Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu. Nichukue pia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyetujalia kuona siku ya leo; lakini pia nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa inayofanyika kwenye Jimbo la Mbulu Mji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze na hoja chache. Mwaka huu wakati wa bajeti hii inayoendelea tuliletewa muhtasari wa mpango wa utekelezaji wa umeme vijini. Tulifurahishwa sana na huu mpango wakati ule ukiwa unaelezea jinsi ambavyo mpango huu utataekelezwa kwenye maeneo yetu, hasa miradi ya umeme. Tuna changamoto kubwa sana kule vijijini kwa sababu tunapofika muda fulani wa kuhitimisha Bunge hapa tunalazimika kwenda kule vijijini ili tuweze kuwaambia wananchi walau Serikali yetu ina mpango upi kwa upande wa kila sekta.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hoja yangu kubwa ni kwamba miradi hii ya REA Vijijini imekuwa michache na inasubiriwa sana na wananchi kwa jinsi ambavyo umeme ni nishati muhimu sana kwa maisha ya kila siku na kwa huduma mbali mbali za jamii. Kwa hiyo katika taarifa ambayo ninaijengea hoja muda huu ni taarifa ya utekelezaji wa mpango huu kwa sababu viko vijiji ambavyo havijafikiwa na umeme hadi sasa kwenye maeneo mbali mbali hususan Jimbo lile la Mbulu Mjini. Jimbo la Mbulu Mji lina vijiji na mitaa. Eneo la vijijini kuna vijiji ambavyo na kata hadi sasa umeme haujafika lakini mkandarasi ana miaka miwili. Ni kwa kiasi gani tunafuatilia utekelezaji huu wa mpango wa umeme vijijini? Na kwamba unafanyiwa tathmini inapofika muda fulani na wakandarasai wanaopewa hii kazi na REA nao wanafuatiliwa ili walau wanachi wapate huduma kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa iliyowasilishwa ya mpango huu ilitupa matumaini kwa sababu katika bilioni 2.705 ya fedha za Wizara hii, kama tulivyoambiwa kwamba hela nyingi za miradi, kwa asilimia karibia 99, ilikuwa ya fedha za ndani; pengine tumekwama huko. Hata hivyo, sasa wananchi kule vijijini hawajapata umeme. Mimi nilikuwa naishauri Serikali, kabla hatujaenda kwenye bajeti ya mwaka unaokuja, huu wa 2023/2024 kwanza tujitathmini hao wakandarasi wamefanya kazi zao kwa kiwango kilichokusudiwa na mipango kazi yao ilienda vizuri? Na kama haikwenda vizuri basi tujitathmini na kuona namna gani tunachukua hatua sasa ya kubadilisha utararibu ule wa kazi zilizoko kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, mkandarasi anatekeleza kwenye mikoa mitatu ndani ya miaka mitatu lakini hakuna eneo liliowasha umeme. Vilevile unakuta ni nguzo tu zimesimikwa, maeneo mengine hakuna nguzo na maeneo ya visima vya maji hakuna umeme, na maeneno mengine yanakosa umeme kwa sababu ya maeneo ya migodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikua naona kama inawezekana historia ya wakandarasi hawa itazamwe upya na hasa yule aliyepewa kazi Mkoa wa Manyara, kwa sababu bado tuna tatizo kwenye mkoa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine, ni eneo la ujazilishi. Kwenye taarifa hii ya Wizara, nitampatia Mheshimiwa Waziri baadaye; kuna maeneo ambayo tulitegemea sana, maeneo ya ujazilishi yanapata miradi lakini kwa bahati mbaya miradi hii ya ujanzilishaji haijaanza hadi sasa. Kwa hiyo, mimi nadhani pia tujikite kwenye utaratibu wa ujazilishi kwa sababu katika kijiji unakuta kuna kaya 20. Kaya zingine zote takriban 200 na kitu hazina umeme kwa sababu hatujaweza kusambaza kwenye vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa kuwa mpango wetu wa awali huu wa mwaka 2022/2023 ulikuwa unagusa maeneo ya ujazilishi, na huu mradi wa ujazilishi uje vizuri kwenye mpango unaokuja ili tuweze kufanikisha adha hii na njia hii ya huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni eneo la ruzuku ya Serikali kwenye mafuta. Tunaipongeza Serikali kwa mpango wake wa kuweka ruzuku kwenye mafuta, na tulitegemea itapunguza makali, na kwa sehemu imepunguza. Hata hivyo tunachoona mafuta yanaposhuka bei ya usafirishaji inabaki pale pale. Mafuta yanapopanda bei ya usafirishaji inabaki pale pale. Sasa hapo ndipo mwananchi mtumia huduma anajiuliza; ni kwa kiasi gani walau ruzuku yetu ya Serikali imekua na tija? Na kama ni kipindi cha tathmini hapo pia tunatakiwa tufanye tathmini ili tuweze kufanya utaratibu mzuri wa ruzuku uwe na tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kutokana na muda niseme pia, kwenye maeneo ya mijini na maeneo ya vijijini sasa hivi TANESCO wametowa utaratibu mpya wa umeme kwa 320,000 na umeme wa 27,000 ubaki kwenye maeneo ya vitongojini. Hata hivyo kwenye miji mingi, hasa Mji wa Mbulu, mitaa kumi ndiyo center ya mji, mitaa mingine 48 na vijiji 34 vilivyoko vijijini ni maeneno ya wananchi. Kwa hiyo, mimi nilikuwa nafikiri kwa kuwa tunajenga Bwawa la Mwalimu Nyerere, na tuwaombee viongozi wetu walioanzisha wazo hili; tuone utaratibu wa maeneo ya vijijini ni kwa namna gani basi umeme ule wa vijijini unarudi katika kiwango cha 27,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa jinsi tunavyokwenda kwenye baadhi ya mitaa na baadhi ya maeneo hata pembezoni mwa miji wananchi wengi hawataweza 320,000. Kwa hivyo kuna haja ya kuona kama tunajenga Bwawa la Mwalimu Nyerere na eneo hili la ujazilishi na eneo hili la uunganishwaji wa umeme litazamwe katika mpango wa bajeti unaokuja, ili kufanikisha taarifa nzima ya utaratibu ambao unaweza ukasaidia wananchi hao ambao tayari wengi wao wamefanya wiring. Tayari wengi wao wana hamu ya kuunganisha. Hata hivyo, wiring tu laki tatu na kitu mpaka laki nne, ukichanganya na laki tatu nyingine na ishirini hizo ni laki saba. Kwa hali ya kawaida ya mwananchi wa kijijini au mwananchi anayetegemea hiyo nishati, kwa kweli hataweza kuunganisha umeme kwa jinsi ambavyo uwezo wa mwananchi ulivyo na hali halisi ilivyo na hatuwezi kuwa na manufaa kwa umeme huu ambao sahizi tunajenga Bwawa la Mwalimu Nyerere. Lengo letu ni umeme uzalishe kwa kasi, lengo letu ni kuangalia kiasi gani wananchi wengi wanaunganisha umeme na wakishaunganisha umeme wanufaike na fursa hii ya kupata umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utaratibu huu wa kuangalia shughuli mbali mbali za miradi ya maendeleo tumekuwa na mipango mizuri sana, mipango ambayo tukienda kutafsiri kwa wananchi baadaye wanachi nao wanatuhoji mbona ule mpango wenu mlioutafsiri kwetu haujatekelezwa. Mimi nilikua nafikiri kama inashindikana wakati fulani tuanze na vipaumbele kama vinavyoainishwa kwenye Wizara mbali mbali na hasa hii Wizara ya Nishati ili mwisho wa siku tuweze kuona ni namna gani tunapata umeme kwa wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine; ni dhahiri wazi 2015 tulisema tutapeleka umeme kila kijiji na kila kitongoji 2020 kwenye…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)