua kila siku wananunua hivyo vitu. Taja kama unaona hatua zilizochukuliwa na Serikali hazitoshi taja za kwako mbadala kwamba Serikali iongeze hatua hii, hatua hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipokuwa makini tutafanya kila kitu kwa kuhemka, leo hii tunavyoongea ninyi Wabunge mmetoka wiki moja kule Majimboni, mkirudi wengine wanakaribia kuanza kuvuna mazao yao, sasa mnataka leo tuagize mahindi ya Pakistan, tuagize mchele wa Pakistan uje ukutane na uzalishaji wa wazalishaji wetu, Bunge lijalo usimamishe shughuli za Bunge tujadili mazao ya wakulima hayana bei yatakuwa yamekutana flooding.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara zote ukiona kelele zinapigwa kwenye haya mambo ya dharura kuwa makini sana, wakati mwingine unaweza ukabeba na deal za watu humo humo, lazima tuwalinde wakulima wetu na lazima tuwalinde walaji wetu, ni lazima tu-balance. Wananchi wengi wanaona umachinga unaweza ukalipa kuliko kilimo, kwa sababu gani? Kwa sababu tunaki-mistreat kilimo. Mimi nimekulia huko najua jinsi ilivyo kazi kulima asubuhi mpaka jioni halafu uhangaike kutunza yale mazao, halafu uvune. Lazima tuwalinde hao watu, halafu ushuhudie yananyeshewa mvua hayana pa kupeleka. Tulinganishe hata hizo bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie lingine ameongea tena Ndugu yangu na jirani yangu kwamba reserve zinashuka sana, akilinganisha kwamba mwaka juzi reserve zilikuwa Dola bilioni 6,000 sasa zimesharudi bilioni 4,500. Jamani haya masomo ya uchumi ni sayansi, narudia tena, twendeni tufuatilie kwa makini reserve zina-build vipi, reserve zinaongezeka vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilipokuwa 6,300 tulikuwa na Trilioni Moja tumeitoa IMF ndiyo ikaongeza ile reserve, sasa tumeichukua ile tumejengea madarasa yote unategemeaje reserve iwe ile ile? Iliongezeka kwa sababu tulipokea kwa mkupuo trilioni 1.3, tulipoitoa tukajengea madarasa ni kweli itashuka, sasa shida iko wapi? Haya ndiyo matatizo ya kutaka kuonea huruma mbegu, unaogopa kupanda mbegu kwa sababu ghala litapungua, panda ili uvune zaidi, ndicho tulichofanya!

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulileta kwa ajili ya madarasa na vitu vingine, baada ya hapo tumeitoa, ni kweli reserve zitashuka! Lakini siyo hilo tu, reserve pia ni function ya import na export, uwiano au mizania yetu ya importation ni kubwa kuliko exportation, sababu moja ya msingi ni kwamba tunayo miradi mikubwa kuliko nchi zote za SADC, vitendea kazi vyote tunavyojengea miradi hii tuna-import. Uki-import kilo moja ya tumbaku na vyuma vilivyoenda kujenga Bwawa la Mwalimu Nyerere mizania yake hailingani. Uki-export kilo kadhaa za mafuta ya alizeti hapa, galoni kadhaa za mafuta ya alizeti ya Singida, mizania yake na importation ya material tunayotumia kwenye reli, mizania ya reli ni kubwa, kwa maana hiyo mizania ya export na import, import ziko juu kwa sababu ya miradi mikubwa. Tuna daraja la Busisi unategemeaje reserve ziwe zile zile tu. You can’t have your cak and eat it too!

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kazi sana kutumia Bunge lako kufundisha mtu yule yule ambae ametaka kwa maksudi kutokuelewa! Haiwezekani tukawa tunatumia muda wa Bunge kujadili kitu kile kile tunataka ku-achieve kitu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna mashaka kuhusu reserve nchi yetu iko na zaidi ya miezi ya 4.7 ya importation. Wastani ni miezi Minne tu, tuko makini kwenye hilo. Hata ya Deni la Taifa tuna asilimia 73 ya mikopo yetu tangu uhuru imekopwa kwa consessional miaka 40 kipindi cha malipo na grace period miaka 10, interest rate 0.75, asilimia 73 ya mikopo ni consessional.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia hii 26 inayosalia ni commercial ambayo tumeamua kukopa kwa sababu miradi hiyo isingeungwa mkono. Jamani, tumesahau sasa hivi tu vita ya kiuchumi tumeimba muda siyo mrefu. Ulikuwa na option moja tu ama uache miradi hiyo, ama tukope commercial, tukasema tukope commercial tuweke back born ya uchumi wetu na backbone ya uchumi wetu tunao uhakika italipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna uhakika reli italipa, bwawa la Mwalimu Nyerere litalipa, sasa hapa unatishatisha watu kwa ajili ya nini? Ni wahakikishie na wala hata siyo mbaya kwa sababu hii siyo Honorary Doctorate nimeingia darasani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Samia mbinu alizochukua na vision aliyoiweka kwenye masuala ya kiuchumi siyo ya kutiliwa mashaka. Wafuatilieni wabobezi wa IMF, World Bank, wafuatilieni Wachumi wote wanao-classify kuhusu uchumi, wanasema uchumi wa Tanzania unaelekea pazuri, uko pazuri na unaelekea pazuri. Haya siyo maneno ya Mwigulu! IMF wamesema hivyo, World Bank wamesema hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuache kujidharau dharau, Watanzania tumezoea sana kujidharau. Hata juzi imetoka classification kwamba league ya Tanzania ni ya Tano, jamaa mmoja anasema haiwezekani league yetu haiwezekani league yetu ikawa ya tano. Sasa wewe unaumwa nini Tanzania ikiwa inafanya vizuri! (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, majirani wote wanasema Mheshimiwa Rais Samia unaupiga mwingi majirani wote, kote juzi tulikuwa kwenye jukwaa la uchumi la Dunia, (World Economic Forum), miadi ya watu kumuona Mheshimiwa Rais ilikuwa haina hata nafasi, wanaona uchumi wa Tanzania ulivyo imara na matarajio yake yalivyo imara. Halafu sisi kutwa tunaona hatuendi vizuri!

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutofautishe mfumuko wa bei na bei, mfumuko wa bei ambacho ndiyo Wachumi huwa wanapambana nacho kila wakati ni kiwango cha kubadilika kwa bei siyo bei! Inflation is the rate of average change of prices, not prices. Bei ni function ya cost of production na cost of transportation. Kama mtu kanenepesha ng’ombe wake kwa Milioni Moja huwezi kumwambia bei yake iwe Laki Mbili, hiyo ni kuu sekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumuko wa bei wa Tanzania siyo kama nchi zile ambazo asubuhi unabadilika, saa nne unabadilika, saa tano unabadilika, saa sita unabadilika, huo ndiyo mfumuko wa bei ambao it is a problem kwenye uchumi. Kama tatizo ni bei zinashughulikiwa kwa hatua hizi ambazo Mheshimiwa Rais amezichukua za kuongeza uzalishaji. Hatuwezi kuwa unatumia udikteta kwenye shughuli ambazo watu wamewekeza nguvu, wamewekeza fedha, wamewekeza muda. Kwa hiyo, hii hatua ambayo Mheshimiwa Rais ameIchukua actually ni long-term na itaenda kuhamisha watu kutoka mijini kwenda vijijini siyo siku nyingi. Tukifanya kilimo kikawa kinalipa tutaondoa rate hii ya unemployment na hii misongamano ya mjini lakini pia GDP itaongezeka. siyo hilo tu, per capital income itaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijasema mwenyewe tu leo, Mzee Kimei kasema, Balozi wa Kodi Mheshimiwa Subira Mgalu pia kasema, na wengine nao humu wameyaona kwa namna hiyo. Ningeshauri sana Bunge lako Tukufu liwe linatoa ushauri kwenye jambo la dharura, tulenge hilo la dharura halafu tumalize tuendelee na mambo mengine tusiwafanye wananchi wa-panic wananchi. Tunawapanikisha wananchi. Uchumi ni basi tu stock exchange hai-determine sana maisha mengine, nchi zingine ukitoa kauli moja tu unashusha uchumi chini kabisa, kwa hiyo tusiwe tunatoa toa kauli za unazuiwa hapa unapita hii, unazuiwa hapa unapita hii! Tuna-hinder investment, Rais anafanya kazi kubwa ya kuita investment sisi tumekazana kusema hii mbaya hii mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona niliseme hili kwa msisitizo kwamba unaenda vizuri, yale yaliyo maoni tumeyapokea tutayaboresha, bahati nzuri sana maoni haya mengi tunatumia tunapokea kwenye Kamati lakini pia na Bunge zima hili. Kwa hiyo, tutaendelea kuyafanyia kazi yale lakini nitahadharishe tena, tusije tukawa tunajipaka taswira ambayo hatuna. Hali ya Dunia nzima wameongea pia Wabunge wengine, ina madhara kwa namna moja ama nyingine ndiyo maana tunachukua hatua za ndani kuweza kukabiliana nayo, Mheshimiwa Rais jitihada alizofanya ndiyo zinazotofautisha na maeneo mengine, tunakoenda tutakuwa hata imara zaidi kuliko hata hivi tulivyo. Nakushukuru sana Mwenyekiti. (Makofi)