Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii ili niweze kuchangia kwa hizi Kamati zote mbili Kamati ya Bajeti na Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na nianze kwa kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati hizi kwa taarifa zao nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nivipongeze sana Vyombo vya Dola na Vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama kwa kazi nzuri sana ambavyo vinaendelea kufanya hapa nchini. Pia niwapongeze kwa hili, ajira zinazotolewa sasa hivi za Polisi, Magereza, Zimamoto pamoja na Uhamiaji ambazo zimetolewa ajira nyingi kwa wingi, vijana wetu wengi waliokosa ajira sasa watapata ajira. Kwa hiyo, tunawapongeza sana Serikali katika hili na najua sharti kubwa lilikuwa la vijana wale wa JKT na wengine wapo kwenye vikosi kule tunawatakia kila la kheri sana kwa ajili ya kwenda kulijenga Taifa lao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, naomba niunge mkono sana pendekezo la Kamati la kurejesha Tume ya Mipango ili tuwe na think tank ya Taifa katika kugakikisha kwamba mipango yetu inakuwa iko vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la ukusanyaji wa mapato, nilipokea taarifa za mapato ya TRA ya mwezi wa kumi na mbili, naamini kama sikosei takwimu zangu yalikuwa yamefikia shilingi trilioni 2.5. Nawapongeza sana kwa hatua hiyo. Moja ya sababu ilizungumzwa hapa kwamba ni baada ya wao kuwa wameajiri watumishi 1,500 wakaenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge tulishauri hapa, Serikali imeenda kutimiza. Tulihoji, kwa nini watu waliokabidhiwa jukumu kubwa la ku-service deni la Taifa, waliokabidhiwa jukumu kubwa la kulipa mishahara halafu wawe na tatizo la upungufu wa watumishi? Tunawataka sasa waendelee hivyo hivyo, hata ule ushauri uliotolewa kwamba waajiri hata vijana wa mkataba, vijana wetu wengi waliosemea kodi na pia tunao vijana wengi wa JKT kwenye vikosi vya kijeshi ambao wanaweza kuungana na hizi timu kwenda kuhakikisha maeneo yote ambao tunaweza tukapoteza mapato kwenye mipaka yetu, kwenye maeneo ya maji, bandari bubu na maeneo yote ambayo kuna ukwepaji mkubwa wa kodi, waweze kwenda kudhibiti maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu akiba ya fedha za kigeni, wenzangu wamezungumza hapa. Ukweli ni kwamba fedha za kigeni zimeshuka kutoka Shilingi milioni 5,209.8 hadi Shilingi milioni 5,110.3. Hili ni anguko la mwaka mmoja. Kama tusipoziba ufa, tutajenga ukuta. Uchumi wetu hauwezi kuimarika kama fedha za kigeni zinadondoka kwa kiwango hicho. Tutahimili vipi kulipa deni la Taifa? Tutahimili vipi kuagiza bidhaa kutoka nje? Kama unavyosikia sasa hivi wafanyabiashara wameanza kulalamika hawapati Dola; lakini tutahimili vipi uwekezaji hapa nchini? Kama mikataba mingine tumeingia ya Dola, tutahimili vipi kuweza ku-manage mikataba hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama fedha hizi za kigeni zitaendelea kupotea, maana yake Tanzanian Shilling itaendelea kupoteza thamani, itaadimika. Kama Tanzanian Shilling itaendelea kuadimika, lazima tutakuwa tumechochea mfumuko wa bei kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu zipo mbili tu katika hili eneo. Moja, usimamizi hafifu wa Sera za Fedha na Bajeti ambayo ni Monentary and Fiscal Policy lakini pia na ile Balance of Payment. Sasa tuliposema hapa, Waziri wa Fedha akazungumza kwamba labda kazi tunayoiweza ni Uganga wa Kienyeji, lakini hizi ndizo takwaimu ambazo zimezalishwa na taasisi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuchukue hizo hatua sasa za kuhakikisha kwamba tunaweka pendekezo lingine kali sana hapa kwa ajili ya ulinzi wa hizo fedha zetu za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matumizi ya Serikali nje ya bajeti, Waziri wa Fedha siku hiyo alizungumza hapa kwamba Shilingi bilioni 246 zimetumika nje ya bajeti, lakini pia ruzuku ya mafuta, Shilingi bilioni 700, hizo fedha hazimo kwenye bajeti. Pia, akazungumza kwamba Shilingi bilioni 360 alizolipwa SYMBION kama CAG alivyosema siyo hizo, lakini pia hakutaja ni shilingi ngapi yeye anazozijua? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea fedha hizi zote ambazo Serikali imetumia nje ya bajeti, ingekuwa imezipeleka kwenye Kamati ya Bajeti kwa ajili ya kwenda kuangalia uhalali wake ili Kamati ya Bajeti ikubaliane nazo na kuzipitisha, lakini sasa hivi taarifa ya Kamati ya Bajeti haya yote hayamo. Maana yake Serikali imetumia fedha nje ya bajeti kinyume cha sheria, kinyume cha utaratibu na utaratibu unaofuata pale unajulikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Kamati ya bajeti wanatakiwa watusaidie. Kwanza tuweke azimio la kuitaka Serikali ilete matumizi yote ambayo yamefanyika nje ya bajeti halafu sasa kuanzia hapo Bunge lako Tukufu hili liweze kuchukua hatua zinazostahili kwa Waziri wa Fedha aliyesabibisha mkwamo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu deni la Serikali, ukweli kabisa nilitegemea Kamati ya Bajeti wangetuondoa kwenye mkwamo huu. Tulilalamika kwamba Deni la Serikali kwanini limeongezeka kwa kasi? Swali la pili, kwanini deni la Serikali inaonekana kwamba kuna madeni ambayo Serikali imeingia zaidi ya kiwango ambacho kimeidhinishwa na Bunge? Sasa tulitegemea leo Kamati ya Bajeti wangekuja na madeni yote. Wangekuja na jedwali linaloonesha Serikali imekopa fedha kiasi gani na kwa ajili ya miradi gani katika kipindi hiki tunachokizungumza, lakini kwa ulinganifu na zile takwimu zilizowasilishwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka Aprili, 2021 mpaka Juni, 2022 ongezeko la deni la Taifa limekua kwa Shilingi trilioni 10.83, lakini kipindi cha Mei na Juni, 2021 Serikali ilikopa zaidi ya Shilingi trilioni 3.9. Katika kipindi cha mwaka 2020/2021 na 2021/2022, deni la Taifa lilikuwa linakua kwa wastani wa 4% lakini kwa sasa hivi deni la Serikali linakua katika miaka hiyo miaka miwili,...

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina, subiri taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Christopher Ole-Sendeka.

T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maelezo mazuri ya Mheshimiwa Mpina, na kwa kuwa taarifa iliyoko hapa ni ya Kamati ya Bajeti ambayo pamoja na mambo mengine inashughulikia masuala haya ya fedha; kama unavyojua Kamati yetu ilikuwa inashughulikia masuala ya Kero za Muungano na mpaka sasa taarifa yake haijawekwa hadharani na baadhi ya maeneo mengine yalikuwa yanahusiana na fedha na mpaka sasa nchi na Bunge halijatoa taarifa juu ya masuala yanayohusiana na fedha ambayo imeridhiwa katika Kamati ya Kero za Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwanini Kamati hii ambayo ingetumia fursa hii kutupa picha halisi na Serikali iweze kutupa na kanuni zinazotumika katika kugawanya fedha nyingine za Muungano katika pande zote mbili zikiwemo fedha za UVIKO ambazo tulizipata hivi karibuni tujue kanuni ambayo inatumika ili tuweze kuishauri Serikali vizuri katika masuala haya ambayo ni lazima yalindwe kwa wivu wa hali ya juu na pande zote mbili za Muungano ziweze kuridhika maana ndiyo msingi wa umoja na mshikamano wa dhati katika nchi yetu? (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina, unaipokea taarifa?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilindie muda wangu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina unaipokea taarifa au hupokei?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa. Naomba unilindie muda wangu. Nimesema deni la Taifa lilikuwa likikua kwa wastani wa 4% lakini kwa mwaka 2020/2021 na 2021/2022 sasa linakua kwa 12.33.

Mheshimiwa Mwenyekiti, deni la Taifa, Kamati imesema katika jedwali Na. 2 lililowasilishwa na Kamati ya Bajeti, ukifanya hesabu pale inaonekana kwamba Serikali imekopa zaidi ya Shilingi bilioni 322 nje ya kiwango kilichoruhusiwa na Bunge. Ukiangalia pale kwenye jedwali, ni zaidi ya Shilingi bilioni 322. Pia Serikali imeenda kukopa, iliidhinishiwa hapa na Bunge kwenda kukopa mikopo ya ndani kwa ajili ya uwekezaji wa miradi ya maendeleo Shilingi trilioni 1.84, lakini Serikali ikaenda kukopa Shilingi trilioni 2.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni zaidi ya Shilingi trilioni moja. Maamuzi hayo yanasababisha sekta zetu za fedha za ndani zisiweze kupata mikopo. Pia inachochea kuongezeka kwa riba. Kama inasababisha kuongezeka kwa riba, lazima utegemee kuna mfumuko mkubwa wa bei tunaouandaa. Ndiyo maana nasema, usimamizi hafifu wa Sera za Fedha na Bajeti (Monetary and Fiscal Policy) katika nchi yetu sasa hivi umetamalaki sana. Naamini kwamba kuna shida katika utekelezaji wa Wizara ya Fedha kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana tunaposimama hapa Bungeni na mbele ya Bunge lako Tukufu, Mbunge unaambiwa kwamba wewe hujui uchumi, Mbunge eti wewe unaweza kuchangia tu kuhusu uganga wa kienyeji na kwamba mchumi ni mmoja tu katika nchi hii. Aliyesoma uchumi ni Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba peke yake ndio anayeujua uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yanasemwa kwenye Bunge lako. Ni muhimu sana kusikiliza haya ambayo tunachangia.

Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye mfumuko wa bei...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina muda wako umeisha.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja.

MWENYEKITI: Nakuongeza dakika moja kwa ajili ya kuhitimisha hoja yako.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihitimishe dakika moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mbolea, katakata ya umeme na ruzuku ya mafuta. Maeneo haya ni nyeti sana ambayo yame-attract sana mfumuko wa bei hapa nchini. Naomba jambo moja, wafanyabiashara wetu wote ambao wanadai leo malimbikizo ya mbolea ni Shilingi ngapi? Mbolea ya ruzuku iliyosambazwa mpaka sasa hivi kwa wananchi wetu ni tani ngapi? Kwanini Serikali imeshindwa kulipa fedha hizo na kusababisha wananchi wetu waendelee kuteseka na suala la mbolea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nini kilichopelekea usumbufu mkubwa huu wa mbolea nchini ilhali Waziri wa Kilimo aliahidi hapa Bungeni kwamba he is ready to bear any cost. Akasema ruzuku inayokuja sasa hivi haitaibiwa, ruzuku inayokuja sasa hivi haitachakachuliwa, ruzuku inayokuja sasa hivi hatuwezi kuuziwa mbolea bandia, wananchi wetu mbolea yao haiwezi ikatoroshwa na wananchi watapata mbolea kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake leo wananchi wanapata mbolea kwa shida kubwa, wengine wanafia kwenye foleni, wengine wameshindwa kulima ambako tunategemea pia kilimo kitaanguza kutokana na maamuzi hayo tuliyoyafanya. Sasa Serikali ifanye jambo moja, suala hili la mbolea liletwe hapa Bungeni kwa ukubwa wake tulijadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la katakata ya umeme ambayo haina utaratibu liletwe hapa Bungeni tulijadili kwa kina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.