Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi, na nianze kwa kumpongeza sana Mwenyekiti wa Kamati ya UKIMWI, Dawa za Kulevya na Magonjwa Yasiyoambukiza, Mheshimiwa Fatma Toufiq pamoja na Kamati yote kwa ujumla. Tunafanya nao kazi vizuri, na niseme tu kwa kweli maazimio yote saba ambayo wameyaleta katika taarifa yao, sisi Serikali tunayapokea yote kwa mikono miwili na tunahakikisha kwamba tunakwenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niseme tu katika kuchangia katika maazimio haya yaliyogawanyika katika maeneo matatu. Eneo la kwanza ni eneo la UKIMWI ambapo Kamati hii na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wanaonisikia, tumemaliza mkakati wa nne wa mapambano dhidi ya UKIMWI, na sasa tumetengeneza mkakati wa tano. Katika mkakati huu wa tano, msisitizo mkubwa utakuwa ni kutoa elimu juu ya kupima virusi vya UKIMWI pia kufuatilia VVU wale watoro, ufuasi wa dawa na tohara kwa wanaume. Hayo ni maeneo ambayo yatatiliwa mkazo mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni kuimarisha afua za udhibiti wa VVU na UKIMWI na hasa kwenye mikoa ile ambayo maambukizi yamefika asilimia zaidi ya 4.7.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni kutoa elimu kuhusu unyanyapaa na ukatili wa kijinsia ili kupunguza hofu kwa waathirika. Eneo lingine ni kujenga uwezo wa Kamati za UKIMWI na kuhakikisha kuwa Kamati hizi zinakuwa na uwezo na kuchukua hatua na kutoa ushauri unaostahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho katika eneo hili la UKIMWI ni kuhakikisha kuwa vituo vya kutoa huduma ya afya ya mama na mtoto vinatoa elimu pia kwa wamama wajawazito ili kuhakikisha kwamba maambukizi yale hayatoki kwa mama kwenda kwa mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni eneo la magonjwa yasiyoambukiza, ambapo hapa kulikuwa na azimio na azimio moja ambalo limesisitiza zaidi kwamba magonjwa haya ambayo hayaambukizi yanaweza tu kupungua pale ambapo elimu itatolewa kwa wananchi, na pia kuhimiza michezo shuleni. Sisi kwa ujumla tumepokea azimio hili na kazi kubwa ya Serikali ni kwenda kulitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni kuhusu Mamlaka ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya. Hapa yako maazimio mawili na msisitizo mkubwa umekuwa ni umuhimu wa kuhakikisha kwamba sera ya kudhibiti dawa za kulevya na mapambano dhidi ya dawa ya kulevya inatiliwa mkazo na kuhakikisha kwamba inakamilika. Niseme tu hatua za utayarishaji wa sera hii zimekamilika na sasa tuko katika kupeleka kwa wadau ili tuweze kupata maoni na baadaye sera hii itakuwa imekamilika. Nataka niwahakikishie Bunge na Kamati kwamba tuko katika hatua za mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia suala zima ambalo limezunguzwa hapa pamoja na michango ya Wabunge ni umuhimu wa kuweka waratibu wa masuala ya UKIMWI katika Halmashauri zetu za Wilaya. Dawa za kulevya hazina uratibu kule kwenye ngazi za chini. Kwa hiyo, maoni haya yaliyotolewa, nadhani hata kama siyo sehemu ya azimio lililosemwa katika maandishi, lakini ni jambo zuri la kulichukua na sisi Serikali nadhani ni administrative, ni kusema tu katika kwamba masuala ya UKIMWI na dawa za kulevya, tutajaribu kuliangalia katika Serikali tuone namna gani litakavyotekelezwa, lakini siyo jambo baya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilizungumzwa hapa juu ya mradi wa DHS ambao ulikuwa ni mpango ambao unafuatilia na kuangalia hali ya UKIMWI katika makundi mbalimbali. Mheshimiwa Mchafu amezungumza suala hili akasema haishirikishi watoto katika utafiti huu. Ni kweli, nadhani pengine ni upungufu. Tujaribu kuona kwa program hii ambayo kwa kweli inaisha na sasa tunakuja DHS nyingine, tutaangalia namna ambavyo tunaweza tuna- include suala la watoto kuingia katika utafiti huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Afya iko kwenye mchakato wa kuanzisha mpango mkubwa sana ambao utakuja na utafiti mkubwa katika mapambano dhidi ya UKIMWI na madhara yake. Kimsingi nao nadhani wamelichukua hili, tutashirikiana kwa sababu tunafanya kazi kwa pamoja kuhakikisha kwamba katika mpango unaokuja basi tunahakikisha na watoto wanaingia katika nafasi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Vinginevyo, naunga mkono hoja ya Kamati kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)